Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha
Japhet

Japhet

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Wazazi wametakiwa kutoa ushirikiano kwa Maparoko katika parokia zao, ili watoto wao waendelee na mafundisho ya kuwajengwa katika imani baada ya sakramenti zao.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Bikira Maria Mama wa Mungu - Vijibweni, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
“Wazazi na walezi toeni ushirikiano kwa Paroko wenu, ili watoto hawa waendelee kupatiwa majiundo, waendelee kupatiwa Mafundisho ya Imani hata baada ya kupokea Sakramenti hii ya Kipaimara,” alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.
Aidha, Askofu huyo aliwataka vijana kuwa watumishi wa Bwana kikamilifu, huku wakiitambua hadhi yao pamoja na wito wao.
Alisiwahi kuwa watumishi kweli wa Yesu Kristo, badala ya kuwa Wakristo goi goi, wala Wakristo tia maji tia maji katika maisha yao
“Kuweni watumishi kweli wa Yesu Kristo, msiwe Wakristo goi goi, wala Wakristo tia maji tia maji katika maisha yenu. Itambueni hadhi yenu na wito wenu kama Wakristo,” alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.
Aliongeza kuwa kwa kupokea Sakramenti hiyo Takatifu ya Kipaimara, sasa vijana hao wamehitimisha awamu ya kuwa watoto, akiwasihi kudumu katika imani, huku wakiyashika yale yote waliyofundishwa.
Aliwasihi kuendelea kuimarisha imani na maadili, akimsihi Paroko wa parokia hiyo kusimamia ili vijana hao waendelee kupatiwa mafundisho (majiundo), endelevu.
Askofu Mkuu Ruwa’ichi alisema kwamba kwa kuwa hizi ni zama za kelele, upo umuhimu wa kuwasimamia vyema watoto hao ili waendelee kukua katika misingi ya imani, kwani wasiposimamiwa vyema, watapotea.
Katika homilia yake, Askofu huyo aliwasihi vijana, wazazi na Waamini wote kwa ujumla, kupendana kama vile Kristo anavyowapenda, kwani Kristo amewapenda bila kujibakiza.

VATICANCITY, Vatican

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Ulimwenguni, Baba Mtakatifu Leo XIV, amesema kuwa Ekaristi ni Sakramenti ya upendo, zawadi na sadaka ya Kristo Yesu msalabani.
Papa alisema hayo katika Maadhimisho ya Dominika ya Ekaristi Takatifu, aliyoiongoza katika Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Lateran, Makao Makuu ya Jimbo Kuu la Roma.
Aliongeza kuwa hiyo ni Sakramenti ya Altare, ambapo ndipo mahali pa kukutana na Kristo Yesu katika maumbo ya Mkate na Divai, Mwili na Damu yake Azizi, na kwamba ni fumbo na muhtasari wa imani ya Kanisa, chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa.
Baba Mtakatifu alibainisha kuwa huo ni mwaliko kwa Waamini kila siku wanaposhiriki Fumbo la Ekaristi Takatifu, kuwa alama angavu ya dhamana ya Waamini kuhakikisha kwamba, wanakuwa kweli vyombo na mashuhuda wa ushirika, amani, ukarimu na upendo kwa Mungu na kwa jirani zao.
“Ikawadia saa ya majaribu, jua likaanza kuzama pale nyikani na jangwa tupu, hawakuwa na chakula cha kuutosha umati ule wote! Jua lilipokuwa linakuchwa, njaa na hofu vikaongezeka, Mitume wakamtaka Kristo Yesu auage umati ule, lakini akajibu kwa huruma na upendo wake mkuu, akitoa kipaumbele cha kwanza kwa kutangaza na kushuhudia Ufalme wa Mungu…
“Mitume walikuwa na imani haba, kwa kuogopa kwamba mikate mitano na samaki wawili, wasingeweza kufua dafu kwa umati mkubwa kiasi kile! Kristo Yesu akaizima njaa ya watu wa Mungu kwa huruma na upendo wake; akatazama juu mbinguni, akavibariki, akavimega na kuwapa wawaandikie mkutano,” alisema Papa.
Aliongeza kuwa ishara hiyo ni utambuzi wa uwepo wa Mungu kwa njia ya sala, kielelezo cha ushirika na udugu unaosimikwa na kuenziwa na Roho Mtakatifu.
Baba Mtakatifu Leo XIV alisema, “Leo hii katika Ulimwengu mamboleo kuna watu wanaoteseka na kusiginwa na baa la njaa, kielelezo cha ukosefu wa haki msingi, kunakosababishwa na kiburi na jeuri ya binadamu, kinachowafanya binadamu kushindwa kugawana kikamilifu mazao ya nchi na kazi ya mikono ya wanadamu.”
Katika Maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 2025 ya Ukristo, Baba Mtakatifu Leo XIV alisema kuwa mfano wa Kristo Yesu kuwalisha wenye njaa, ni kigezo cha utendaji kazi na huduma, ili kugawana chakula, na hatimaye kuzidisha matumaini tayari kutangaza na kushuhudia uwepo wa Ufalme wa Mungu.
Aliwasihi Waamini kufahamu kwamba, Kristo Yesu anawaalika waja wake kula na kunywa Mwili na Damu yake Azizi, ili waweze kupata maisha na uzima wa milele, kwani yeye ni chakula na kinywaji hai, na kwamba kwa kula chakula hicho, wataishi milele.
Sambamba na hayo, Baba Mtakatifu Leo XIV alikaza kusema kuwa Maandamano ni sehemu ya hija hiyo ya maisha ya kiroho, ambapo watu wote wa Mungu wanalishwa na kushibishwa na Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, huku wakimwabudu Kristo Yesu wa Ekaristi na kumpitisha kwenye barabara zao kama ushuhuda wa imani.
Aliwaalika Waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kumbeba Kristo Yesu nyoyoni mwao, kwani huyo anawashirikisha waja wake katika mpango mzima wa Ukombozi, huku akiwasisitiza kushiriki katika Karamu ya uzima wa milele.

