Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha
Makala

Makala (25)

MWANZA

Na Paul Mabuga

Upepo unavuma katika jua la saa nane, na miti iliyo karibu inatoa ukinzani,  hali hii inazalisha mvumo ulio sawa na wimbo mzuri unaopigwa kwa ala tupu! Hakika, hali hii ingeweza kuwa ya kufurahisha, lakini la hasha! Aron Malifweda [48], [siyo jina lake halisi kwa sababu za kitaaluma], zaidi ya kutafakari kila swali analoulizwa kwa ajili ya makala haya, huku akiwa ameketi kiambazani kwenye nyumba yake iliyo kwenye moja ya miji mdogo kanda ziwa, ni kama haoni wala kusikia kingine cha ziada katika mazingira yake.
Ni kwa sababu amechanganyikiwa na kuzama katika fikra zisizo na msaada wala  ufumbuzi, anaona ni kama ametengwa na jamii yake kutokana na hali aliyonayo, anachokitamani anaona kama ananyimwa, na hivyo kukata tamaa.
Alitaka awe na  watoto, ikashindikana kwa nguvu za kiume [syo rijali]. Lakini sasa anataka kuasili mtoto anakayerithi mali zake, lakini amepewa sharti, kwamba ni  lazima aoe na kuishi na mke.
“Unajua nimehangaika kwa  miaka mingi, iwe kwa madaktari hospitali, ama tiba asilia, lakini sikufanikiwa. Baadaye daktari mmoja ninayemwamini akaniambia kwamba siwezi kuondokana na hali hiyo nilipata huzuni sana siku hiyo, na nikaona dunia yote imeniangukia.
Nikifikira maisha ya kukaa bila mke wala watoto, nilikiona hata kifo kinaninyemelea! Nimehangaika hivii kwa zaidi ya miaka 15,” anasema Malifwedha, wakati akisimulia kisa chake cha sharti la kuhifadhiwa utambulisho.
Anasema kuwa kama suluhisho katika hilo, alishauriwa na daktari huyo kwamba atafute mtoto wa kuasili ndiye atakayekuwa  mrithi wa mali zake, jambo ambalo anaeleza kuwa  awali lilikuwa gumu, kwani wapo waliomkatisha tamaa kwa kumtishia kuwa anaweza kupata kijana, akamlea, lakini baadaye atakapokua, asimjali na kumkimbia akirejea katika familia yake ya uzao wa kibayolojia.
“Walikuwa wananiambia, Unaweza kupata mtoto wa kuasili na kumsomesha, lakini akifika chuo kikuu, akakukumbia na kukutelekeza,” anasimulia Malifwedha na kuongeza kuwa, “Baada ya ushauri wa Maafisa Ustawi wa Jamii katika eneo langu, nilipata moyo wa kuanza mchakato wa kupata mtoto wa kuasili, ambao. Licha ya jambo kwenda vyema, lakini sasa nimefikia pahala umekwama kutokana na sharti nililopewa, kwamba ni lazima nioe!”
Kwa mujibu wa Tovuti ya Wakala wa Uzazi na Vifo, kuasili watoto ni mchakato wa kisheria ambao huhamisha uwajibikaji wa mzazi kutoka kwa wazazi wa kuzaliwa kwa watoto, kwenda kwa wazazi  wa kuwalea. Kuasili mtoto kunaongozwa na sheria  ya kuasili mtoto, Sura Namba 335 Toleo la Mwaka 2002.
Na kwa mujibu wa sheria hiyo, mara mtoto anapoasiliwa, basi unajengwa uhusiano wa kudumu na wa moja kwa maoja kati yake na wazazi waliomuasili, na kwamba haki zote kutoka kwa wazazi wake wa kibayolojia [wa damu] zinafutika na kuhamia katika familia yake mpya. Pia, Wazazi wa damu nao haki zao kwa mtoto aliyeailiwa, nazo zinakoma.
Tukirejea kwa Malifedha, anaeleza kuwa baada ya kupata mtoto wa kuasili, na wazazi wake wa damu kutoa ridhaa chini ya usimamizi wa Maafisa Ustawi wa Jamii, na uchumguzi wa kina kufanyika katika kipindi cha miezi sita, alijaza fomu mbali mbali na taarifa za ufuatiliaji zikaandikwa, tena zikionesha kwamba ana mwenendo mzuri, na ana uwezo wa kuasili.
Bila shaka mchakato kama huu, kulingana na taratibu, baadaye ulihitaji idhinisho la mamlaka ya juu ya Ustawi wa Jamii. Kutoka hapo, hoja hupelekwa mahakamani mbele ya jaji, na  kama kutakuwa na kukidhi matakwa ya kisheria, basi, hutolewa amri ya kuasili, na mchakato huwa umekamilika. Hata hivyo, katika muda wote Maafisa Ustawi wa Jamii huendelea kufuatilia ustawi na maslahi ya mtoto.
Pengine kilichoonekana kuwa ni kikwazo kwa Malifwedha kwa mujibu wa sheria hiyo, ni kwamba mzazi wa kiume anayeishi pake yake haruhusiwi kumuasili mtoto wa kike, ama vingunevyo kuwe na mazingira mahsusi! Ingawaje hata huvyo  anaruhusiwa kuasili mtoto wake wa kiume. Na pia, kuwe na tofauti ya umri wa miaka  isiyopungua 21 kati ya mzazi anayeasili, na mtoto anayeasiliwa.
Tena basi, inaelekezwa katika kanuni za sheria hiyo kwamba katika mazingita yanayofaa, mtoto aliyeasiliwa, atakapofikisha umri wa miaka 14, ataelezwa hali ya kuasiliwa kwake na maafisa ustawi wa jamii katika eneo husika.
Kuhusu suala na kuoa Malifwedha anasema, “Nilikwenda kwa wanasheria, wakaniambia kuwa huyo mwanamke nikimuoa, atakuwa na haki zote kama mke kwenye mali zangu, hata kama itakuwa ni ndoa ya kudanganyia ili tu nipate kibali cha kuasili! Hilo nalo nkaliona gumu. Nikashauriwa niende kwa Wakurya,  eti huko ukioa mwanamke aliyezalia nyumbani, na ukishatioa mahari, watoto wanakuwa mali yako.”
Sadick Hunga ambaye ni Mwandishi wa Habari anayefanya kazi zake Mkoani Mara, na ambaye ni mmoja wa wanajumuia ya Wakurya wanaoishi Mkoani humo,  anasema katika mahojiano kwa njia ya simu kwamba, mila hiyo ipo katika jamii yake na imeendelea kuwepo, kwamba katika jamii hiyo, wakati wote watoto huwa ni mali ya mwanaume aliyelipa mahari.
“Huyu jamaa sisi tunamuambia karibu ‘tata’ [baba]! Yaani huku kwetu, kama mwanamke amezalia nyumbani, akaja mwanaume kumuoa, analipa mahali ya mke, mathalani ng’ombe sita, lakini baadaye atatakuwa kuwalipia watoto mahari nyingine inayoitwa ‘kuborora’, ambayo inaweza kufikia hadi ng’ombe wawili kwa kila mtoto, na kutokea hapo watoto hao wanakuwa mali yake daima dumu, hata wana umri mkubwa namna gani,” anasema Hunga.
Katika mtazamo mwingine Hunga anasema kuwa miongoni mwa jamii ya Wakurya, ikiwa mwanamke ameachana na mume wake, na  ikatokea akaolewa na mwanaume mwingine, basi, watoto wote watakaozaliwa katika familia mpya ni mali ya yule mume wa awali, “na hii imetokea majuzi huko Serengeti! Itaondoka tu ikiwa mume mpya atalipa mahari kurejesha iliyokwishakulipwa kabla.”
Wakati hali ikiwa hivi, Malifwedha bado yupo njia panda juu ya nini akifanye ili kukabiliana na hali hii, kwani ana malalamikio mengine. Anadai kwamba ndugu zake wanamtenga na hususan yanapokuja matukio kama harusi huwa hashirikishwi, na hilo linamuongezea mawazo! “Yaani utasikia tu kuna harusi huko, lakini hushirikishwi, huwa najiuliza, sijui wananionaje,” anasema.
Kuna changamoto nyingine pia, kwani Malifwedha akifikisha umri wa miaka 50, yaani katika kipindi cha miaka miwili ijayo, kwani suala la kuasili litakuwa na kipingamizi, kwani halitakuwa katika maslahi ya mtoto, na hususani katika maendeleo na makuzi yake. Na itakuwa ni kazi kubwa kujenga hoja dhidi ya pingamizi kama hizi kulingana na kanuni za kuasili.
Mrumbi wa masuala ya ndoa na muendeshaji wa kipindi cha ‘Ndoa Aminifu’ cha Runinga ya Tumaini, Paschal Maziku, anasema kwamba ndoa katika Kanisa Katoliki huwa ni kwa ajili ya manufaa ya wanandoa wenyewe, watoto wanaowalea na jamii kwa ujumla, na wala siyo kwa manufaa binafsi kama ilivyo katika jambo hili katika makala haya.
“Isitoshe, huyu bwana hawezi kuwa na ndoa, kwani ndoa huwa kati ya mwanamke na mwanaume rijali. Sasa jamaa na hali aliyonayo, haiwezekani, maana ndoa ili  ikamilike inahitaji kuwa ‘consummated’ [tendo la ndoa kufanyika ndani ya muda unaovumilia kwa busara ana kupatilizwa], kinyume na hapo inavunjwa”
Kuhusu, kuasili watoto, Maziku anasema, huko ni sawa na mtoto kuwa ‘displaced’ [kuwa pasipostahili],  na kwamba, “ni vema tukarejea katika mila zetu, kama ni yatima ama ana mazingira magumu, basi ndugu wa karibu, wajomba, mathalani baba wadogo na wengine, wachukue majukumu yao.”

Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliawaletea mada ya historia ya jinsi Uinjilishaji ulivyoingia nchi za Ethiopia, Eritrea na Somalia. Leo tunaendelea na historia ya Uinjilishaji katika nchi za Maghreb.. Sasa endelea…

