Na Pd. Richard Mjigwa, C.PP.S
Jalai 12, kila mwaka, Mama Kanisa huadhimisha Dominika ya Utume wa Bahari, ikiwa ni Siku ya kumwomba, kumtukuza, kumsifu na kumshukuru Mungu kwa huduma yao.
Hakika ni mchango mkubwa, unaotolewa na mabaharia hao, pamoja na wavuvi, kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.
Kwa kawaida, hiyo ni siku maalumu ya kutambua mchango na sadaka ya watu hao, ambao wakati mwingine, utu na heshima yao vinahatarishwa kutokana na changamoto mbalimbali, wanazokumbana nazo kila siku.
Utume wa Bahari, “Opus Apostolatus Maris”, unaojulikana na wengi kama “Stella Maris”, ulianzishwa tarehe 4 Oktoba 1920, na Waamini Walei wanaoshiriki: Ukuhani, Unabii na Ufalme wa Kristo Yesu, unaopata chimbuko lake kutoka katika Sakramenti ya Ubatizo.
Ni jukumu na wito wa Waamini Walei, kuutafuta Ufalme wa Mungu, unaosimikwa katika kweli na uzima; ni ufalme wa utakatifu na neema; ni ufalme wa haki, mapendo na amani; huku wakiyashughulikia mambo ya dunia, na kuyaelekeza kadiri ya mpango wa Mungu.
Waamini Walei wanaitwa kuyatimiza majukumu yao wenyewe, wakiongozwa na roho ya Kiinjili, ili kumtangaza na kumshuhudia Kristo Yesu kwa imani, matumaini na mapendo thabiti!
Ili kuonesha na kushuhudia ukaribu wa Kanisa kwa mabaharia, wavuvi pamoja na familia zao, Papa Pio XI, tarehe 17 Aprili 1922, aliridhia kuanzishwa kwa Utume wa Bahari “Opus Apostolatus Maris.” Leo hii kuna jeshi kubwa la watu, wanaojisadaka zaidi kuwadumia mabaharia na wavuvi, katika bandari 300 kwa kutembelea meli zisizopungua 70,000 kwa mwaka.
Mama Kanisa anawashukuru kwa dhati Mitume hawa, wanaoendelea kujisadaka bila ya kujibakiza, kwa ajili ya huduma makini kwa mabaharia, wavuvi pamoja na familia zao.
Wadau wa Utume wa Bahari, wamekuwa ni mashuhuda na vyombo vya uinjilishaji wa kina, kwa kuwafunulia watu wa Mungu, ile sura pendelevu ya Mama Kanisa, kwa kuonesha ukaribu wake kwa watu watakatifu wa Mungu, na hivyo kuwahamasisha kujisikia kuwa, ni sehemu hai ya Fumbo la Mwili wa Kristo yaani Kanisa.
Takribani miaka 100 iliyopita, Dominika ya Utume wa Bahari, imekuwa ni kipindi muafaka cha ujenzi wa misingi ya majadiliano ya kidini, kiekumene na kitamaduni, kutokana na mwingiliano wa watu kutoka katika dini, tamaduni na Mataifa mbalimbali duniani.
Papa Pio XI alitamani sana kuona kwamba, Utume wa Bahari unaendelezwa kwenye Bahari na fukwe mbalimbali za dunia. Roho Mtakatifu, kwa maombezi ya Bikira Maria, aendelee kupyaisha utume na huduma hii, mintarafu mahitaji ya ulimwengu mamboleo!
Kuna mabaharia ambao dhamiri zao zinahangaika sana, na mara nyingi Mapadri wa maisha ya kiroho, kwa mabaharia na wavuvi, wamekuwa ni msaada mkubwa.
Mabaharia ni watu wanaofanya kazi zao, katika mazingira magumu na hatarishi, mara nyingi nje ya nchi, makazi na familia zao!
Mapadri washauri wa kiroho katika muktadha kama huu, wanakuwa ni mashuhuda na vyombo vya Injili ya matumaini, kwa mabaharia na wavuvi waliopondeka na kuvunjika moyo! Mapadri wanapaswa kuwa ni watu wenye huruma, wapole na wanyenyekevu wanapowahudumia mabaharia, wavuvi pamoja na familia zao.
Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliwaletea historia ya kuibuka kwa Madhehebu mengine ya Kiprotestanti. Leo tunaendelea kuwaletea kuibuka kwa Madhehebu ya Kiprotestanti, hususani Uprotestanti chini ya John Calvin. Sasa endelea…
John Calvin 1509-1564:
Kati ya Waprotestanti waanzilishi, Calvin ndiye aliacha nyuma mafundisho ya msingi kwa Waprotestanti. Calvin alizalilwa mwaka 1509 huko Ufaransa. Alijifunza elimu dunia ya wakati huo (humanist), vilevile akajifunza Kilatini, Kiyunani na Sheria.
Mwaka 1533, anasema aliongoka na kuitikia wito wa Mungu kuwa “Chombo cha kutangaza ukweli”. Alipokea wito huo kwa moyo wake wote na kuanza kuhubiri.
Mwaka 1535, ilimbidi akimbie kutoka Ufaransa na kwenda Basle-Uswizi, kwa sababu ya upinzani dhidi ya mafundisho yake.
Akiwa Basle, Uswizi, aliandika mafundisho yake ya dini, Teologia, ambayo baadaye aliyaboresha. Ni muhimu kujua mafundisho haya ya Calvin, kwa sababu madhehebu mengi ya Kiprotestanti hata yale ambayo hayamkubali kama mwanzilishi wake, mafundisho yao yameingiliwa na teolojia yake.
Calvin kimsingi alifundisha yafuatayo:
1. Kwanza ya yote, Mungu ni mwenye mamlaka yote. Yeye ni Muumbaji, Mtegemezaji na Mtawala. Yeye yuko juu sana na mwenye uamuzi wote.
Yeye huamua anavyotaka, hana sheria inayombana. Hivyo, binadamu hawezi kuungana naye kama walivyofundisha watakatifu, bali la kufanya ni kujiweka chini ya utashi wake na maagizo yake. Kwa hilo alikuwa karibu na mafundisho ya Waislamu.
2. Alifundisha kwamba, tangu milele, watu wengine walipangiwa tayari kwenda mbinguni na wengine kwenda motoni (predestination). Mtu hawezi kufanya lolote kugeuza hilo.
Kwa wale waliopangiwa kwenda mbinguni, kuna ishara tatu za kuwatambua. (a) Kushika imani ya kweli (b) Maisha ya uadilifu (c) na kushiriki chakula cha Bwana.
Yeye na wafuasi wake, kwa sababu walikuwa na ishara hizo, ilikuwa ni wazi kwamba wamepangiwa mbinguni. Hapo mtu anaweza kusema “Nimeokoka” kwa sababu kama mtu amepangiwa kwenda mbinguni haiwezi kugeuka.
Mtu hana uhuru wa kutenda mabaya au mema, kwa sababu yeye ni mwovu, bali Kristo anamhesabia wokovu. Hata hivyo yule anayekosa lazima aadhibiwe kwa sababu hakulazimishwa na mtu kutenda mabaya.
3. Biblia ndio chanzo pekee cha ufunuo, na ishikwe na kufuatwa neno kwa neno kama ilivyoandikwa.
4. Kuna Kanisa lisiloonekana na Kanisa linaloonekana. Kanisa lisiloonekana, ni la wale wote waliopangiwa kwenda mbinguni, tangu mwanzo wa nyakati hadi mkamilisho wake. Kanisa linaloonekana ni la watu wale wanaotimiza masharti anayoyafundisha.
5. Anazitambua Sakramenti mbili tu Ubatizo na Ekaristi; lakini sakramenti hizo siyo za lazima kwa wokovu. Katika ibada mbalimbali, anakataza nyimbo, pawepo zaburi tu, vilevile anakataza ibada nzuri, hija, maandamano, sanamu nk.
6. Katika mafundisho yake alisisitiza sana juu ya umisionari. Alitayarisha watu ambao walikuwa tayari, bila kujali shida kwenda kuhubiri na kuwaongoa watu, kwa mafundisho yake.
Walifundisha vikundi na watu binafsi nyumba hadi nyumba.
7. Hawakumtambua Papa, Maaskofu au Mapadri. Kwao, kila mmoja aliyebatizwa ni Padri. Hivyo, kiongozi wa ibada huchaguliwa na watu, au huteuliwa na yeye na anaweza kumfukuza wakati wowote.
