DAR ES SALAAM
Na Edvesta Tarimo
Katika jamii nyingi, viatu vyenye kisigino kirefu vimejijengea nafasi ya kipekee kama alama ya urembo, hesima, hadhi na kujiamini kwa mwanamke. Kwa muda mrefu, kuvaa kiatu chenye kisigino kirefu kumechukuliwa kama sehemu ya mwonekano wa kitaaluma na kifahari, hususani katika mazingira ya kazi na hafla rasmi. Hata hivyo, nyuma ya mvuto huo wa nje, tafiti za kisayansi zinaendelea kuibua hoja nzito, kuhusu gharama ya kiafya inayoweza kujificha kwenye mtindo huu.
Kihistoria, kumbukumbu zinaonesha kuwa viatu vyenye kisigino havikuanza kama vazi la wanawake. Tafiti za kihistoria za mitindo zilizokusanywa na Fashion Institute of Technology, zinaonesha kuwa takribani mwaka 1000 BK, wanaume wa Uajemi waliokuwa wakipanda farasi, walitumia viatu vyenye kisigino, ili kuimarisha mshikamano wa mguu na farasi.