Katika Kiarabu, nchi za Magharibi mwa Misri huitwa ‘Maghreb’. Nchi hizi ni pamoja na Libya, Tunisia, Algeria na Morroco. Zamani nchi hizi, hasa kwenye mwambao, zilikuwa za Kikristu hadi zilipotekwa na Waislamu katika karne ya saba. Pole pole Ukristo uligandamizwa na kupotea.
Ufaransa iliteka Algiers mwaka 1830 na kufanya Algeria nzima koloni lake, baadaye waliteka Tunisia mwaka 1881 na Morocco mwaka 1912. Libya ilitekwa na Waitaliani mwaka 1912 na kuipoteza kwa Waigereza wakati wa Vita Vikuu vya Pili, mwaka 1942.
Wakati wa ukoloni, Wakristo walikuwa na uhuru wa kuinjilisha, na waliongezeka hadi kufikia milioni moja na nusu. Hata hivyo, hawakuwa na mafanikio makubwa kati ya Waarabu Waislamu. Wengi wa waumini wao walikuwa Wazungu waliohamia kule.
Waarabu walioongoka hawakuzidi 10,000. Utume katika nchi hizo ulifanywa hasa na Wamisionari wa Afrika (Mapadre Weupe) waliokuwa na Makao Makuu yao kule Algiers, Algeria.
Utume wao mkubwa ulikuwa utume wa kuwepo kwa kuonyesha mfano na kufanya matendo mema. Walianzisha vyuo vya kujifunza lugha ya Kiarabu na Uislamu kwa wageni.
Mmisionari mwingine alikuwa Charles de Foucard aliyeanzisha Mabruda na Masista Wadogo wa Yesu. Wao wanajaribu kuishi katikati ya watu na kufanya kazi pamoja nao katika viwanda na sehemu nyingine.
Nchi za Maghreb zilipopata uhuru wake, Wazungu karibu wote bila kungoja kufukuzwa, walirudi Ulaya. Kadri siku zilivyopita, nchi hizi ziliweka sheria ngumu ya kuwabana Wakristo, na hivyo hata Wakristo Waarabu walikimbilia Ulaya na kufanya kazi huko. Hivyo katika nchi za Maghreb hadi leo, Ukristo ni kama haupo.
MOROCCO
Morocco ilipata uhuru wake bila matatizo mwaka 1956. Ingawa iliwekwa sheria ya kukataza Waislamu kuongoka kuwa Wakristo, uhusiano na Kanisa ulibaki mzuri. Tangu mwaka 1952 kuna monasteri ya Wabenediktini inayoendesha semina hasa juu ya Mahusiano ya Dini mbalimbali. Kati ya wakazi milioni 31, Wakristo ni asilimia 0.5, na Wakatoliki ni asilimia 0.2 tu.
ALGERIA
Algeria ilipata uhuru wake mwaka 1962 baada ya vita vikali vilivyodumu miaka 8. Kwa sababu wakati wa vita, Askofu Mkatoliki Etienne Duval alitetea haki za wazawa, baada ya uhuru Kanisa liliheshimiwa.
Hata hivyo, Wakatoliki 800,000 waliondoka wakabaki 80,000 tu. Ila, Mapadre na Watawa walibaki kuwahudumia watu bila ubaguzi. Kati ya wakazi milioni 34, Wakristo ni asilimia 0.9 na Wakatoliki ni asilimia 0.6 tu. Kuna majimbo manne, Mapadre 62 na Watawa wanawake 116.
TUNISIA
Tunisia ilipopata uhuru mwaka 1956, kwa makubaliano kati ya serikali ya Kiislamu na Wamisionari wa Afrika, alama na mambo mengi ya Kikristo katika mji wa Tunis yaliondolewa.
Kwa mfano, sanamu ya mwanzilishi wa shirika iliyokuwa katikati ya mji, ilipelekwa makaburini, Cathedral nzuri ilifanywa makumbusho, kati ya makanisa sabini, sitini na tano yalipewa kwa serikali kwa matumizi ya umma, hata na cheo cha Askofu Mkuu cha Kartago kilishushwa na kuwa Usimamizi wa Kitume.
Hata hivyo, waliimarisha urafiki na Rais wa Tunisia, Bourguiba, ambaye alianzisha uhusiano wa kibalozi na Vatikano. Wamisionari walibaki na chuo chao cha kufundisha Kiarabu kilicholeta mahusiano mazuri. Kati ya wakazi milioni 10, Wakristo ni asilimia 0.3 na Wakatoliki ni asilimia 0.2 tu. Mwaka 1996 Papa Yohane Paulo II (1978-2005), alitembelea Tunisia kuwatia moyo.
LIBYA
Libya ilipata uhuru wake mwaka 1951 kutoka kwa Waitaliani. Baada ya uhuru, idadi ya Wakatoliki ilishuka hadi kubakia 5,000 tu, na baadaye Wamisionari walifukuzwa, Wakopti nao walibakia wachache.
Baada ya mapinduzi ya Kanali Ghadafi, katika makubaliano na Vatikano, Kanisa lilibakiza kanisa moja tu kule Tripoli. Ila baadaye Gadafi aliwaalika Masista manesi kwenda kusaidia watu wake. Hata Masista Watanzania wa Shirika la Konsolata walikwenda huko. Kati ya wakazi milioni 5.4, Wakristo ni asilimia 2.1,   na Wakatoliki ni asilimia 0.3 tu.
Ingawa katika nchi nyingi za Maghreb kuna uhusiano wa kidiplomasia na Vatikano, hakuna uhuru wa kuabudu. Haiwezekani kujenga kanisa au kuhubiri dini kwa Waarabu Waislamu. Kwa Mwarabu kuongoka na kuwa Mkristo, ni kosa linaloadhibiwa kisheria, mahali pengine hata kuuawa.

DAR ES SALAAM

Na Pd. Dkt. Clement Kihiyo (TEC)

Mwaka wa Liturujia Leo ya Wokovu
1. Utangulizi:
Ishara na matendo yanayofanywa kwa wakati huwa njia ya wokovu kwetu. Mwaka wa Liturujia ambao pia huitwa mwaka wa Kanisa ni fumbo la Kristo. Ni kwa njia ya maadhimisho ya kumbukumbu takatifu ndani ya Mwaka wa Liturujia, ndipo tunapata wokovu. Katika Mwaka wa Liturujia, Fumbo zima la Kristo linafunuliwa; yaani, kutoka Umwilisho na kuzaliwa, na kutoka Kupaa hadi Pentekoste
Mama Kanisa Takatifu huchukulia wajibu wake kuadhimisha kwa kumbukumbu takatifu kazi ya ukombozi ya Bwanaarusi wake aliye Mungu, katika siku zilizopangwa katika mwenendo wa mwaka mzima. Kila juma, Kanisa katika siku aliyoiita “Dominika”, yaani “Siku ya Bwana”, linaadhimisha kumbukumbu ya ufufuko wa Bwana. Kwa namna ya pekee, linauadhimisha ufufuko huo pamoja na mateso yake yenye heri mara moja kwa mwaka katika Sikukuu ya Pasaka, iliyo kubwa kuliko maadhimisho yoyote (SC 102).
Katika mzunguko wa mwaka mzima, Mama Kanisa analikunjua fumbo la Kristo, tangu umwilisho na kuzaliwa, hadi kupaa mbinguni, mpaka siku ya Pentekoste na kungojea kwa tumaini lenye heri kurudi kwake Bwana. Anapokumbuka namna hii mafumbo ya ukombozi, Kanisa huwafungulia waamini utajiri wa uweza na mastahili ya Bwana wake. Kwa njia hii, uwepo wa mafumbo haya unakuwapo kwa nyakati zote, ili kutoka humo waamini waweze kuchota na kujazwa neema ya wokovu.
Mwaka wa Liturujia pia unawakilisha na kueneza tena  imani, maisha ya Kikristo na uwepo wa ukombozi wa Kristo na utajiri wa wokovu (SC. 102c). Mwaka wa Liturujia ni safari ya wokovu wa Kristo Mwenyewe na Kanisa lake (Lk, 24:15). Mwaka wa Liturujia sio mfuatano wa jumla wa siku na miezi, lakini unakuwa alama/ishara ya mfuatano ambao matukio ya neema yanatokea kama matukio ya wokovu kwetu hapa leo. Mwaka wa Liturujia ni wakati wa wokovu, ‘epifania’ ‘hic et nunc’ (hapa na sasa) kwetu.

2. Baadhi ya Mambo Makuu ya Mwaka wa Liturujia
2.1 Mwaka wa Liturujia ni Maadhimisho:
Matukio ya Mwaka wa Liturujia sio tu mifano ya kutafakari au kuiga uungu, lakini ni ishara zenye ufanisi za wokovu, ambao Kristo katika Utatu Mtakatifu, wamekamilisha kwa wokovu wa wanadamu. Mambo makuu ya ukombozi ni sisi kuadhimisha na kurithisha kwa kizazi kingine. Mwaka wa Liturujia una nguvu maalum ya kisakramenti na ufanisi wa kuimarisha maisha ya Kikristo.

2.2 Mwaka wa Liturujia Kuanzia Ufufuko:
Tukianzia na habari ya wanafunzi wa Emao (Lk 24:25-26); Yesu alieleza kisa chote kuanzia Ufufuko hadi Manabii. Ina maana kila kitu kinamhusu Kristo. “Bila ufufuko imani yetu haina maana” (1Kor. 15:13-17). Ufufuko ni chanzo na kitovu cha Mwaka wa Liturujia. Ufufuko ni siku ya Adamu Mpya (Rum. 11:5, Efe 2:5,8).
2.3 Siku ya Kwanza ya Juma-Dominika- Siku ya Bwana
Tangazo la ufufuko lilianza siku hii kwa amri ya Bwana (Mk.16.7, Mt. 28.7, Lk. 24.9). Ndipo wale wanawake wakatangaza ufufuko siku ile ile. Kwa hiyo, Dominika ni mwendelezo wa tangazo la Ufufuko. “Tunasherehekea Dominika kwa sababu ya Ufufuko Mtukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo, na tunafanya hivyo sio tu wakati wa Pasaka bali pia kila mzunguko wa juma, yaani kila Siku ya Kwanza ya Juma. Mtakatifu Augustino anaiita Dominika kwa usahihi kama Sakramenti ya Pasaka  (Taz . In Io. Tract . XX, 202: CCL 36,203), (SC 26, 184). Kwa Kanisa la Mashariki Dominika ni ‘Anastasimos hemera’, yaani, siku ya ufufuko.
Matendo ya kiliturujia si matendo ya kila mmoja peke yake, bali ni maadhimisho ya Kanisa, ambalo ni “sakramenti ya umoja”, yaani taifa takatifu linalokusanywa na kuratibishwa chini ya uongozi wa Maaskofu SC 26.
Kwa sababu hiyo matendo hayo ni ya mwili wote kabisa wa Kanisa, nayo huudhihirisha na kuuimarisha. Aidha, kila mmoja wa wanakanisa anahusika kwa namna tofauti, kadiri ya utofauti wa daraja, wa majukumu, na wa ushiriki kiutendaji
Matukio maalum ya kimungu siku ya Dominika pia yanaipa siku hii umaalumu wake. Maana yake:

i.    Roho Mtakatifu alitolewa kwa Wanafunzi siku ya Dominika (Pokeeni Roho Mtakatifu, wowote mtakaowaondolea dhambi wameondolewa),
ii.    Pentekoste ilikuwa siku ya Dominika,
iii.    Dominika ni siku ya Amani, siku ya Yubilei ya Roho Mtakatifu (Lk 4:18-19, Isa 61:1-3).
iv.    Kwa namna ya pekee, Dominika ni siku ya uumbaji mpya, siku ya Jua Jipya (Mal, 4:2).

2.4 Dominika ni Kitovu na Kiini cha Mwaka wa Liturujia:
Dominika ni Kitovu na Kiini cha Mwaka wa Liturujia kwa muktadha ufuatao:
Dominika ni siku ya Bwana. Wayunani wanaiita, “Kyriake Hemera”, ambapo kivumishi ‘Kyriake’ kinarejelea Kyrios, yaani Bwana aliyefufuka pamoja na Roho (1 Kor. 16:2, Mdo, 20:7, Ufu.1.10).
Dominika ni siku ya kimungu ya kumwadhimisha Bwana, siku kwa ajili ya kumega mkate na Neno, siku kwa ajili ya karamu na kwa ajili ya kukusanya sadaka kwa ajili ya maskini (2 Kor, 9:12, Rum. 15:27).
Dominika ni siku ya mwanzo wa uumbaji, ni siku ya nane baada ya ufufuko. Ni siku ya nane kwa sababu ni nje ya muda unaopimwa katika wiki. Siku ya nane ni siku ya Ekaristi. Hivyo, Dominika hugusa fumbo zima la wokovu. Inaleta pamoja na yenyewe ulimwengu wote wa mfano wa Kikristo. Inaangazia siku ya mwisho, siku ya Parousia.
Kwa hiyo, Dominika ni siku maalum na siku pekee  ya Bwana. Inaunda mwendelezo halisi wa adhimisho wa Kanisa kutoka Pentekoste hadi kurudi kwa Bwana. Maadhimisho mengine, isipokuwa kama yana umuhimu mkubwa, hayatapewa kipaumbele kuliko Dominika ambayo ndiyo msingi wa kweli na kiini cha Mwaka mzima wa Liturujia.
Kadri ya mapokeo ya Mitume, yanayopata asili yake katika siku ya ufufuko wa Kristo, Kanisa huadhimisha fumbo la Pasaka kila siku ya nane, katika siku ile iitwayo kwa haki kabisa Siku ya Bwana au Dominika. Katika siku hii Waamini wanapaswa kujumuika pamoja ili, wanaposikiliza Neno la Mungu na kushiriki Ekaristi, wafanye ukumbusho wa mateso, ufufuko na utukufu wa Bwana Yesu. Na pia watoe shukrani kwa Mungu “aliyewazaa upya katika tumaini lenye uhai kwa njia ya ufufuko wa Yesu Kristo katika wafu” (1Pet, 1:3). Kwa hiyo, siku ya Dominika ni Sikukuu ya kwanza ambayo ni lazima ielezwe vizuri na kuingizwa, kwa kadri inavyowezekana, katika maisha ya kidini ya Wakristo, ili iweze kuwa pia siku ya furaha na ya kuacha kazi. Maadhimisho mengine yasitiliwe mkazo sana, isipokuwa yale yenye umuhimu zaidi, kwa sababu siku ya Dominika ni msingi na kiini cha mwaka mzima wa Liturujia (SC. 106).