8. Kwake mwisho wa dunia, uko mbali, hivyo lazima binadamu afanye kazi sana na kuendeleza ulimwengu. Faida inayopatikana katika kazi hiyo, isitumike kwa anasa na starehe, bali iwekezwe au kusaidia maskini.
Hii iliwapa Waprotestanti, nguvu za kipesa na kuhamasisha ubepari. Hadi leo Waprotestanti wanajua biashara, kuwekeza na kuzalisha kuliko Wakatoliki.
VATICAN CITY
Wakristo wameitwa kuleta chachu ya ukarimu kwa ulimwengu, hasa katika ulimwengu unaoathiriwa kila mara na mantiki ya ubinafsi, huku wakifikiria na kuishi kulingana na mantiki ya kweli zaidi, ile ya ukuaji fungamani wa mwanadamu.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Leo XIV, huku akiwaelekea Waamini katika kituo cha IFEMA, Madrid, ikiwa ni hotuba yake ya mwisho, kabla ya kuanza sehemu ya Pili ya ziara yake ya kitume nchini Hispania.
Hitaji la kufikiria na kuishi, kulingana na mantiki ya maendeleo fungamani ya binadamu, limesikika katika hotuba ya Baba Mtakatifu Leo XIV, akihitimisha hija yake mjini Madrid, kwa kukutana na watu wa kujitolea 17,000, katika Ukumbi wa 3 wa IFEMA, kabla ya kupanda Ndege kuelekea kwenye Mji wa Barcelona, ikiwa ni sehemu yake ya Pili ya ziara ya 4 ya Kitume nchini Hispania, iliyoanza tangu Juni 6 na kuhitimishwa Juni 12, kwa kutembelea pia Visiwa vya Kanari na Tenerife.
Banda hilo la 3 ni moja ya taasisi tano muhimu zaidi, za maonyesho ya biashara barani Ulaya, moja kuu nchini Hispania, ambapo alifika kwa gari katikati ya watu wa kujitolea, waliotambulika kwa rangi ya machungwa.
Katika hotuba yake Askofu huyo wa Roma, alianza na shukrani kwa Mwadhama José Kardinali Cobo Cano, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Madrid, kwa kaka na dada wapendwa katika Jimbo hilo.
Hapa wote walisikika wakitoa ukelele wa kusikitika, na Papa akaendelea. “Kila mmoja wenu na wengine wengi, ambao hawakuweza kuwa hapa asubuhi ya leo, wanastahili “shukrani” maalumu sana, kwa sababu mmetoa uwepo wenu na huduma yenu, na mmefanya hivyo kwa upendo kwa Bwana, Kanisa na Papa.”
Na Pd. Gaston George Mkude
Amani na Salama!
Injili ya leo, tunakutana na Yesu mbele ya makutano, waliokuwa wamechoka na kutawanyika. Makutano si tu wanawakilisha watu wa nyakati zile za Yesu, bali hata katika siku zetu leo hii.
Ni watu wangapi leo wanapitia magumu na mahangaiko, pamoja na mateso ya kila namna, labda hata baadhi yetu tumechoka, na kutawanyika kama kondoo tusio na mchungaji.
Wangapi leo wanaishi maisha yenye kila majeraha na maumivu! Wangapi leo wamechoka kimwili, kiakili na hata kiroho, kiasi cha kutawanyika na hata kutangatanga kiimani.
Wapo wanaokwenda kila siku, kwa wanaojiita mitume na manabii, na wengine kwa waganga wa kienyeji na wapiga ramli! Yesu anamuona kila mmoja wetu, na moja tu kutoka kwake, anatuhurumia!
Labda mara nyingi tunajiuliza, kwanini Mungu aliye upendo na huruma, anaruhusu wana na watoto wake tupitie magumu kiasi hicho?
Je, Mungu hawezi kutukinga na mateso na magumu? Au je, Mungu hatupendi hata anatuacha tukipitia kikombe hicho cha mateso na mahangaiko?
Ni maswali msingi na ya haki kabisa, kutuingiza katika tafakari ya fumbo la mateso, katika maisha ya ufuasi wetu.
Ni katika Injili ya leo, tunaona Yesu anapokutana na makutano wale, hata anapokutana nasi katika hali ngumu na taabu, anajawa na moyo wa huruma.