DAR ES SALAAM

Na Nicolaus Kilowoko

Mchezaji wa zamani wa klabu ya soka ya Simba ambaye alikuwa anakipiga eneo la kiungo, Abdulhalim Humud ameendelea kusisitiza kuwa, bado ana uwezo wa kucheza ligi ya Tanzania na kufanya makubwa.
Humud alisema kuwa wapo ambao wanambeza kuhusu kiwango chake, kuwa hawezi kucheza kwa sasa katika Ligi ya NBC, ambayo imekuwa na ushindani mkubwa.
Alisema kuwa uwezo alionao kwa sasa bado anaweza kumudu vema kabisa kucheza katika Ligi kuu, kutokana na kuwa umri wake unamruhusu kucheza soka kwa kiwango kizuri.
Nyota huyo alisema kwamba wapo mashabiki wa soka ambao wamekuwa wakimbeza, wakidai umri wake umeenda hivyo hawezi kuwa bora tena, kama ambavyo alikiwasha huko nyuma.
“Mimi kwa sasa nina uwezo wa kucheza kwa kiwango bora sana katika Ligi Kuu, japo wengine wanasema umri umeenda, sasa nashangaa kama naweza kucheza vyema katika Ligi ya Zambia, nashindwaje Tanzania”, alisema Humud.
Alisema kuwa Ligi ya Zambia kama utimamu wako wa mwili hauko vizuri, huwezi kucheza kwa kuwa ni moja ya ligi yenye kasha kasha kubwa, kutokana na ubora wa klabu zao.
Humud alisema kuwa matamanio yake ni kurejea tena kucheza katika ligi ya Tanzania, lakini wapo watu wengine ambao wakati mwingine wanakatisha tamaa, na wanatamani usiwe sehemu yao.

DAR ES SALAAM

Na Nicholaus Kilowoko

Uongozi wa klabu ya soka ya Azam FC, umesema kuwa baada ya kocha kurejesha ripoti yake ya msimu mzima, wanatarajia kusajili wachezaji wa kazi watakaoisaidia timu.
Mkuu wa Kitengo cha Habari, Thabith Zakaria Zaka marufu Zakazi Zaka alisema kwamba, msimu huu umekuwa na mambo mengi na kuwafanya washindwe kutimiza malengo yao, lakini wanaamini mara baada ya kupokea ripoti hiyo, itatafsiri muelekeo wao ujao.
Alisema kuwa msimu huu unavyohitimishwa unategemea ripoti ya kocha, ambayo itawaongoza wao katika usajili wa wachezaji ambao wataisaidia timu hiyo msimu ujao.
Aliongeza kuwa kusajili kwao ni lazima, haijalishi wachezaji watawatoa katika timu zao za vijana au nje ya nchi, lakini lazima wakiimarishe kikosi chao msimu ujao kutokana na matokeo ambayo waliyapata msimu ulioisha.

Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Kalmeri Bunju, Jimbo Katoliki la Bagamoyo, Padri Dominic Somola akiwa amebeba Monstranti yenye Ekaristi Takatifu, wakati wa maandamano ya Ekaristi katika Parokia hiyo, wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika ya Sikukuu ya Mwili na Damu ya Yesu Kristo. (Picha na Yohana Kasosi)

VATICAN CITY

Hayati Baba Mtakatifu Fransisko ameacha wosia wake wa kiroho kwa Ulimwengu akisema kwamba, siku zote amekabidhi maisha na huduma yake ya Kipadri na Kiaskofu chini ya ulinzi na tunza ya Bikira Maria, Mama wa Bwana wetu Kristo Yesu.
Katika wosia wake huo Hayati Baba Mtakatifu Fransisko aliomba maisha yake ya kibinadamu yabaki yakipumzika, katika Kanisa Kuu la Bikira Maria Mkuu, huku akingojea Siku ya ufufuo wa wafu.
Alitamani kuona safari yake ya mwisho ya hapa duniani iishie mahali patakatifu pa Bikira Maria, mahali ambapo alienda kusali.
Mazishi ya Baba Mtakatifu yalifanyika Jumamosi tarehe 26 Aprili 2025, kwenye Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na kuongozwa na Kardinali Giovanni Battista Re, Dekano wa Baraza la Makardinali.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam amewataka Waamini kumtangaza Kristo, aliyefufuka kutoka kwa wafu.
Kardinali Pengo aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika ya Pasaka, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Benedicto Abate-Wazo Hill.
“Katika kumtangaza Kristo inatakiwa uwe tofauti  na wengine kwa sababu wewe umepata Sakramenti, na uwe na msimamo wa kiimani na siyo kusema tu kwa sababu ni

maneno ambayo umeambiwa au kuhadithiwa, bali aone katika maisha yako kwamba una imani hiyo iliyo thabiti,”alisema Kardinali Pengo.
Kardinali Pengo alisema kwamba Kristo alimuita kila mmoja kudhihirisha ufufuko wake katika maisha ya kila mtu, na hiyo ndio iliwaongoza wafuasi wa Bwana tangu mwanzo wake na wote walikubali kufa kwa sababu hiyo.

Dar es Salaam

Na Laura Mwakalunde

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Sana Jude Thaddeaus Ruwa’ichi amewataka Wanakwaya kutambua kwamba wanapoimba muziki Mtakatifu,  wazo sio kutumbuiza bali ni kuinjilisha.
Rai hiyo aliitoa hivi karibuni katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Utume wa Kwaya Katoliki Tanzania (UKWAKATA), Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Petro-Oysterbay, jimboni humo.
“Wanakwaya siyo watumbuizaji na kama unataka kutumbuiza, basi ni vyema kwenda kwenye mahall ya disco… lakini ukitaka kuinjilisha kwa kuishi ukristo wako na katika kanisa lako, huku ukimshukuru Mungu kwa zawadi ya kipaji alichokujalia cha kuinjilisha kwa njia ya kuimba, salia Kanisani,”alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.
Aidha, alisema kuwa kila mbatizwa anaitwa kuwa shahidi wa Kristo kwa kutumia Kipaji alichojaliwa na Mungu, akiwaasa Wanaukwakata hao, kutumia vyema vipawa vyao.

Dar es Salaam

Na Mwandishi wetu

Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Rita wa Kashia-Goba Mwisho, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Musa Kihoo, amewataka Waamini kufuata mafundisho ya Bwana Yesu Kristo, kwa sababu  yeye ni njia ya ukweli ya kwenda Mbinguni.
Padri Kihoo alisema hayo wakati wa Ibada ya Ijumaa Kuu, Kuabudu Msalaba Mtakatifu iliyofanyika parokiani hapo.
Padri Kihoo alisema kwamba Waamini wengi wanamchukiza Bwana Yesu Kristo kwa kutenda dhambi, ikiwemo kusema uwongo, umbeya, kusengenya wenzao, kunyanyasa wapangaji na ujambazi.

VATICAN CITY-Vatican
Maadhimisho ya kumtangaza Mwenyeheri Carlo Acutis kuwa Mtakatifu yamesitishwa kufuatia kifo cha Papa Fransisko.
Maadhimisho hayo yaliyokuwa yafanyike Dominika ya Aprili 27, mwaka huu yamesitishwa kusubiria kupatikana kwa Baba Mtakatifu mpya.
Kijana huyo aliyefariki dunia akiwa na umri wa miaka 15, kwa sababu ya ugonjwa wa saratani ya damu Oktoba 12, mwaka 2006 tayari ametangazwa Mwenyeheri huko Assisi Oktoba 10, mwaka 2020.
Mwili wake umekuwa ukipumzika tangu 2019, katika Kanisa la Mtakatifu Maria Mkuu (Maria maggiore), Assisi.
Kwa njia hiyo Ofisi ya Waandishi wa Habari ya Vatican imefahamisha kwamba, Adhimisho la Ekaristi Takatifu na ibada ya kutangazwa kuwa Mtakatifu iliyopangwa kufanyika katika Maadhimisho ya Jubilei ya Vijana, imesitishwa.