3. Fumbo na Mafumbo ya Kristo:
Imani ya Kikristo inaadhimisha Fumbo Kuu Moja la Pasaka, nalo ni  Fumbo la Kristo, aliyeteswa, akafa, akazikwa na kufufuka. Kanisa linaendelea kuadhimisha Fumbo hili kwa njia tofauti. Fumbo hili lilianza kufunuliwa katika Agano la Kale; na linatimizwa kihistoria katika maisha ya kidunia ya Kristo, na lipo katika mafumbo ya kisakramenti.
Fumbo la Pasaka huadhimishwa katika mwaka kwa njia tofauti, lakini katika utaratibu ule ule wa Neno, mwili na kikombe cha Yesu Kristo. Awamu tofauti za maadhimisho zinalenga kutufanya tuelewe vizuri Fumbo hilo. Katika uwezo wetu mdogo wa kibinadamu na kisaikolojia, hatuwezi kulielewa na kuliadhimisha hilo Fumbo kwa wakati mmoja na kuchota utajiri wa neema ya Fumbo hilo la Kristo”, kwa hivyo, Mwaka wa Liturujia unatupa muda wa kutosha wa kuliadhimisha na kuchota neema zake.
Kwa muktadha huu, katika kila Misa kuna Majilio, Noeli, Epifania, Alhamisi Kuu, Ijumaa Kuu, Pentekoste, Pasaka, Kupaa, na Watakatifu wote. Kwa hiyo, Mwaka mzima wa Kanisa ni Fumbo Moja, “ Sakramenti Paschale ” ambalo huadhimishwa kila Dominika.
Kutoka hili Fumbo Kubwa la Pasaka, linajigawa katika mafumbo kadhaa yanayorejelea matukio tofauti katika maisha ya Kristo, na ni ushiriki na ukuzaji wa Fumbo moja pekee la Pasaka, ambalo huanza kutoka Usiku Mtakatifu wa Ufufuo hadi wakati wa Pasaka hadi Pentekoste, Wiki Takatifu, Kwaresima, Wakati wa Kawaida, Majilio, Noeli hadi Epifania na Sikukuu mbalimbali.
Itaendelea toleo lijalo.

DODOMA

Na Bartholomew Wandi

Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 hauko mbali sana kuanzia sasa, kwani ukipiga hesabu umebaki takribani muda wa mwaka mmoja (1) na miezi kadhaa hivi. Wananchi wengi ambao watafikisha miaka kumi na minane wakati wa jukumu hili, waliofikisha miaka kumi na minane (18) tayari na zaidi, na wale ambao waliokuwa na sifa zote za kuandikishwa mwaka 2020, lakini kutokana na sababu zisizoweza kuzuilika walikosa nafasi ya kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, wataandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Awamu ya Kwanza na ya pili  ya uboreshaji.
Mpaka sasa mikoa yote 25 Tanzania Bara tayari ina watu ambao wanahitaji kuandikishwa kuwa wapiga kura wenye sifa nilizozielezea hapo juu.Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni hitaji la kisheria na Kikatiba pia. Tume ya Taifa ya Uchaguzi, imepewa jukumu la kisheria kuandikisha wapiga kura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuliboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania na pia Madiwani Tanzania Bara.
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utakuwa mahsusi kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura wapya, wanaohitaji kurekebisha taarifa zao zilizokosewa awali, waliopoteza kadi za kupigia kura, wenye kadi zilizoharibika ili waweze kupata kadi nyingine,  na wale ambao wanataka kuhama Jimbo au Kata kwenda Jimbo au Kata nyingine ili waweze kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Kifungu cha 12 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inaeleza, “Mkurugenzi wa Uchaguzi ataweka, atatunza na kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililoanzishwa chini ya kifungu cha (1)”.
Kulingana na Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, Kifungu cha 9 (2) inasema, “Bila kujali Masharti ya kifungu kidogo cha (1), na kwa kuzingatia uthibitisho wa umri , Mtanzania yeyote ambaye hajapoteza sifa chini ya Sheria hii au Sheria nyingine yoyote ya Bunge, na ambaye wakati au kabla ya tarehe ya Uchaguzi atatimiza umri wa miaka kumi na minane (18) atastahili kuandikishwa kuwa Mpiga Kura chini ya
Kifungu cha 13 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, pia inaeleza kwamba, “Tume itamwandikisha mtu yeyote Tanzania Zanzibar ambaye anastahili kuandikishwa kuwa mpiga kura katika Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano”.
Zaidi ya hayo, Ibara ya 5(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inafafanua, “Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka kumi na minane (18) anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi. Na haki hii itatumiwa kwa kufuata masharti ya ibara ndogo ya (2) pamoja na masharti mengine ya Katiba hii na ya Sheria inayotumika nchini Tanzania kuhusu mambo ya uchaguzi”.
Pamoja na hayo, pia Ibara ya 5(3)(a-d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inaeleza kuwa Bunge  litatunga sheria ya uchaguzi na kuweka masharti kuhusu kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuweka utaratibu wa kurekebisha yaliyomo katika Daftari hilo, kutaja sehemu na nyakati za kuandikisha wapiga kura na kupiga kura, utaratibu wa kumwezesha mpiga kura aliyejiandikishwa sehemu moja kupiga kura sehemu nyingine na kutaja masharti ya utekelezaji wa utaratibu huo, na kutaja kazi na shughuli za Tume ya Uchaguzi na utaratibu wa kila uchaguzi ambao utaendeshwa chini ya uongozi na usimamizi wa Tume ya Uchaguzi.
Marekebisho ambayo yanapaswa  kuingizwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni kuondoa wapiga kura waliojiandikisha zaidi ya mara moja, waliojiandikisha na huku wako chini ya umri wa miaka kumi na minane (18), waliofariki dunia  au kupoteza sifa ya kuwa wapiga kura kwa namna nyingine, kuwapa kadi za mpiga kura mpya waliopoteza kadi zao, kurekebisha taarifa za wapiga kura zilizokosewa awali,  na kuwaingiza waliofikisha umri wa miaka kumi na minane (18) na kuendelea.
Kifungu cha  16(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inasema, “Tume itakuwa na jukumu la kupanga muda na kupitia upya uandikishaji wa wapiga kura katika kila eneo la uchaguzi ndani ya jimbo”
Kwa mujibu wa kifungu cha 16 (5) cha  Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, inaeleza kwamba Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika mara mbili kwa miaka mitano (5), yaani baada ya Uchaguzi Mkuu kupita, na kabla ya siku ya uteuzi.
Uchaguzi Mkuu wa Mwisho ulifanyika Oktoba 28 mwaka, 2020, na sasa Tume ipo kwenye maandalizi ya kuboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Mchakato wa Uboreshaji huo wa Daftari umeanza kwa kukagua vituo vilivyotumika kuandikishia Wapiga Kura mwaka 2019/2020.
Uhakiki huo wa vituo hivyo vya kuandikishia wapiga kura, unalenga kuona kama kuna haja ya kuongeza vituo, kuona kama vilivyopo bado vinakidhi matakwa ya kisheria, na kufanya marekebisho mengine kama vile kubadilisha au kurekebisha majina ya vituo vilivyokosewa.
Matokeo ya uhakiki huo kwa Tanzania Bara yanaonesha kuwa, vituo vya kuandikisha wapiga kura vimeongezeka kutoka 37,814 hadi 40,126 ambapo kati ya vituo hivyo, 39,709 ni vya Tanzania Bara na vituo 417 ni vya Zanzibar.
Baada ya kazi ya kukagua vituo hivyo, Tume imefanya Uboreshaji wa majaribio (pilot) unaofanyika katika baadhi ya vituo vilivyoko kwenye halmashauri za Wilaya na Halmashauri za miji kwa  lengo la kujaribu kuona namna na jinsi vifaa vya uboreshaji vinavyofanya kazi katika mazingira tofauti, na kupata namna bora ya kufanikisha zoezi hili la uboreshaji.
Tume tayari imeshafanya uboreshaji wa majaribio katika kata ya Ikoma iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rorya Mkoani Mara na Kata ya Ng’ambo iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Mkoani Tabora. Kata hizi zilichaguliwa ili kupata mazingira tofauti ya kijiografia, pamoja na idadi ya watu.
Uboreshaji huu wa majaribio umefanyika kwa mafanikio kutokana na kuboreshwa kwa vipuri na mfumo wa uandikishaji wa wapiga kura. Aidha, ilibainika kuwa betri mpya za BVR Kits zinao uwezo wa kuhifadhi chaji kwa muda mrefu, na hivyo zitaweza kukabiliana na changamoto ya nishati ya umeme katika baadhi ya maeneo ambayo hayana miundo mbinu hiyo.
Pamoja na mafanikio hayo kulikuwa na changamoto ndogo ya baadhi ya  wapiga kura kutokuwa na uhakika ama kukumbuka majina yao wanapokuja kurekebisha taarifa zao na hivyo kuchukua muda mrefu kituoni kutokana na kazi ya kutafuta majina yao kwa usahihi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi  itaendelea kuwaelekeza Wapiga Kura kuhakikisha wanakumbuka taarifa zao kwa usahihi ili waweze kuhudumiwa kwa haraka vituoni.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele wakati akiongea na Waandishi wa Habari Mjini unguja, Zanzibar, amesema kuwa uzinduzi rasmi wa Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika Mkoa wa Kigoma tarehe 01 Julai, 2024.
Uboreshaji huo wa Daftari kwa Teknolojia ya BVR kwa mwaka huu 2024, hautakuwa tofauti na wa mwaka 2019/2020, ambao ulihusisha wananchi wote wapya wenye sifa za kuwa wapiga kura, waliohama jimbo au Kata, na ambao kadi zao zilipotea au kuharibika.
Wapiga kura ambao waliandikishwa mwaka 2015 na  2020 na wanazo kadi zao za kupigia kura na hazina matatizo yoyote, au hawajahama Jimbo/Kata kwenda Jimbo/Kata nyingine au hakuna mabadiliko yoyote ya mipaka ya kiutawala,  wanatakiwa pia kwenda katika vituo vya kuandikisha Wapiga Kura ili kuhakiki taarifa zao kwenye Daftari.
Kwa upande wa idadi ya Wapiga Kura watakaoandikishwa awamu hii, Tume imeshafanya makadirio kulingana na uandikishaji uliopita pamoja na matokeo ya Sensa ya watu na makazi uliofanyika mwezi wa Agosti mwaka huu, 2022.
Mhe. Jaji Mwambegele aliwaambia Waandishi wa Habari kuwa, makadirio ya Tume kwa kutumia ripoti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ya Sensa ya Watu na Makazi, inatarajiwa idadi ya Wapiga Kura kuongezeka kufikia 34,746,638 kutoka 29,754,699 ya Wapiga Kura katika mwaka 2020, idadi hii itajumuisha wapiga kura wapya 5,586,433, sawa na asilimia 18.7 wanaotarajiwa kuandikishwa.
Pamoja na hayo, Mwnyekiti wa Tume anasema kuwa inakadiriwa Wapiga Kura 594,494 wataondolewa katika Daftari kwa kupoteza sifa na jumla ya Wapiga Kura 4,369,531 wataboresha taarifa zao. Hawa watakaoboresha ni wale ambao taarifa zao zilikosewa au wamehama kutoka Kata au Jimbo moja kwenda eneo lingine la Uchaguzi, na wengine ni wale ambao kadi zao zimeharibika au zimepotea.
Hata hivyo, Uboreshaji wa safari hii hautofautiana sana na ule wa mwaka 2015 na 2020, kwani Teknolojia itakayotumika ni ile ile ya kuchukua alama za kibaiolojia yaani Biometric Voters Registration (BVR), pamoja na Android.
Aidha, mabadililiko yanayotazamiwa ni kwa upande wa kupunguza ukubwa na uzito wa BVR Kits ambapo awali wakati wa uboreshaji wa Dafrari wa mwaka 2014/2015 na 2019/2020 BVR zilikuwa na uzito wa kilo 35 lakini kwa uboreshwaji wa mwaka huu kwa 2024/2025, uzito umepunguzwa  hadi kufikia kilo 18 ambapo yapo masanduku mawili, moja ni kwa kuhifadhia mashine ya BVR Kits, na lingine ni kuhifadhia vifaa vingine vya kuunganishia BVR Kit hiyo ikiwemo kishikwambi kwa ajili ya kupigia picha ya Mpiga Kura na kuchukulia alama za vidole, ila vifaa hivi vitatoa huduma ile ile ya kuandikisha wapiga kura na kutoa kadi hapo hapo kituoni.
Mabadiliko mengine katika Uboreshaji wa Daftari ni Tume kuanzisha mchakato wa uboreshaji kwa njia ya mtandao (Online) ambapo mpiga kura anaweza kuanzisha mchakato huu wa awali kwa njia ya mtandao ili kurekebisha, au kubadilisha taarifa zake, kuhamisha taarifa zake kutoka kituo cha awali kwenda kingine, au anayetaka kufanya vyote kwa pamoja.
ITAENDELEA WIKI IJAYO.
Wapiga kura wanaotaka kuboresha taarifa binafsi na wanaohama vituo au vyote viwili kwa wakati mmoja, wanaweza kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zao kwa njia ya mfumo wa mtandao ‘online’ kuingia kwenye Tovuti ya Tume www.inec.go.tz kwa kutumia kompyuta au simu janja, kisha atabonyeza kiunganishi (link) iliyoandikwa Boresha Taarifa za Mpiga Kura, au atatumia anuani ya ovrs.nec.go.tz itakayompeleka moja kwa moja kuanzisha mchakato huo.
Katika mfumo huu, wapiga kura wanatakiwa kuingiza namba ya kitambulisho cha taifa (National Identity Number: NIN), namba ya kadi ya mpiga kura, namba ya simu anayotumia kwa sasa, na jina la Kata, kisha watapata ujumbe wenye namba za utambulisho (token namber) ambazo wataenda nazo kituoni ili kukamilisha taratibu za kupata kadi za mpiga kura.
Mwombaji ambaye ni mpya anatakiwa kwenda kituoni bila kuwa na kitambulisho cha aina yoyote kiinachomtambulisha ili aweze kupatiwa kadi ya mpiga kura. Mwaombaji huyu atakapofika kituoni atamwona Mwandishi Msidizi wa Kituo cha kuandikisha Wapiga Kura na  kuajaza fomu Na. 1,
Baada ya kujaza Fomu Na. 1, Mwombaji huyo Mpya atampatia Afisha Mwendesha Mashine ya Bayometriki (BVR Kits Operetor) ambaye ataingiza taarifa zake kwenye BVR Kit, atapigwa picha, atachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili  na kuweka saini na kupewa Kadi ya Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Kwa wapiga kura ambao walipoteza, kuharibika au kukosewa Kadi zao na ambao hawatajaza Online, watakapofika Kituoni, watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo , kisha Afisa Mwendesha Mashine ya Bayometriki ataingiza taarifa zao kwenye BVR Kit, akisha watapigwa picha, watachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili, na kuweka saini na mwishowe watapewa Kadi zao za Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Vile vile,, Wapiga Kura ambao wanataka kuhamisha taarifa zao, pia watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo ili kuomba kuhamishiwa taarifa zao kwenda Jimbo au Kata na Kituo kingine cha Kupigia Kura wakati wa Uchaguzi Mkuu, na Chaguzi nyingine Ndogo zitakazofuata baada ya Uchaguzi Mkuu kupita.
Aidha, Mtu anatakiwa aende mwenyewe kituoni na anatakiwa kujiandikisha mara moja tu. Ni kosa la jinai kwa mwananchi yeyote kwa makusudi kwenda kituoni na kujiandikisha zaidi ya mara moja. Mwaka 2015, Kwa Mkoa mmoja tu wa Njombe, Kanzi Data hiyo imeweza kung’amua wapiga kura zaidi ya 600 waliojiandikisha zaidi ya mara moja, na walichukuliwa hatua za kisheria.
Kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024,  kifungu cha 114(1)(b) inaeleza kuwa “kwa kujua au ana sababu ya kuamini kuwa ameandikishwa katika eneo la Uchaguzi anaomba kuandikishwa kinyume na kifungu cha 25, na bila kufichua kwa Msimamizi wa Uchaguzi kujiandikisha kwake kwa awali katika eneo jingine la Uchaguzi atenda kosa na akitiwa hatiani atapaswa kulipa faini isiyopungua shilingi laki moja na isiyozidi shilingi laki tatu au kifungo cha muda usiozidi Miaka miwili au vyote kwa pamoja”.
Baada ya zoezi hili, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itaandaa Daftari la Awali la Wapiga Kura na kupelekwa mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) kwa ajili ya wapiga kura kuangalia kama majina yao yamo kwenye Daftari.
Kama baadhi ya majina hayaonekani, Wapiga Kura watamweleza Mwandishi Msaidizi kutoonekana kwa majina hayo na Mwandishi Msaidizi ataandika majina ya Wapiga kura hao waliokosekana kwenye Daftari la Awali na kisha ataleta orodha hiyo ya Majina Tume kwa ajili ya kuingizwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Pamoja na hayo, dhumuni lingine la Tume kupeleka Daftari la Awali la Wapiga Kura mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) ni kuwapa fursa Wapiga Kura kuangalia kama kuna majina ya Wapiga Kura walioandikishwa na hawana sifa kisha watawawekea pingamizi kwa kujaza fomu Na. 3B na kumkabidhi Mwandishi Msaidizi fomu hiyo ambaye ataileta Tume kwa ajili ya Wapiga Kura hao ili wafutwe kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kama kweli hawana sifa.
Hata hivyo, Majina hayo yaliyowekewa pingamizi hayafutwi moja kwa moja kwenye Kanzi Data ya Tume badala yake yanahifadhiwa sehemu nyingine kwenye Kanzi Data ili kama mtu huyo ana ushahidi wa kutosha kuwa ana sifa za kutosha kuandikishwa na kubaki kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura anarudishwa mara moja, Machapisho mbalimbali ya Elimu ya Mpiga Kura ya uhamasishaji ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yatasambazwa nchi nzima  ili kuwaelimisha Wapiga Kura kuwa na uelewa na mwamko wa kujiandikisha kwa wingi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga kura.
Mchapisho hayo pia yanasistiza Wapiga Kura kutunza Kadi zao za kupigia kura na hatimaye kujitokeza kwa wingi kupiga Kura kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2025 utakapowadia na Chaguzi Ndogo zitakazofuata  na kila mmoja anatakiwa awe na Kadi yake ya kupigia kura.
Tume pia katika uhamasishaji wake wa Uboreshaji wa Daftari itatumia vyombo mbalimbali vya habari kama Magazeti, Radio kubwa na Radio za Kijamii, TV, INEC TV ONLINE, Tovuti ya Tume na Mitandao ya Kijamii, machapisho yakiwemo mabango, vijitabu na vipepeperushi, gari la Elimu ya Mpiga Kura na kushirikisha wadau kwa kutoa vibali kwa taasisi na asasi za kiraia.
Mwandishi wa Makala haya ni Afisa Habari Mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) Simu  0754203015.