Yesu alipowaona, aliwahurumia! Huruma kama alivyokuwa anatukumbusha daima, hayati Baba Mtakatifu Fransisko, ndio haswa sura na utambulisho halisi wa Mungu wetu.
Mungu ni upendo na huruma! Papa Fransisko daima alipenda kurudiarudia na kusema ni sisi tunaochoka kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu, kwani Mungu kamwe hachoki kutuhurumia na kutukumbatia tena na tena!
Shime katika kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu! Jina na utambulisho wa Mungu ni Huruma!
Nabii Isaya anapotambulisha wema na huruma ya Mungu, anajaribu kutuonesha Mungu anatupenda zaidi ya mama anavyopenda watoto wake.
Sisi ni watoto wa Mungu kwa nafasi ya kwanza, na hivyo Mungu kwetu anajifunua kama upendo na huruma. (Isaya 49:14-16).
Na Mwandishi Maalumu
Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, ameitaka Hispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana, katika utamaduni ili hatimaye, kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini.
Katika hotuba yake hiyo, Papa alikazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kuongozwa na kauli mbiu ya Umoja wa Ulaya umoja katika utofauti, mambo yanayounda amana na utajiri wa watu wa Mungu.
Hija hiyo ya 4 ya Kitume nchini Hispania imebebwa na kauli mbiu: “Alzad la mirada” Yaani “Inueni macho yenu.” Yn 4:35.
Baba Mtakatifu Leo XIV, alikutana na Waziri mkuu wa Hispania Pedro Sánchez Pérez-Castejón, ambaye amekuwa madarakani tangu Juni 2, 2018 na ndiye kiongozi mkuu wa Serikali ya Hispania.
Papa pia amekutana na kuzungumza na Bunge la Hispania na baadaye amepata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania na baadaye jioni wakakutana kwa sala na Ibada kwa Bikira Maria Mama wa Almudena “Santa María de la Almudena” ambaye ni Mlinzi na Mwombezi wa Jimbo kuu la Madrid, Hispania na kila mwaka ifikapo Novemba, 9, mwaka huu, anakumbukwa na Mama Kanisa nchini Hispania. Baadaye usiku, Baba Mtakatifu Leo XIV amekutana na kuzungumza na Jumuiya ya Jimbo kuu la Madrid, Hispania, Waswahili wanasema, siku hii ilikuwa “full shangwe.”
Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, ameitaka Hispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana, katika utamaduni ili hatimaye, kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini.
Amekazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kuongozwa na kauli mbiu ya Umoja wa Ulaya “In varietate concordia” yaani “Umoja katika Utofauti” kwa kusimikwa katika tofauti za tamaduni, mapokeo na vipaumbele tofauti; mambo ambayo kwa pamoja yanaunda amana na utajiri mkubwa wa watu wa Mungu nchini Hispania.
Mama Kanisa anatembea bega kwa bega na binadamu, anashiriki matumaini na madonda yake, anaendelea kusikiliza na kujibu maswali msingi ya binadamu wa kila nyakati na kwamba, kuna tofauti ya utendaji kati ya Kanisa na Serikali; na kwamba, utu, heshima na haki msingi za binadamu ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kuzingatia kwamba, uhuru ni zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu.
Na Dk. Philip Komba
inaadhimishwa ifikapo Juni 3, kila mwaka nchini Uganda, na inakumbusha sadaka ya watu kadhaa, kutoka mahakama ya Mfalme Mwanga II, waliouawa kati ya mwaka 1885 na 1887, kwa kubadili dini na kuwa Wakristo.
Dini hiyo, Mfalme aliiona kama tishio kwa mila za kikabila, na kikwazo cha maisha yake.
Hivyo, kutokana na hilo, Papa Paulo VI mwaka 1969, huko Kampala nchini Uganda, akihutubia Bunge alisema kwamba: “Ninyi Waafrika mnajua maana kubwa ya jumuiya, ni mojawapo ya sifa zenu nzuri na za kibinadamu.”
Kundi la watumishi 22 Wakatoliki (karibu wote ni Waganda), wa mahakama ya Mfalme (Kabaka) Mwanga II wa Buganda, ambao Mama Kanisa aliwatangaza kuwa Watakatifu, waliteswa sana na baadaye kuuawa kishahidi kati ya 1885 na 1887, kwa kutetea imani yao ya kidini.
