Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

MADRID, Hispania
Mkurugenzi Mtendaji wa Saudi Pro League, anadai uhamisho wa Vinicius Junior ‘ni suala la muda tu,’ huku Real Madrid wakipania kupata ofa nyingine kubwa.
Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Brazil, akiwa na umri wa miaka 24 tu, tayari ameona kuhamia Mashariki ya Kati kunakisiwa.
Imedaiwa kuwa kifurushi kilichovunja rekodi cha thamani ya Euro bilioni 1 (£854m/$1.1bn) kinawekwa akilingana katika ligi ambayo tayari inawahesabu magwiji wa Real Cristiano Ronaldo na Karim Benzema ndani ya safu yake.
Omar Mugharbel, Mkurugenzi Mtendaji wa Saudi Pro League, anaamini kwamba Vinicius atapita njia sawa ya kazi, wakati fulani katika siku zijazo zisizo mbali sana.
Kuvutiwa na Ligi ya Saudia kunaendelea kuimarika kote ulimwenguni, huku Mugharbel akiwa na imani kuwa wanaweza kushindana na timu zinazoongoza barani Ulaya.
Aliendelea kusema: “Sisi ni ligi namba moja barani Asia, lakini tunataka kuwa sehemu ya 10 bora duniani. Sasa hivi siwezi kukuambia tulipo. Tunapaswa kusubiri hadi mwisho wa msimu”.

MIAMI, Marekani
Kocha wa klabu ya soka ya Inter Miami Javier Mascherano amejibu maoni ya Neymar kuhusu uwezekano wa kuungana tena na Lionel Messi na Luis Suarez katika klabu ya Inter Miami.
Akizungumza na vyombo vya habari, Mascherano alisema kuwa hawawezi kumzungumzia Neymar kwa sababu hawana lolote, japokuwa ni wazi kwamba Neymar ni mchezaji mkubwa.
Mascherano alisema kwamba kila kocha duniani anamtaka, lakini kwa sasa, Ligi yao inatawaliwa kuhusu kikomo cha mshahara kwa wachezaji, hivyo kwao kwa wakati huu, haiwezekani kujaribu kufikiria juu yake.
Neymar amekuwa akihusishwa na uwezekano wa kuondoka Al-Hilal msimu wa joto, huku timu hiyo ya Saudi Pro League ikiripotiwa kutokuwa na uwezekano wa kuongeza mkataba wake kwa mwaka mwingine.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 32, amesalia kimya kuhusu mustakabali wake, huku akitarajia kupata tena utimamu kamili na kujenga mdundo ufaao kabla ya kutamba na Brazil kwenye Kombe la Dunia la 2026.
Neymar amekuwa akihusishwa na kutaka kujiunga na klabu ya Ligi Kuu ya Soka ya Inter Miami ili kuungana na wachezaji wenzake wa zamani wa Barcelona Messi, Suarez, Jordi Alba na Sergio Busquets, na kuchochea tetesi za uhamisho wiki ya jana.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Mshambuliaji wa Timu ya Taifa ya Tanzania “Taifa Stars” Simon Msuva amefunguka kuwa hafikirii kurejea nchini kwa miaka ya hivi karibuni kutokana na kuwa bado anajiona ana uwezo wa kuendelea kupambana katika soka la ushindani nje ya nchi.
Msuva alisema kuwa pamoja na umri wake wa miaka 31, lakini haumfungi yeye kutundika daruga hivi karibuni na kufungua milango ya kurudi kucheza katika Ligi Kuu Tanzania.
Alidai kuwa muda ukifika atarejea nchini, ila kwa sasa bado ana njaa ya kutafuta fedha, na ikitokea amerudi Tanzania basi itakuwa ni mipango tu ya Mungu, ila kwa sasa bado sana kurejea nchini, kwani anatamani kuendelea kusakata kabumbu kwa miaka mingi zaidi nje ya nchi.
Alisema kuwa kwa sasa yeye maamuzi yake ya kuendelea kupambana nje ya nchi ni kuhakikisha anatafuta hela kwa kila hali, kwani bado ana nguvu kuliko vijana ambao kwa sasa wanaonekana wako vizuri uwanjani.
“Itakapofikia, nitarudi tu Tanzania wala Watanzania wasijali, ila kwa sasa bado sana naitafuta hela Waswahili wanasema kwa sasa nina njaa, kwani nataka kuendelea kutafuta hela sana, na wala siyo kurudi nchini kwa sasa”, alisema Msuva.
Alisema kuwa wakati ukifikia, ataweka wazi wazi kuwa ni wapi atakapomalizia soka lake, kama ni Simba au Yanga, ila kwa sasa bado hajafikiria kurudi, kwani mipango yake ni kuendelea kupambana kukusanya sana fedha.