Dar es Salaam

Na Edvesta Tarimo

Kwa mujibu wa Benki ya Dunia (World Bank -2023), inakadiriwa kuwa uzalishaji wa taka utaongezeka kwa 70% kutoka tani bilioni 2.01 hadi bilioni 3.40 ifikapo mwaka 2050.
Kulingana na ripoti ya taarifa ya kiuchumi ya Urejelezaji wa Marekani
(U.S Recycling Economic Information - REI), San Francisco, Marekani, ni jiji la kijani kibichi hasa, na linatajwa kama kinara kwa urejeshaji wa taka (recycling), kwa zaidi ya asilimia 80 ya taka zake.
Urejelezaji wa taka na mifumo mizuri ya kushughulika na majitaka, utasaidia kuongeza ajira, kuongeza viwanda vidogo vidogo, kuongeza teknolojia mpya, pamoja na kipato ambacho kimekuwa kikipotea, ikiwa ni pamoja na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.
Majiji mengine yanayofanya vizuri kwenye urejeshaji wa takataka ni pamoja na Curitiba - Brazil, iliyofanikiwa kwa asilimia 70, pamoja na Vancouver-Canada, waliofanikiwa kwa asilimia 60 wakiwa na lengo la kufikia asilimia 100 ifikapo mwaka 2040.
Wanafanyaje? Kwa kushikamana na mipango madhubuti ya kuchakata taka na sera ya kulipa fedha kadri wakazi wake wanavyotupa taka zisizoweza kutumika tena, huwafanya wananchi wawe na ufahamu zaidi wa mazingira, hasa kuhusu bidhaa wanazonunua katika kuepuka kulipishwa fedha zaidi za taka.
Nini kifanyike kukabiliana na hili?
Jiji la Dar es salaam ambalo linatajwa kuwa kitovu cha biashara, lenyewe linakadiriwa kuzalisha zaidi ya tani 4,252 za taka kwa siku moja. Kati ya taka hizo, ni asilimia 50 tu ndizo zinazopokelewa kwenye maeneo maalumu, nyingine zikisalia na kutupwa kwenye mitaro, maeneo ya wazi, na hata barabarani.
Hapa Tanzania, baadhi ya wadau wa mazingira wamekuja na mpango mkakati wa kuweka mazingira katika hali safi kwa kukusanya takataka, na kwa kupita baadhi ya masoko katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kama vile Ilala, Buguruni. n.k.
Alpha Ntibachunya  ameamua kushiriki katika utunzaji wa mazingira kwa kuanzisha kampuni ya LIMA ya kurejeleza taka ngumu katika matumizi mengine, badala ya kutupwa na kuchafua mazingira.
Ntibachunya anasema kuwa yeye na mwenzake walifanya utafiti wa kujua takataka zinazotupwa zinapelekwa wapi baada ya kukusanywa, na baada ya utafiti, waligundua kuwa kuna fursa nyingi zinazopatikana kwenye takataka.
“Kilichotupelekea tukaanzisha huu mradi, tulikaa tukafanya utafiti na kugundua kwamba kuna changamoto, baada ya hapo tukapata wazo linguine, tukaja na wazo hili la kuzalisha chakula cha kulishia mifugo, na mbolea ambayo tulitazama zaidi wakulima wadogo, hasa wa vijijini,” anasema Ntibachunya.
Anaongeza kusema kuwa njia mbili tofauti wanazotumia katika kukusanya taka, kwa kwenda sokoni, mfano soko la matunda Buguruni, hotelini na kutumia njia ya boksi hai ambalo hupeleka majumbani mwa watu kwa ajili ya kukusanyia mabaki ya vyakula majumbani mwa watu, kisha wanakwenda kuzichukua na kwenda kuzichakata.
Anasema kuwa wametumia changamoto ya mlundikano wa takataka katika maeneo tofauti tofauti katika jiji kugeuza kuwa sehemu ya kujipatia ajira, na kuajiri vijana wengine katika kukusanya na kuzichakata na kuwa chakula cha kulishia mifugo, na mbolea ambayo ni halisia isiyokuwa na makemiko ya aina yoyote.
Ntibachunya anasema kwamba uchakataji wa taka katika matumizi mengine umekuwa mchango mkubwa wa nafasi ya ajira kwa vijana wengi, kwani uzalishaji wake hauhitaji kiwango cha elimu, bali utayari wa kijana wa kuelekezwa kufanya kazi hiyo.
Kuchakata taka kunanufaisha mazingira, na kunatoa ajira kwa vijana, kunakuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla. Kwa kutenganisha taka zinazoweza kutumika tena kama karatasi, nguo chakavu, glasi, plastiki, aluminium na mabaki ya vyakula na taka za elektroniki, watumiaji wanaweza kusaidia kuunda kijani kibichi kwenye majiji makubwa duniani.
Anitha Erasmi ni mama wa watoto wanne, anasema kuwa uchakataji wa taka umekuwa sehemu yake ya kujipatia kipato cha kuendesha maisha ya familia yake, licha ya ndugu kumwona kama amechanganyikiwa.
“Mwandishi, ndugu zangu na jamii, iliniona kama chizi, lakini mimi sikujali kwa sababu mjini kama huna kazi, ukichagua kazi utashindwa kuishi. Nakusanya mamboga mboga nazipeleka kuziuza, napewa pesa,” anasema Anitha.
Philbert Alphonce mkazi wa Goba jijini Dar es Salaam, anasema kwamba amekuwa anakikusanya taka ngumu kutoka soko na kuzipeleka sehemu wanakozichakata na kuzirejelesha katika matumizi ya kulisha baadhi ya mifugo, na pia mbolea asilia ambayo hutumiwa na wakulima wadogo wadogo kuweka kwenye mashamba ya mboga na maua.
Alphonce anasema amekuwa akiendesha familia yake ya mke na watoto wawili kupitia kazi yake ya ukusanyaji wa mabaki ya mbogamboga na kwenda kuziuza, ambapo kwa wiki anakwenda sokoni mara mbili, huku siku nyingine akizitumia kwa shughuli zake nyingine.
NEMC,Wadau watoa neno
Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (National Environment Management Council – NEMC), Dk. immaculate Sware Semesi anasema NEMC, na taasisi ya mazingira, kituo cha Sayansi cha Mazingira (Centre for Science and Environment - CSE), kutoka India, wamekutana nchini Tanzania kujenga uelewa wa nini kifanyike katika taka ngumu, kuchukua takwimu ni taka kiasi gani zinazalishwa na zinatunzwaje, ili ziwe fursa badala ya kuwa uchafuzi wa mazingira.
Dk.Semesi anasema sambamba na hilo, kutambua ni teknolojia gani itumike ili kufanya taka zisiwe kero katika manispaa na jiji, bali ziwe fursa ya kuzalisha ajira au nishati kutokana na taka.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila katika moja ya hotuba yake alisema kwamba anaiona fursa kubwa kwenye wingi wa taka hizo, na tayari alisafiri mara moja kwenda kwenye jiji la Bursan nchini Korea Kusini kujifunza namna wenzetu walivyofanikiwa kwenye urejelezaji wa taka, na kuzifungamanisha na fursa kwa vijana wa rika mbalimbali.
Chalamila anasema kwamba jiji la Dar es salaam linaweza kuwa mfano kwa majiji mengine nchini Tanzania na Afrika Mashariki kwa fursa ya ajira kwa njia ya urejeleshaji wa taka, endapo juhudi za makusudi zitachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa vitendo.
Anaongeza kuwa urejelezaji wa taka (recycling) ni mchakato wa kutibu taka kwa lengo la kuokoa malighafi zilizopo ndani ya taka na kuzirejesha kwenye matumizi ya kiuchumi.
Vifaa vya kielektroniki kama simu na kompyuta hurejelezwa na kutumika tena katika kutengeneza matofali, saruji na vyombo vipya vya glasi.
Taka za kaboni kama maganda ya matunda na mbogamboga, zinatumika kutengeneza mbolea na karatasi zikirejelezwa na kutumika kama makasha ya mayai na vifungashio vya bidhaa mbalimbali.
Ripoti ya Benki ya Dunia kuhusu maendeleo ya miji, inaonesha kuwa Afrika huzalisha tani milioni 70 za taka kwa mwaka.
Wakati huu ambapo ongezeko la watu wanaohamia mijini linaongezeka kwa kiasi kikubwa, Benki ya Dunia inasema kuwa kufikia mwaka 2025, uzalishaji wa taka huenda ukafikia tani milioni 160 kwa mwaka.
Tafiti zinasema kwamba ni rahisi kutengeneza bidhaa kutoka nyenzo zilizorejelezwa, kwani bidhaa kama ya aluminium iliyorejelezwa inaweza kuandaliwa tena na kuuzwa kwa bei nusu, kutokana na kuhitajika nishati kidogo ya kuchakata aluminium iliyorejelezwa, kuliko kutumia aluminium mbichi ya kiwandani inayotumika kwa mara ya kwanza.
Urejelezaji pia huepusha gharama ya utupaji wa taka kwenye dampo na vichomaji (incinerators), kwani baada ya kuanza kwa urejelezaji, dampo chache zitahitajika, na ardhi zaidi zilizokuwa zimetengwa kuhifadhi taka huweza kutumika kiuchumi.
Aidha, mapato ni sehemu nyingine aliyoiona Chalamila, kwani urejelezaji huimarisha tasnia ya uchakataji, na hivyo kutengeneza nafasi mpya za kazi kwenye viwanda vidogo vitakavyoundwa, kama viwanda vya chuma, karatasi, glasi, pamoja na ajira kwenye vituo vya ukusanyaji taka, na hata warejeshaji husika.
Utafiti wa U. S Recycling unaonesha kuwa nguvukazi ya kuchakata na kutumia tena malighafi zinazotokana na taka, imekuwa kubwa zaidi kwenye mataifa mengi, zaidi ya nguvukazi inayotumika kwenye uchimbaji wa madini na usimamizi wa taka zisizorejelezwa.Mashirika yanayorejeleza taka, huzalisha takribani dola bilioni 240 kwenye mapato ya kila mwaka.
Huko Carolina kusini pekee, zaidi ya wafanyakazi 15,000 na dola za Marekani milioni 69 za ushuru, hutokana na uchakataji wa taka, huku Carlifonia urejelezaji wa taka ukiajiri watu 85,000.
Kila mwaka, dunia inageuka kuwa makao ya takribani tani bilioni 2.01 za taka ngumu, na idadi hiyo inatarajiwa kufikia bilioni 3.40 miaka 30 ijayo, sawa na ongezeko la 70%.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, (World Bank – WB), mataifa yenye kipato cha juu inaonesha kwa siku kuna ongezeko la 19%, huku mataifa yenye uchumi wa kati na chini, ukiongezeka kwa 40% au zaidi.