Watu wengine 150 walikufa katika mapigano kati ya vikundi tofauti, vilivyohusishwa na ushawishi wa wamisionari Wakatoliki au Waprotestanti, na wafanyabiashara wa Kiswahili au Wamisri.
Kifo cha kwanza cha shahidi mnamo Januari 1885, kilifuatiwa mnamo Oktoba, na kile cha Askofu wa Kiingereza J. Hannington na Joseph Mukasa Balikuddembe. Kundi la Waislamu lilimshawishi Mwanga, kuhusu kuhusika kwa Wakristo katika kuchomwa moto, kwa eneo la kifalme (1886), na kwa hiyo ukatili wa mfululizo mpya wa mauaji, uliwashtua sana viongozi wasio Wakristo, kiasi kwamba walizuia mauaji zaidi na hata kusababisha ongezeko la ubatizo. Mashahidi 22 Wakatoliki, walitangazwa kuwa Watakatifu mnamo 1964 na Papa Paulo XIV, ambaye pia alifanya ziara ya Kitume nchini Uganda.
Mtakatifu Paulo VI, alitimiza ziara hiyo kuanzia tarehe 13 Julai hadi tarehe 2 Agosti 1969. Ziara hiyo ya Uganda mara nyingi, imekumbukwa kwa kutia moyo Kanisa changa la Afrika, kukua katika ukomavu, kwa ajili ya kukuza ubinadamu na kwa ajili ya kutafuta amani.
Papa Mtakatifu akikutana na baadhi ya Waamini wa Kiislamu, katika Ubalozi wa Vatican mjini Kampala alieleza kuwa:
“Tuna uhakika wa kuwa katika ushirika nanyi, tunapomwomba Mwenyezi Mungu, aamshe mioyoni mwa Waamini wote barani Afrika, hamu ya upatanisho na msamaha, ambayo mara nyingi hupendekezwa katika Injili na Kurani.
Na tunawezaje kushindwa kuhusisha na ushuhuda wa uchamungu, na uaminifu wa mashahidi Wakatoliki na Waprotestanti, kumbukumbu ya wale wanaoungama imani ya Kiislamu, ambao historia yao inatukumbusha kwamba, walikuwa wa kwanza mnamo 1848, kulipa kwa maisha yao kwa kukataa kukiuka maagizo ya dini yao?”
Hotuba ya Papa Paulo XIV kwa Uganda
Ndugu msikilizaji na msomaji, vilevile Mtakatifu Paulo VI akikutana na Rais, Mamlaka za kiraia na kikosi cha Kidiplomasia cha Uganda, katika Ukumbi wa Bunge huko Kampala tarehe 1 Agosti 1969, wakati wa hija yake ya kitume alitoa hotuba yake.
Katika muktadha huu wa maadhimisho ya Mashahidi, tunapenda kukumbusha hotuba hii ya Kinabii, katika ziara yake ya kwanza barani Afrika. Maono yake na utabiri wake, ulikuwa kama wa watangulizi wake, na wale ambao walifuata hadi leo hii. Mapapa wote kilio ni kimoja. Katika ulimwengu uliogawanyika vipande vipande na vita, unahitaji amani, haki na usawa.
Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliendelea kuwaletea historia ya Uasi wa Martin Luther na historia ya maisha yake ya uasi.
Leo tunaendelea kuwaletea historia ya uasi wa Luteri hata kwa Shirika lake, na mafundisho yake ya dini. Sasa endelea…
Februari 3, mwaka 1518, Luteri aliitwa na Mkutano Mkuu wa Shirika lake, lakini kwa kulindwa na Frederick, hakuudhiwa na hata ndugu zake wengine shirikani walimshangilia.
Tarehe 16/05/1518, Luteri akiogopa kutengwa na Kanisa, alihubiri akipinga uwezo wa Papa kumtenga Mkristo.
Hapo Papa alimwita afike Roma kwa hukumu, lakini Frederick wa Saxony, aliweza kumfanya Papa akubali, asikilizwe huko huko Ujerumani na Kardinali Kajetani.
Luteri alikataa kuacha uzushi, na baadaye akakimbilia kwa Frederick asikamatwe. Bahati mbaya Papa hakufanya lolote, akihofia kupoteza urafiki wa Frederick.