Katika safu hii wiki kadhaa ziliyopita, tulisoma Historia ya Kanisa la Misri na Uinjilishaji wa Misri na Kanisa la Kaskazini mwa Afrika pamoja na kuangazia Uislam ulivyoingia Afrika. Leo tusome jinsi Uislam ulivyoiteka Afrika Kaskazini. Sasa Endelea…

Baada ya dola ya Kirumi Magharibi kuanguka, Wavandali waliokuwa wameiteka Afrika ya Kaskazini, walishindwa na Kaizari wa Mashariki katika dola ya Kostantinopoli. Kaizari alimweka gavana kutawala kwa niaba yake.
Mwaka 647 Gavana Gregori wa Kartago aliwaasi wakubwa zake wa Konstantinopoli. Waislamu walipokuja toka Misri chini ya Ukba Ibn Nafi, alidhania wanakuja kumsaidia dhidi ya Konstantinopoli, hivyo akawaunga mkono wakaingia kwa urahisi.
Baadaye walimgeuka na kuteka Afrika ya Kaskazini. Wakristo Wazungu yaani wenye asili ya Ulaya walikimbilia Ulaya na wakabaki Waberba wenye asili ya Afrika, kutetea Ukristo na nchi yao.
Mwaka 711, Mussa alimtuma Tarik (riq ibn Ziyd) jemadari wa Kiberba aliyeongokea Uislamu na jeshi lao la watu 7,000 kushambulia Uhispania. Walipoanza kupata mafanikio naye alikwenda na jeshi lake, wakateka pamoja Uhispania.
Katika kugawanya nyara hizo, Waarabu na Waberba wakawa marafiki. Guba la Gilbraltar ni ukumbusho wake ‘Gebel al Tarik’. Waberba wengi waliongoka na kuwa Waislamu kwa sababu bila kuwa Mwislamu, wasingepata sehemu ya hizo nyara na marupuuupu mbalimbali.
Mwishoni mwa karne ya 8, Afrika ya Kaskazini yote ilishakuwa ya Kiislamu. Wakati wa Mtakatifu Augustino, Afrika ya Kaskazini palikuwepo na maaskofu 700, lakini walipovamia Waislamu walibakia 35, na katika karne ya 12 walikosa maaskofu watatu wa kumweka wakfu mwenzao; na karne ya 14 hapakuwepo hata askofu mmoja.
Tofauti na Misri, ambapo ingawa lilidhoofishwa, bado Wakristo wapo licha ya unyanyasaji. Kanisa huko Afrika ya Kaskazini, maarufu kwa watakatifu na wanateologia kama Sipriani, Tertuliani na Augustino, lilitoweka kabisa.
Kosa kubwa la kwanza la Kanisa hilo ni kwamba lilijipenda na kujiendeleza kwa ndani, lakini likasahau kuinjilisha. Dini ilibaki tu katika mwambao wa dola ya Kirumi, tofauti na Misri waliotoka nje na kwenda Nubia hadi Uhabeshi.
Vilevile, dini ilibakia katika utamaduni wa kikoloni wa Kilatini hata wakawa Walatini kuzidi Roma. Hata mtakatifu Augustino ambaye mama yake alikuwa Mberba, hakuandika chochote katika lugha yao au kuingiza utamaduni wake katika Ukristo.
Wazawa walijua Ukristo kama waliingia utamaduni wa wakoloni wao. Hivyo wakoloni walipoondoka na lugha ya Kilatini, Dini ikatoweka pamoja nao. Misri waliendeleza lugha yao na kutengeneza ibada ya Kikopti, tofauti na Kigiriki.
Kanisa lisiloinjilisha na kutamadunisha, hufa. Hivyo, ile tabaka ya juu ya Walatini ambao ndio walikuwa Wakristo walipovamiwa na Waislamu, wao walikimbilia Ulaya pamoja na Maaskofu na Mapadre. Hili ni somo kubwa kwetu, Kanisa ili lidumu lazima liingie katika utamaduni na masiha ya kila siku ya watu, la sivyo litabaki kama vazi la Jumapili.
Waislamu katika Nubia (Sudan ya Sasa):
Baada ya kuiteka Misri, mwaka 641, Abdallah Ibn Saad aliishambulia Nubia. Ili kuhimili mashambulio hayo, falme mbili za Kaskazini Nobatia na Makuria ziliungana na kuwa ufalme wa makuria.
Kwa pamoja, zilishinda dhidi ya mashambulizi. Baadaye ufalme wa Makuria ulifanya umoja na ule wa Kusini wa Alodia na kupata nguvu kiasi kwamba mwaka 737 walituma kikosi hadi Aleksandria, Misri kumtoa mahabusu Patriarka aliyekuwa ametekwa na Waislamu.
Miaka kati ya 700 hadi 1250, kilikuwa kipindi cha maendeleo mazuri kwa Nubia. Walijenga makanisa mazuri, na hata mengine yamevumbuliwa na wachimbaji wa mambo ya kale. Alodia peke yake ilikuwa na makanisa zaidi ya 400 na monasteri nyingi. Pamevumbulika na maandishi mengi waliyoyaacha yakielezea ibada zao, na hasa sala.
Mwaka 1172 Misri ilitawaliwa na Waturuki wa Mamluki ambao walikuwa na nguvu na vilevile wakatili sana. Hawa walizonga Nubia, na ili kujihami, Misri iliweka Waislamu Kaskazini mwa Makuria kama ugo dhidi ya mashambulizi.
Bahati mbaya Nubia ilikuwa imekatwa kutoka ulimwengu mwingine wa Wakristo, na baadaye pakawepo mfarakano katika urithi wa wafalme. Hata hivyo waliweza kuwahimili Waislamu hadi mwaka 1504 ufalme ulipotekwa na Waislamu kutoka Misri.
Kwa miaka 1,000 walikuwa na Ukristo imara. Wamisionari waliporudi mwaka 1845 hawakukuta alama zo zote za Ukristo. Ilibidi waanze upya kati ya Waafrika weusi wa Sudan ya Kusini.
Uhabeshi (Ethipia ya sasa) na Uislamu
Uhabeshi ilikuwa na bahati ya kunusurika kutekwa na Waislamu. Sababu za kunusurika kwake kwanza ni kwamba Muhammad alipofukuzwa kutoka Mekka, Waislamu wengine walikimbilia Axum, Mji Mkuu wa Uhabeshi na kupokelewa vizuri.
Kwa sababu hiyo, Muhammad aliagiza katika Korani kwamba Uhabeshi  isishambuliwe, labda kama ni kujikinga.  Mwanzoni agizo hilo liliheshimiwa sana. Pili, nchi ya Uhabeshi iko milimani na si rahisi kuifikia na kuishambulia.
Wote waliozunguka Uhabeshi walitekwa na Waislamu, na yenyewe ikabaki kama kisiwa. Hata hivyo, Waislamu wengine waliingia mipakani na kuishi pembezoni na Waislamu wafanya biashara walioingia ndani walipeleka pamoja nao mawazo ya dini yao.
Mara nyingine ilikuwa vigumu kumpata askofu (Abuna) kutoka Misri, na hivyo kukaa miaka bila askofu au uongozi imara. Ili kujikinga na Waislamu, Wakristo walikimbilia zaidi ndani na milimani.
Kwa kwenda ndani ilisaidia kuinjilisha wazawa wa ndani ya nchi, na kuingiza zaidi utamaduni wao katika maisha ya dini. Ndani ya nchi yalikuwemo makabila ya Wahabeshi (Abyssinia), na mchanganyiko ukazaa utamaduni mpya wa Kihabeshi wenye lugha ya Amharic, ambayo sasa ndiyo lugha rasmi ya taifa, lakini lugha ya ibada iliendelea kuwa ‘Gaez’, lugha ya zamani ya Axum.
Mwaka 1270 Mfalme Yekuno Amlak (1270 - 85) na baadaye Mfalme Amda Seyon (1312 - 1342), walifufua kwa nguvu ukoo wa ufalme wa Suleman ambao ulikuwa umepoteza madaraka kwa Wazagwe tangu mwaka 1137.
Mfalme Zara Yokob (1411-1468), alifikisha katika kilele ustawi wa ufalme wa Uhabeshi. Akitaka kuimarisha nguvu zake dhidi ya Waislamu Wasomalia waliosaidiwa na Waturuki, alituma ujumbe Roma kwa Papa kuomba msaada.
Kama Konstantino kwa Warumi, naye alilazimisha ustaarabu wa Kikristo kwa Wahabeshi wote hata kwa wapagani, yakiwemo maadili ya Kikristo kama ndoa ya mke mmoja. Mkuu wa Kanisa la Uhabeshi alikuwa ni ‘Abuna’ aliyetumwa kutoka Misri kama kiungo cha umoja na Kanisa mama.
Chini yake alikuwepo ‘Echege’ aliyemsaidia Abuna katika mambo ya utamaduni na desturi mahalia. Hata hivyo, kiongozi halisi wa Kanisa hilo alikuwa ni ‘Negus Negasti,’ ikimaanisha ‘Mfalme wa Wafalme’. Hii iliendelea  mpaka wakati wa Negus Haile Sellasie katika karne ya 20.
Malkia Helena akishikilia kama mlezi kwa ajili ya mtoto wake mdogo Negus Lebna Dengel, upinzani wa dola za Kiislamu za Kisomali uliongezeka kwa vita vikali, naye aliomba msaada kwa Wareno.  Mjumbe Mreno alipofika kukagua alikuta mfalme Lebna Dengel (1508-40) amekimbilia milimani, na nchi yake imeharibiwa na Wasomali wa Haral chini ya Ahmedi Ihn Ibrahim, wakisaidiwa na bunduki za Waturuki.
Mwaka 1543 Wareno walituma askari 400 wenye bunduki wakawashinda Wasomali, Ahmedi akauawa vitani. Hii ilinusuru ufalme wa Ethiopia na kufungua uhusiano na nchi za nje. Hapo kinaishia kipindi cha kwanza ambapo Ethiopia ilikuwa imefungwa bila uhusiano na nchi za nje za Kikristu.

MWANZA

Na Paul Mabuga

Biashara ya huduma ya usafiri wa pikipiki maarufu hapa Afrika Mashariki na hata katika miji na vijiji vyetu kama bodaboda, ni ajira ya uhai na kifo!
Ni kazi ya raha kwa kuwa inaiingiza  kipato, lakini pia ni ya karaha kutokana na wakati mwingine jamii inavyowatazama wanaoiendesha.
Pia, kazi hii imejaa mzuka wa kilele cha tijira kwa vijana wa fasheni, wanaopenda muziki ‘mnene’ na bomba la moshi linalobalaruka kwa sauti kubwa.
Kwao, hawa hii ni ruya ya kupaa hadi anga la saba na kujisikia katika ndoto ya kilele cha furaha, na hili ni zilizala katika ajira hii, ikisimuliwa kwa Tumaini Letu na waendesha bodaboda watatu kutoka katika Jiji la Mwanza.
Wa kwanza ni Emmanuel Kalima mwenye umri wa miaka 32 hivi sasa na mkazi wa Ilemela katika jiiji la Mwanza. Leo  analazimika kuendesha bajaji katika  kituo cha Sabasaba jijini humo baada ya kupata ulenavu uliotokana na kukatwa mguu wa kulia  kufuatia ajali aliyoipata miaka tisa iliyopita  wakati akiwa na kazi ya kuendesha bodaboda.
Kalima yupo katika kituo chake cha kazi akisubiri abiria, akiwa na Rozari yake shingoni, bila shaka ana matumaini kibao kwamba  maombi yake yatasikika, pengine leo kama jana atapata fedha ya kutosha kununua chakula kwa  familia yake ya  watoto wawili na mke, pia kumudu mahitaji ya shule kwa wanae wawili  wakubwa wanaosoma darasa la kwanza na la pili mtawalia. Lakini pia ana jukumu la kupeleka hesabu kwa mmiliki wa chombo hicho cha usafiri.
“Nipo naishi na mke wangu na watoto, na maisha ni ya furaha, hakuna unyanyapaa ndani ya familia yangu, na kuna mapenzi makubwa. Tunafurahia maisha kwa wakati huu,” anasema Kalima ambaye mara baada ya kumaliza elimu yake ya Kidato cha Nne  mwaka 2007, aliingia katika mapambano ya kutafuta naisha.
Wa pili ni Nhumba Mihaye ambaye pia aliacha kazi ya udereva wa bodada aliyokuwa akiifanya katika jiji la Mwanza na  kuamua kuedesha bajaji katika kituo cha Buswelu jijini humo.
Kwa sasa ana umri kama wa miaka 55 hivi na alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuanza biashara hiyo ya huduma katika jiji hilo. Kama ilivyo kwa Kalima, Mihaye naye anatakiwa kukamilisha hesabu ya ‘bosi’ na nyingine ya kujikimu kwa familia yake.
“Boda hapa ziliingia mwaka 2008, na mie wakati huo niliingia kufanya kazi hiyo. Ili kumudu maisha na mipango yangu, nilikuwa nakesha na  kipindi hicho kupata hesabu ya shilingi 70,000/- hadi 80,000/- kwa siku, ilikuwa ni kawaida.
 Ingawa abiria walikuwa wachache, lakini na sisi watoa huduma tulikuwa wachache, na  kazi ilikuwa nzuri kwa kweli kulinganisha na sasa  hivi ambapo ushindani ni mkubwa, na watu wamepigika, hawana fedha hadi wengine wanatembea kwa miguu” anasema Mihaye.
Anashukur u kwa kazi hiyo kwa kuwa ameweza kujenga nyumba, na ana watoto ambao angalau wamesoma hadi chuo kikuu. Lakini changamoto alizokutana nazo wakati huo ndizo zilizomfanya aachane na udereva wa  bodaboda, hasa baada ya kuona kuwa anaweza kupoteza maisha.
Wa tatu ni Bahati Yohane, mkazi wa Kiseke Jijini humo, na  yeye anashukuru kwa kazi ya bodaboda kwa kuwa  ilimfanya akapata mke ambaye anaye hadi sasa. Anasema wakati huo anaendesha boda boda, mambo yalikuwa mazuri na hata alimudu kila mahitaji katika familia yake.
“Kutokana na kuwa na fedha nyingi, nilijikuta naongoza matumizi ambapo kila baada ya kazi kabla ya kurudi nyumbani, nilikuwa napita baa na kupata  [nakunywa bia] kidogo.  Ilifikia mahali, mke wangu alikuwa anagomba sana kuendesha piki piki nikiwa nimelewa, lakini sikukoma, hadi nilipokomeshwa, na ndiyo maana unaniona hivi, nachechemea,” anasema Yohane ambaye ana umri wa miaka 46, ambaye kwa sasa amehamia kwenye bajaji.
Yohane anasema kuwa nyakati hizo wandesha bodaboda walikuwa wakituhumiwa  kuwapa ujauzito mabinti wanafunzi, na anadai kwamba kwa siku hizi hilo limepungua  kwa kuwa wasichana wengi wamejitambua na hawadanganyiki na vitu vidogo vidogo kama ilivyokuwa zamani. Na pia wazazi wametambua majukumu yao ya kuwatimizia mahitaji mabinti zao.
Anasema pia ni kweli wapo waendesha boda boda  ambao hata wanafikia hatua ya  kufukuzwa kwenye vituo kutokana na tuhuma za unyanyasaji wa kingono kwa abiria wao, wakiwemo watoto na wanawake. Anaongeza kuwa licha ya tabia hizi mbaya  kupungua, lakini zimekuwa zikijenga taswira mbaya ya kazi hiyo machoni pa jamii.
“Ila kisa cha kuacha kazi ya bodaboda, ilikuwa ni siku moja pale Kiseke, nilikuwa nimekunywa pombe na naendesha, nikajikuta naingia  barabara kubwa bila tahadhari. Ilitoka huko, bodaboda kwenye barabara kuu ikiwa kasi na kunichota kama  mwewe anavyonyakua ikifaranga. Kutoka hapo sikujitambua hadi nilipojikuta  hospitalini natibiwa na hicho ndicho kisa cha huu ulemavu nilionao,” anasimulia Yohane.
Kwa upande wake Mihaye anasema kuwa kuna mtindo wa vijana, kupanua mabomba ya moshi ya pikipiki zao ili zitoe mlio mkubwa wakiendesha, wengine wanaweka muziki sauti ya juu kujifirahisha na hata kuzing’oa sight mirror  [vioo vye pembeni; na kuweka urembo mwingine kama fasheni.
“Ila wengi wanaong’oa vioo vya pembeni, huwa ni wahalifu, nia yao huwa ni kwamba wakimkwapua abiria wa pikipiki ya mbele yao au mtembea kwa miguu, wakimbie bila kikwazo cha kuona kuna mtu anawafuata, wanaamini kwamba, wakiwa wanaona wanafuatwa wataghafirika na kupunguza mwendo,” anasema Mihaye na kuongeza,
“Kuna siku nilikuwa na abiria mwanamke napita barabara ya hospitali ya mkoa  wa Mwanza, Sekou Toure. Vijana wanamna walikuwa nyuma yangu na pikipiki yao, wakakwapua mkoba wa abiria huyo. Niliamua kumshusha na kuanza kuwafukuza.
Walikuwa  wakikata mitaa ninao, huku ninapiga kelele  za mwizi, na walipoona ninawakaribia wakautupa chini mkoba, nikauchukua na kumrejeshea abiria kule  nilikomuacha baada ya kuachana na wezi hao.”
Na kuhusu kisa cha kuachana na udereva bodaboda, anasema kuwa, siku moja saa nane za usiku, alimpakia abiria mwanamke na hakujua kuwa yule alikuwa ni sehemu  ya majambazi, “ilikuwa ni ile njia ya kutoka Ilemela Mahakamani kuja njia  ya lami, tulipokaribia sehemu yenye miti isiyo na watu wengi, yule abiria alianza kujichezesha nyuma ili  nipunguze mwendo ama kuanguka, na kwa mbele nikaona kundi la vijana wakiwa na nondo na mapanga.
“Nilipoona hivyo, nikaendesha pikipiki kuwafuata waliko ili niwagonge, wakatawanyika na kujiweka mbali  walipoona hivyo, nikashuka na kumg’amg’amia yule mwanamke kwenye pikipiki,huku nikimpiga na kumgeuza kinga endapo wangenishambulia;
“Waligundua manbo ni magumu, wakakimbia na nikabaki na yule abiria feki, nikamwambia alete hela yangu, akabisha, nikamsachi na kumkuta ana shilingi 15,000/= nikamnyang’anya, nikamwambia ondoka naye akatimka kama hana akili sawa sawa.  Na huo ndio mwisho wangu na bodaboda,” anasimulia Mihaye.
Kalima yeye anasema kwamba kwa siku hizi mambo mengi yamebadilika, uhasama wa wenye magari au madereva wa daladala na waendesha bodaboda kitu ambacho kilikuwa chanzo cha ajali nyingi, umepungua baada ya kila upande kuuheshimu mwingine.  Pia uelewa wa sheria miongoni mwa madereva wa bodboda kumeondoa pia ile tabia ya wao kufukuzana na askari wa usalama barabarani.
“Nimeshuhudia vifo vya madereva boda boda sita ama saba hivi kutokana na ajali zilizo katika mazingira haya tangu nianze kuendesha bodaboda mwaka 2010,” anasimulia Kalima ambaye kabla ya kujinunulia pikipiki yake alifanya kazi ya ajira Halmashauri ya Jiji la Mwanza kama mhudumu, na baadaye hotelini, na hivyo kujipatia fedha kwa ajili hiyo.
“Hata hivyo siku moja mwaka 2015,  nikiwa naendesha pikipiki kuelekea mjini kutoka Airport na abiria wangu akiwa dereva bodaboda mwenzagu, na wakati trafiki wameyazuia magari ya  upande mmoja wa barabara, [wakati huo barabara ya Aiport haijawa na njia mbili] ili kuruhusu basi la timu ya Mbao iliyokuwa ikifanya mazoeazi katika viwanja vya DIT hapa Mwanza, kuingia barabara kuu ili waelekee upande wa kulia kwetu,  lilikuja gari moja likiwa na mwendo mkali.
Gari hilo ni kama lilikataa amri ya trafiki na kuingia upande wetu ulioruhusiwa,  na hivyo kukutana uso kwa uso na sisi  na kutugonga. Ilikuwa ajali mbaya sana. Tulipakiwa katika magari mawili tofauti, mwenzangu akapelekwa Sekou Toure na mimi nikapelekwa Bugando [hospuali] na huko, baada ya kulazwa kama mwezi mzima wakanikata mguu,” anasimulia Kalima, na kuongeza kuwa, “ Baada ya kukatwa mguu, nilikaa siku tatu bila fahamu, baadaye nilijitambua na kujiona mwenye afya na nikawa nakula chakula kama kawaida.
Nilishtuka  baada ya kuona kama kuna wepesi usio wa kawaida kwenye mguu wa kulia, na ndipo nilpotambua kuwa umekatwa. Nilisikitika sana, wakanipa moyo kuwa, utaota na kurejea hali ya kawaida, na nikayaamini haya maneno.”
Anasema aliielewa hali hiyo baadaye na kuendelea kuisha nayo.  Ila kwa sasa anawaomba wasamaria wema kama wanaweza kusaidia  fedha za kupata mguu bandia ili maisha yake yaendee kawaaida. Anapatikana kwa namba  0786858676, mwenye kuwiwa kumsaidia anaweza kuwasiliana nae. Kwa naelezo ya awali anadai mguu bandia  unaweza kugharimu kati ya shilingi milioni mbili hadi tatu.