Mambo yalifikia kilele mwaka 1519, Luteri alipobishana na Mdominikani makini sana John Eck, aliyemzidi akili na utundu.
Kabla ya hapo, Luteri alikuwa akijificha katika maneno magumu ya teolojia, lakini sasa ilibidi aseme wazi, kujibu maswali makali ya John Eck.
Pale alikiri, mawazo yake na kusema kwamba, siyo tu Papa lakini hata Mtaguso Mkuu, unaweza kufanya makosa na mtu binafsi akaupinga.
Sasa ikawa wazi kwamba, ni mzushi na vyuo vikuu vikubwa vikamkana kama mzushi. Ni tokea wakati huo, sasa Luteri akahesabika rasmi kama mzushi katika Kanisa.
Tarehe 15/06/1520, Papa Leo X, alituma hukumu ya kumtenga na Kanisa kwa Luteri, akimpa siku 60 akane uzushi.
Luteri badala ya kukana uzushi, akaichoma ile hukumu hadharani, kama dharau kwa Papa. Mwaka 1521, aliitwa na Mfalme Mkuu Karoli V, kukana uzushi na alipokataa alihukumiwa, lakini akakimbizwa na Frederick na kufichwa.
Wakati huo, ambapo Mfalme Mkuu Karoli angefuatilia kwa matendo, ilimbidi aondoke haraka kurudi Hispania kwa shida maalumu.
Hispania ilikuwa ikigombana na Ufaransa, na wakati huo huo Waturuki walitaka kuiteka Ulaya. Mfalme Mkuu Karoli, hakuweza kurudi Ujerumani mpaka baada ya miaka 9, yaani mwaka 1530.
Katika muda huo, Luteri aliachwa kueneza mafundisho yake, kwa sababu hakuna mwingine ambaye angelimsema au kumshika, kwa sababu alilindwa na Frederick wa Saxony.
DAR ES SALAAM
Na Edvesta Tarimo
Katika jamii nyingi, viatu vyenye kisigino kirefu vimejijengea nafasi ya kipekee kama alama ya urembo, hesima, hadhi na kujiamini kwa mwanamke. Kwa muda mrefu, kuvaa kiatu chenye kisigino kirefu kumechukuliwa kama sehemu ya mwonekano wa kitaaluma na kifahari, hususani katika mazingira ya kazi na hafla rasmi. Hata hivyo, nyuma ya mvuto huo wa nje, tafiti za kisayansi zinaendelea kuibua hoja nzito, kuhusu gharama ya kiafya inayoweza kujificha kwenye mtindo huu.
Kihistoria, kumbukumbu zinaonesha kuwa viatu vyenye kisigino havikuanza kama vazi la wanawake. Tafiti za kihistoria za mitindo zilizokusanywa na Fashion Institute of Technology, zinaonesha kuwa takribani mwaka 1000 BK, wanaume wa Uajemi waliokuwa wakipanda farasi, walitumia viatu vyenye kisigino, ili kuimarisha mshikamano wa mguu na farasi.
DAR ES SALAAM
Na David Mpangile
Ili kutimiza wajibu wao Wakristo, ikiwa ni sehemu ya matunda ya ubatizo, Waamini hujaliwa karama mbalimbali.
Mafundisho ya Kanisa yanasisitiza kuwa karama yoyote itokayo kwa Roho Mtakatifu, yafaa katika kumsaidia mwamini katika safari yake ya kuutafuta utakatifu.
Karama hiyo pia inaweza kuchangia katika ustawi wa Kanisa, na ni msaada kwa ndugu wengine katika Kristo. Hivyo ni makosa kuacha kuitumia. Hata hivyo, bado kuna kishawishi cha Walei wengi kushindwa kutumia vipawa walivyo navyo, kwa sababu wanatafsiri kwamba karama ni zile tu zinazohesabika kuwa kubwa, kama vile kutenda miujiza na kunena kwa lugha.
Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliendelea kuwaletea historia ya Papa Gregori Mkuu, ambaye alikuwa Baba wa Kanisa wa mwisho na kiungo kati ya dola ya Kirumi ya zamani na ulimwengu mpya wa kishenzi. Leo tunawaletea historia ya maisha ya Mtume Muhammad na mwanzo wa Uislamu. Sasa endelea…
Maisha ya Muhammad:
Katika kipindi cha ghasia na uvamizi wa Ulaya, ndipo Muhammad alizaliwa mwaka 570. Wazazi wake walikufa akabakia yatima na akalelewa na baba mdogo. Akiwa kijana alifanya kazi katika misafara ya ngamia ya mjane mmoja tajiri aliyeitwa Khadija.