Na Joseph Mihangwa

LIPOISHIAI
...Ni utawala wa Chama dola na Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea. Ingawa tumeingia mfumo wa Vyama vingi, Katiba inanuka harufu ya Chama kimoja kiasi cha watu wengine kukiita Chama kilichoshinda “Chama dola”, wakati ukweli dola si ya Chama, bali ni ya wananchi!.

ENDELEA...
Mhimili wa Chama na Ujamaa kati ya mitatu umekwishavunjika; Sera za Ujamaa na kujitegemea zimevunjwa na Azimio la Zanzibar mwaka 1992; nao mfumo wa Chama kimoja umeuawa na mfumo wa Vyama vingi vya siasa tangu mwaka 1992. Mfumo huu na ule wa uchumi huria, havikuwa katika mawazo ya watunga Katiba ya 1977. Ndiyo maana, Katiba ya sasa inakinzana kwa sehemu kubwa na mengi yanayotokea nchini.
Tunachosema hapa ni kwamba madaraka makubwa ya Rais asiyeambilika, yalidumu na kuweza kufanya kazi tu kwa msaada wa mafiga mawili yaliyovunjika – [Ujamaa na Chama kimoja], na kwamba, maadam sasa msaada huo haupo tena, madaraka makubwa ya Rais yataendelea kuelea na kupwaya kwa vigezo vyovyote vya utawala wa Sheria, demokrasia na utawala bora. Na pale Rais atajaribu kutenda kwa ubunifu wake binafsi kinyume na haya, hataepuka kuitwa “dikteta”.
Tunaambiwa, nchi yetu inafuata mfumo wa Utawala wa “Westminster”, unaozingatia Mgawanyo wa Madaraka.  Chini ya mfumo huo, muhimili mmoja wa Serikali unakatazwa kuingilia kazi za muhimili mwingine ili kila muhimili uchunge mwenendo wa muhimili mwingine.  Dhana hii sasa ipo kwa jina tu kama tutakavyoona hivi punde.
Marekebisho ya hapa na pale yaliyofanyika baadaye kwenye Katiba hayakugusa madaraka ya Rais, lakini badala yake, kadri sekta ya umma ilivyozidi kupanuka na ukuu wa mfumo wa Chama kimoja kujiimarisha, ndivyo jinsi madaraka ya Rais yalivyozidi kuwa makubwa. 
Aliweza kutumia nyundo ya Chama wakati huo huo kama Rais wa Nchi, na aliweza kutumia pia ngao ya Rais kulinda Chama wakati huo huo kama Mwenyekiti wa Chama. Rais wa Nchi na Mwenyekiti wa Chama Taifa kilikuwa na hadi leo ni kitu kimoja. Na ndiyo sababu ya Chama madarakani kuitwa “chama dola”! Kwa sababu hii, madaraka ya Rais yalipanuka kinyemela kuanzia na Katiba ya Nchi, hadi kwenye Katiba ya Chama cha Siasa tawala. Kwa sababu hii, Rais asiyeambilika [The Imperial Presidency], anachukuliwa kama moja ya nguzo au misingi mikuu mitatu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, inayoendelea kutumika hadi leo.
Uhalali wa madaraka makubwa ya Rais kwa mtazamo wa Watawala wa enzi hizo, ulikuwa ni kuharakisha maendeleo kwa njia ya “udikteta” wa Mkuu wa Nchi, ili asiulizwe ulizwe.  Mtazamo huu unadumu hadi leo.
Na katika kutekeleza hilo, Katiba ilitungwa kwa lengo la kuweka madarakani mtawala mwenye nguvu za imla, kwanza kuonesha kwamba Watanganyika sasa walikuwa huru kuweza kuendesha mambo yao wenyewe.
Pili, ilikuwa ni kuwezesha Serikali kuingilia kikamilifu [na bila ya kuhojiwa] katika maisha ya kijamii na kiuchumi ya wananchi, ili kuharakisha maendeleo kwa nguvu na imla ya kiutawala kwa “kushikisha adabu” waliohoji mwenendo wa nchi na wa watawala katika “kusukuma gurudumu la maendeleo.”
Maandalizi ya uchaguzi wa kwanza wa Rais asiyeambilika yalianza Juni 18 mwaka 1962 kwa kuandikisha wapiga kura 1,800,000 katika majimbo 50 ya uchaguzi. Wagombea walikuwa wawili – Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Rais wa Chama cha TANU, na Bwana Zuberi Mtemvu, Rais wa Chama cha African National Congress – ANC. Uchaguzi ulifanyika Novemba 1, 1962 ambapo Mtemvu alishindwa vibaya kwa kupata kura 21,276, na Mwalimu Nyerere alipata kura 1,127,978.
Kuanzia hapo, Katiba ya nchi imekuwa ikiandikwa au kurekebishwa kukiwa na uwepo wa Rais, Mwalimu Nyerere vichwani mwa Waandishi wa Katiba. Hali haijabadilika.  Katiba yetu [ibara ya 63] inamfanya Rais kuwa sehemu ya Bunge la nchi kama njia ya kudhibiti demokrasia, kinyume na dhana ya Mgawanyo wa madaraka. Na ingawa mamlaka yote ya kutunga Sheria yamo mikononi mwa Bunge [ibara 64], lakini muswada wa Sheria hauwezi kuwa Sheria mpaka utiwe sahihi na Rais. Hakuna muda maalum aliopewa Rais kwa ajili hiyo; anaweza kukalia muswada kwa muda wowote atakavyo, kana kwamba yuko juu ya Wananchi kupitia Bunge.
Endapo atakataa kutia sahihi muswada asioutaka, na Bunge likashikilia msimamo wake juu ya muswada huo, Rais ana uwezo wa kulivunja Bunge na kuitisha uchaguzi mpya. Haya ni madaraka makubwa mno kwa Rais dhidi ya wawakilishi wa wananchi. Maana yake ni kwamba ingawa Bunge laweza kupitisha Muswada wa Sheria, ukweli Rais ndiye anayetunga Sheria kwa sababu ana hiari ya kukataa au kukubali Muswada wa Bunge na asiulizwe.
Rais anapogeuka kuwa Mtunga Sheria, Bunge lifanye kazi gani? Ili kulinda hadhi na ukuu wa Bunge linalowasilisha wananchi, busara inaelekeza Bunge lidhibiti bajeti yake, Tume yake ya Utumishi ina uwezo wa kupitisha miswada kuwa Sheria inapotiwa sahihi na Spika.
Kama ilivyokuwa kwenye Katiba ya Jamhuri [1962] kwa Rais kuongoza nchi atakavyo, na kuwa halazimiki kupokea ushauri wa mtu yeyote, Katiba ya sasa [ibara 37] bado inampa ridhaa hiyo, na hawezi kuhojiwa au kushtakiwa kwa vitendo vyovyote alivyofanya akiwa Rais na baada ya hapo [Ibara 46]. Pengine ni kwa sababu hii zama zetu, kumekuwa na vitendo visivyoendana na maadili ya taifa kwenye Ikulu bila ya woga, vilivyomfanya Baba wa Taifa apige kelele kwa kusema “Ikulu ni mahali patakatifu, panatakiwa paheshimiwe”, na akaonya pasigeuzwe pango la wafanyabiashara na walanguzi.
Kama lengo la kuwepo mihimili mitatu [Utawala, Mahakama na Bunge], ni pamoja na kuimarisha demokrasia, demokrasia itatoka wapi mhimili wa utawala unapodhibiti mihimili mingine?. Inapokuwa hivyo, kwa nini tuendelee kudai tunafuata mfumo wa demokrasia wa kibunge [Parliamentary Democracy], wakati vitendo vinaonesha kinyume chake?
Rais ndiye anayeteua Jaji Mkuu na Majaji [wanaosimamia mhimili wa Mahakama], Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Viongozi wengine. Kitendo cha kuteua chenyewe pekee kinamaanisha kwamba wateule hao wanawajibika kwake. Na kwa sababu hiyo mhimili wa kulinda haki [Mahakama], unawajibika kwa Rais pia. Hii inakwenda kinyume na dhana nzima ya mgawanyo wa madaraka na ya utawala wa Sheria kwa ujumla, kwa Rais kudhibiti Bunge na Mahakama, pamoja na Watendaji wake.
Kwa kusema haya, hatumaanishi kwamba kwa watawala kuvuka mipaka ya Kikatiba mara kwa mara hakuzai matunda siku zote, bali kwamba panatakiwa tamko thabiti lenye kueleweka juu ya aina ya demokrasia tunayopaswa kufuata kuweza kujipima na kuweza kupimwa pia kimataifa. Uhuru na demokrasia si lelemama, bali “UHURU”, kama alivyosema Baba wa Taifa, “ni KAZI”.
Tafsiri ya neno “demokrasia” ni pana kwa kuzingatia mahali na mazingira ya nchi. Lakini, kama Katiba ya Nchi ni hati yenye “utakaso”, na pia dira na ramani ya madaraka ya kuzingatiwa na kila mtu, basi, mfumo unaosimikwa na Katiba hiyo unapaswa kufahamika, kuzingatiwa na kuheshimiwa na wote; kinyume chake Katiba na demokrasia inageuka kuwa kejeli kwa wananchi wanaoitunga wakitarajia kwa matarajio kuona inafanya kazi. Ilivyo sasa, nchi yetu inafuata mfumo gani wa demokrasia: demokrasia ya [ukuu wa] kibunge, demokrasia ya kinasaba au ukuu wa kivikundi kwa misingi ya vyama vya siasa?
Tuseme nini zama hizi za siasa na uchumi huria na kwa Serikali kuachia nguvu za “soko” kusimamia sera na uchumi wa nchi na hivyo maisha ya watu, inapotokea mhimili wa Bunge na Utawala kuungana kuwa kitu kimoja?. Uhuru wa Mahakama utatoka wapi, kwa mfano, kwa kulazimisha chungu cha mstakabali wa nchi na demokrasia kukaa juu ya mafiga mawili badala ya matatu?
This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it.
0713-526972

MWANZA

Na Paul Mabuga

Zawadi ya  tuliyopewa na Mungu ya huduma,  uhai na maisha ya mpendwa wetu Edward Lowassa, tuliyemhifadhi katika nyumba yake ya milele hivi majuzi huko Monduli, Mkoani Arusha ina mengi ya kutufundisha, lakini zaidi ni kwamba kila binadamu anazaliwa na haki ya kusifiwa, isipokuwa huwa inaporwa na ndiyo maana inahitaji kulindwa na kutetewa.
Kwamba, binadamu hatapata sifa kwenye familia yake au watu wa karibu nae basi ataitafuta nje yao. Wakati mwingine matokeo yanaweza kujenga uhitaji wa kuilinda haki hiyo huku wengine wakiibomoa katika ushindani ambao unajaa vitimbwi. Lakini wakati mwingine, sifa hutolewa bila kufurahisha wengine.
Kuna picha jongefu fupi mtandaoni ambapo mwongeaji hamasa, anayejitambulisha kwa jina la Michael Maundi, anajizungumzia yeye kama mfano ambapo anasema, tangu wakati anasomasoma shule ya msingi nafasi yake kwenye mitihani  ilikuwa ya 160 na 180, na hata alipofaulu kwenda kidato cha kwanza shule ye sekondari Kibasila mama yake alimuuliza, “huko darasani kwenu hakuna Michael Maundi Mwingine?” Akimaanisha mama yake alikuwa haamini kama amefaulu.
“Watu wote na hasa watoto wadogo walio nyumbani tunapenda sana sifa, tusipoipata nyumbani ama shuleni tunaitafuta mitaani! Mtaa unasifia, mtaa ukipakata kete [dawa za kulevya], mtaa unakuambua mwanangu umetisha… hata .. uki[anaonyesha ishara ya kuvuta bangi] mtaaa unakuambia mwanangu mwanangu, yaani wewe bonge la Mwambaaa!” anasema akionyesha umuhimu wa kuwasifia  watoto kabla ya kupata zile zisizo na maana.
“Mtoto anafanya kitu kikubwa nyumbani  wewe hata hushangilii, hustuki,[ inatakiwa] hata kama unakijua unashangaa, heee umejuaji mwanangu! Mtoto anapata moyo wa kutafuta vitu vingine kujua ili kuhadithia, … siyo anakuja kukuelezea kuhusu mto Kirumi uko hivi na hivi, halafu wewe unamvwambia, kwa hiyo wewe ndiyo umejua leo!” anaeleza Maundi katika kadamnasi inayomtazama katika picha hiyo fupi jongefu.
Kinyume chake anasema mwalimu wake wa darasa la saba wakatti anapata hesabu alama saba kwa hamsini kwenye mtihani wa kwanza,alimwambia Maundi una akili sana ili huitumii vuzuri. Wa pili alipopata 11 ya hamsini, akamyanyua juu na kumwambia, wewe ni nomaa, wewe ni mkemia mkuu, na mtihani uliofuata alipata alama zote.
“Mtoto mdogo atakuja kukupa kile [anachokiona] unachokiamini! Ukimuaminisha anaweza [ukimsifia unampa deni kubwa sana, … lakini kimuambua mjinga  mpumbavu mende paka .. atakuwa akijisemea hata mama anajua kuwa mimi ni paka!” anasema Maundi na kuongeza kuwa watu wengi duniani wamefanya makubwa kutokana na kulelewa katika miingi hiyp ya motisha ya kusifiwa.
Pia kuna majadiliano katika mtandao wa facebook  kupitia uzi mmoja ulioanzishwa na chombo kimoja cha habari nchini Kenya, ambapo inaonekana hoja ni Tanzania angalau kucheza Afcon 2023 iliyomalizika hivi karibuni, ambapo mmoja wa wachangiaji raia wa nchi hiyo ya awali anaandika katika hali ambayo inaonyesha pengine kutofurahia sifa za nchi yake ya jirani.
“Jirani hana dollar, jirani hana umeme, jirani hajui kizungu, jirani hakushinda hata mechi moja Afcon, jirani ana shida kweli kweli,” analeza Ogeto Nyamwange katika mtandani huo. Wapo pia engi waolichangia katika mtazamo huo. Mtanzania Caroline P Mwaipungu  anajibu, “Majirani mnajikutaga wazungu etu? Kama wa ulaya vile wakati hatutofautiani shida… eti kuzungu nini?? Mko na umbea mwingi loo!
Ingawa ni utani wa kawaida ambao hata umekuwepo kwa muda sasa kati ya raia wa nchi hizi lakini umekuwa hauna madhara. Zaidi utani huu ni kielelezo cha namna ambavyo binadamu anahitaji sifa, na anapohisi inachukuliwa anaona kuna haja ya kuilinda.
Usishangae binti akiingia gharama ya usafiri kurudi nyumbani kubadili mavazi baada ya kuambiwa aliyoyavaa hayajampendeza. Tunaponunua nguo tunalipia kupendeza siyo mavazi. Hii ni hoja ya kale kina binadamu alivyo.
Tukirejea katika enzi za uhai wake Lowassa  licha kusifiwa ambako kwa hakika kulijengwa na kupendwa kutokana na wasifu wake, na hata kuwa kipenzi cha watu, lakinini pia ni ukweli kuwa katika kipindi chake cha kazi na maisha aliukutana na bête noire [tanka bete nwaa], ikiwa na maana ya hali ya  kuchukiwa na sehemu fulani ya jamii..
Katika pande zote alizokuwa katika kazi zake, alikuwa kipenzi  na kupewa  sifa kem kem kwa upande mmoja huku kwa upande mwingine akipata bête noire.  Upande mmoja wa binadamu hao hao wakimpa sifa na kumtetea kwa nguvu zote wakati wa pili ukizipopoa sifa hizo ili kumpa bête noire kwa kila gharama yoyote.
Kitu kimoja cha msingi ni kwamba wakati kunyang’anywa kwa haki ya asili ya kusifiwa kunaweza kusababisha athari za kiafya katika maisha ya binadamu, lakini mara nyingi tumekuwa hatujali na  hatutoki mbele na kuwanusuru.  Watu walioporwa sifa wanazostahili kwa haki tumekuwa  tunasubiri wakati wakiaga dunia ili kuwasifia.
Na adui mkubwa wa sifa kwa mwanadamu ni ubinafsi ambao kila mmoja wetu anao. Yaani tunajijali zaidi kwanza sisi, na tunapoona ubinafsi wetu unatishia sifa zetu, tunapambana hata kama katika kufanya hivyo tunawanyang’anya wengine stahiki zao. Siyo lazima kila sifa imfurahishe mwingine, lakini inapaswa kuwa haki ya mmiliki.

Na Dk. Deoscorous B. Ndoloi

Mpendwa msomaji, karibu tena katika makala yetu juu ya mikabala ya ushawishi, wakati wa kuzungumza katika hadhara. Tayari tumekwishaona aina saba za mikabala, kama ifuatavyo: kutishia (kutia hofu), kukaripia, kususa, kutoa mchapo au hadithi fupi (anecdote), kuuliza maswali balagha (rhetorical questions), kutangaza ole, na kutoa mlinganisho. Kabla hatujaendelea, ni vema kutambua kwamba kuorodhesha hii mikabala (kama vile inajitegemea) kunatusaidia kuielewa zaidi kuliko kuizungumzia kwa pamoja. Lakini ukweli ni kwamba katika wasilisho moja unaweza kutumia mikabala zaidi ya mmoja kulingana na lengo la wasilisho, mazingira, aina ya wasikilizaji, na mabadiliko unayotarajia kwa hadhira husika. Katika makala hii, tumalizie mada hii juu ya mikabala ya ushawishi.
Mkabaka wa aina ya nane wa ushawishi ni kufanya rejeo katika ushahidi unatokana na tafiti za kisayansi. Binadamu tumeumbwa na ‘katatizo’ kadogo ka kutilia mashaka hasa vitu ambavyo aidha hatujavizoea ama hatujawahi kuviona. Hili linasaidia wakati mwingine kwa vile huweza kuibua hali ya udadisi na kutaka kupata taarifa sahihi. Kwa mfano, inaweza kuwa vigumu katika wasilisho kuhusu afya, kuwashawishi wavuta sigara waache kwa vile kuna madhara makubwa kiafya. Kwa vile kuvuta sigara ni uraibu na siyo rahisi kuacha, wapo wasikilizaji wengine watasema, “Mbona yuko mzee mmoja anavuta sana sigara na ana umri wa miaka 80, madhara yako wapi”? Ikiwa mwasilishaji anajua yapo mawazo kama haya miongoni mwa wasikilizaji, anaweza kutoa ushawishi kwa kutumia takwimu za vifo vinavyotokana na uvutaji wa sigara. Kwa mfano anaweza kusema, “Kulingana na takwimu za Shirika la Afya Duniani, vifo vinavyotokana na uvutaji wa sigara kwa mwaka ni watu milioni nane (WHO, Januari 2022). Hawa ni kama watu wote wa Mkoa wa Dar es Salaam, wanafariki kila mwaka”. Takwimu hizi zinatisha, wapo wanaoweza kushawishika kuacha kabisa sigara. Siyo maneno ya mwasilishaji, bali ya utafiti wa kisayansi. Dhamira ya msikilizaji inaweza kumsuta ikamwambia, “Kama na hilo huliamini, endelea kuvuta”.
Mkabala wa aina ya tisa wa ushawishi ni kupeana kazi ya nyumbani (homework) baada ya wasilisho. Ushawishi huu ni tofauti kidogo kwa sababu wasikilizaji wako watashawishika baada ya kuondoka katika mhadhara. Kwa mfano unatoa wasilisho juu ya afya ya akili (mental health), na kwamba kukosa amani katika familia mara nyingi kunapandisha mhemko, mfadhaiko, msongo, shinikizo, na kupelekea kushindwa kujenga familia zenye ustawi wa mwili, akili, mali, elimu, mahusiano, afya, nk. Unaweza kuwaambia wasikilizaji wako, “Ukitoka hapa, angalia watoto mtaani wanapiganapigana kila wakati; je nyumbani kwao unakujua? Wazazi wao wakoje? Ukitoka hapa kachunguze mtu yeyote unayefikiri ana makelele sana, wakati mwingine, yasiyo na sababu. Watu wa familia yake unawajua? Wakoje? Baada ya semina hii, nataka ukachunguze watu ambao unafikiri wanahamakihamaki sana, na hawana utulivu wa kufikiri na kupambanua mambo. Angalia uhusiano wake na ndugu au marafiki zake. Utakachogundua, njoo utueleze. Kaangalie watoto ambao hawataki kabisa kucheza na wenzao, kitu ambacho kwa mtoto siyo kawaida. Chunguza wazazi wake. Ndiyo utakuja kukubalian na mimi kwamba afya ya akili, kwa kiasi kikubwa, inahusiana na kiwango cha amani anachokuwa nacho mtu”. Hapa unawapa ushawishi rejea (protracted persuasion), na watashawishika baadaye, na kila mtu kwa muda wake.

Mkabala wa aina ya kumi wa ushawishi ni kuonesha thamani ya wanaokusikiliza. Watu wote wanapenda sifa (tabia ya binadamu). Hapo awali, katika makala ya tano ya mwezi Septemba 2023, tuliona kwamba binadamu hapendi sana kuoneshwa kwamba yeye ana mapungufu, hasa pale anapoambiwa kwa namna ya kudharauliwa. Niliwahi kusema kwamba binadamu anataka kuambiwa kwamba, “Kama yai, yeye anaweza kuwa na ufa kidogo, lakini ubora wake kama yai uko palepale, likikaangwa linaliwa bila shida”. Ninachotaka kusema ni kwamba ushawishi unaweza kutokana na wewe mwasilishaji kuwahakikishia wasikilizaji kwamba wana thamani katika hilo unalolisema. Wahakikishie kwamba wewe ni mchokoza mada tu, na ni tegemeo lako kwamba una mengi ya kujifunza toka kwao. Wakitoa mchango wa mawazo, sema, “Asante, kwa mawazo mazuri, na mimi nimepata faida hapo”. Kuionesha hadhira kwamba na wewe unajifunza, siyo tu dalili ya unyenyekevu, unawashawishi hata kukubali unayosema.
Mkabala wa aina ya kumi na moja wa ushawishi ni kutumia vema mawasiliano silonge (non-verbal communication), au kuongea kwa matendo. Ili uweze kushawishi watu – zungumza kwa mdomo, lakini ongea na mwili mzima. Huwezi kushawishi watu ukiwa umeweka mikono mfukoni. Huwezi kushawishi watu ukiwa umekaa. Huwezi kushawishi watu ukiwa umesimama sehemu moja muda wote. Huwezi kushawishi watu ukiwa umenuna. Huwezi kushawishi watu ukiwa huwatazami. Kila sehemu ya mwili wako ichangie katika kutoa taarifa na maarifa. Wale wachekeshaji (comedians) maarufu wanavunja watu mbavu kwa yale wanayosema, lakini kwa kiasi kikubwa wanavyoyasema na kwa matendo yao.

Wiki ijayo tutaona kanuni za kuandaa na kutumia zana (presentation aids) wakati wa kuzungumza katika hadhara, na pengine tutakuwa tumefikia mwisho wa hii mada ya kuzungumza katika hadhara, ili tuanze mada mpya.  Tumsifu Yesu Kristu!
Itaendelea wiki ijayo.

Page 1 of 2