Alifanya kazi vizuri, hata baadaye Khadija alimfanya Muhammad kuwa Mkuu wa misafara yake. Muhammad akiwa na umri wa miaka 25, alimwoa mwajiri wake Khadija aliyekuwa na miaka 35. Ndoa yao ilikuwa nzuri na ilidumu.
Mwanza
Na Paul Charles Mabuga
Simulizi ya Amos Katama (sasa marehemu) ni kioo cha maumivu ya kizazi kizima. Kauli yake kuhusu “soli ya 20 ya kiatu kuchakaa akitafuta ajira” si dhihaka, bali ni kovu la kisaikolojia linalowatafuna wahitimu wengi. Amos aliondoka duniani akiwa na Shahada ya Uandishi wa Habari mkononi, lakini mfuko ukiwa mtupu. Hali hii inatufanya tujiulize: Je, vyuo vyetu vinazalisha wasomi au vinazalisha watafuta kazi waliofungwa pingu za kifikra?
Na Askofu Mstaafu Method Kilaini
Wahuni:
Wahuni walikuwa wapiganaji wakali sana, na ndio walioleta matatizo yaliyozusha uvamizi. Wahuni walikuwa watu wa Mashariki ya mbali (Mongoliani, waasia wa ngozi ya njano). Wahuni walikuwa wachungaji wakiishi Kaskazini ya Milima ya Himalaya.
Malisho yalipoisha, hawa wapanda farasi, walianza kuvamia nchi nyingine. Mwaka 200 Baada ya Kristo (BK), walikwea ukuta wakaivamia China na kusambaratisha himaya yake, na tangu hapo ikawa nyakati za giza kwa miaka 400 iliyofuata kwa China.
MWANZA
Na Paul Mabuga
Mjadala wa “Uswahili ni nini”, uliibuliwa hivi karibuni na mchambuzi Maggid Mjengwa, akirejea fikra za Jenerali Twaha Ulimwengu na marehemu Edwin Mtei.
Swali hili limezua taharuki chanya: Je, Mswahili ni nani katika ulimwengu wa leo? Je, bado ni yule “muongo muongo” aliyemchukiza Mtei, au ni utambulisho uliopata sura mpya, kuanzia mitaa ya Dar es Salaam hadi jijini Berlin?
Jenerali Ulimwengu, akizungumza hivi karibuni, katika makiwa ya marehemu Edwin Mtei, alifungua ukurasa wa kumbukumbu uliosisimua wengi.
Alieleza kuwa Mzee Mtei alikuwa na msimamo usioyumba, dhidi ya kile alichokiita “Uswahili.” Katika muktadha wa kujiuzulu kwake Uwaziri, Mtei aliamini kuwa mfumo wa “Uswahili”, ulikuwa kikwazo kwa uadilifu wa kitaifa.
Na Mwandishi Wetu
Katika makala haya kuhusu Ubatizo wa Bwana, Mwadhama Protace Kardinali Rugambwa katika mahubiri yake, ametumia fursa hii kufafanua alama muhimu, zilizojionesha wakati Kristo Yesu alipobatizwa mtoni Yordani.
Anasema kwamba alama ya kwanza ni Maji: Alama ya kifo na uhai; Mbingu zikamfunukia, Roho Mtakatifu akashuka juu yake kama hua; Alama ya pili ni kufunguka kwa mbingu; Alama ya mabadiliko ya ndani ya mwanadamu, mbele ya Mwenyezi Mungu; Alama ya tatu ni Roho Mtakatifu aliyemshukia Kristo Yesu na sauti ya Baba wa milele ikasikika: Huyu ni mwanangu, mpendwa wangu.
Ubatizo ni sakramenti inayotuingiza katika Ukristo, ni sakramenti inayotuondolea dhambi ya asili na adhabu zake zote. Ni kwa njia ya Ubatizo tunazaliwa upya kwa maji na Roho Mtakatifu, na hivyo tunakuwa ni watoto wa Mungu na wa Kanisa.