Aidha, aliweka wazi kuwa maamuzi hayo ni ya kwake, na wala siyo ushauri wa mtu mwingine yeyote, kwani anachokifahamu ni kuwa muda bado unamruhusu kuendelea kuonekana sana uwanjani kutokana na uwezo aliokuwa nao.
Msuva alisema kuwa soka lake lazima atalimalizia Tanzania, hivyo kuhusu kuchaguliwa timu ya kucheza pale ambapo atakaporejea, siyo kitu ambacho atakiwekea kipaumbele, kwani anatamani kumaliza soka lake kwa heshima ili historia yake iendelee kuandikwa.
Aliendelea kudai kuwa siyo ndani ya miaka mitatu au minne ya hivi karibuni kurejea nchini, kwani bado ana nguvu za kutafuta hela katika soka la Kimataifa.
“Hayo ni maamuzi yangu mwenyewe, na siyo ya mtu mwingine kunichagulia nikacheze Simba au Yanga, kwani nina nguvu sana ya kukimbia zaidi ya wachezaji wengine vijana. Hivyo, sijachoka kama wengine wanavyodhani”, alisema Msuva.
Msuva ni mmoja ya wachezaji waliofanikiwa kuisaidia Taifa Stars kufuzu kucheza michuano ya Afcon mwaka 2027, na amekuwa msaada mkubwa katika timu hiyo kutokana na uwezo wake kuwa mkubwa.
Katika misimu ya karibuni, Msuva amekuwa akihusishwa kurudi katika klabu za nyumbani Tanzania lakini mwenyewe amesema bado hajaamua, na Watanzania wasiwe na wasiwasi ni wapi atakapocheza, kwani atahitaji muda wa kufikiria juu ya kucheza Simba au Yanga.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam limepata Parokia mpya tatu, na hivyo kufikisha idadi ya Parokia 170 na kulifanya jimbo hilo kuwa na parokia nyingi ikilinganishwa na majimbo ya Kanisa Katoliki nchini.
Parokia mpya ambazo awali zilikuwa Parokia Teule, ni Parokia ya Mtakatifu Karoli Lwanga - Mwongozo, inayozaliwa kutoka Parokia ya Gezaulole, ambayo Paroko wake ni Padri Miki Mbuku, Parokia ya Mtakatifu Stephano - Makurunge, inayozaliwa kutoka Parokia ya Kiluvya, ambayo Paroko wake ni Padri Amani Shirima, na Parokia ya Bangulo, iliyozaliwa na Parokia ya Mt. Padri Pio, Ulongoni, ambayo Paroko wake ni Padri Daniel Matungwa.
Hayo yalifanywa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu hilo, Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi OFMCap, wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Daraja Takatifu ya Ushemasi kwa Mafrateri 11 katika Parokia ya Roho Mtakatifu – Kitunda, jimboni humo.
Mashemasi hao wapya waliopokea Daraja hiyo Takatifu, ni Shemasi Benjamin Maganga Bundala, Shemasi Francisco Benedicto Chabili, Shemasi George Arnold Mbago, Shemasi Josephat Wilson Mlacha, Shemasi Emmanuel Lazaro Mbuya, Shemasi Gabriel Victor Kihondo, Shemasi Richard Osvaldo Villar Zorilla na Shemasi Mark Clement Xavier, wote wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam.
Wengine ni Shemasi Christian Leonard Mlela- MI, Shemasi Charles Msabila- MI, na Shemasi Kanuth Martin Nyoni -MI, wote wa Shirika la Wahudumu wa Wagonjwa, yaani Wakamiliani.
Askofu Mkuu Ruwa’ichi alifanya mabadiliko ya Mapadri katika baadhi ya Parokia za Jimbo Kuu hilo, ambapo Padri Charles Kayumba amekuwa Paroko wa Parokia ya Misugusugu, Padri Venance Shiganga Paroko Msaidizi wa Parokia ya Kibiti; Padri Canisius Hali, Paroko Msaidizi wa Parokia ya Muungano; na Padri Baltazar Mbwale amekuwa Paroko Msaidizi wa Parokia ya Makongo Juu.
Katika nasaha zake, Mchungaji Mkuu huyo wa Jimbo aliwahimiza Mapadri hao kuendelea kujituma na kuwajibika ipasavyo katika maeneo yao wanayofanyia kazi za kitume, ili waweze kutekeleza vyema Utume wao.
Awali, katika homilia yake Askofu Msaidizi wa Jimbo hilo, Mhashamu Stephano Musomba aliwataka Mashemasi hao wapya kutambua kwamba kwenye sehemu ya Liturujia, wana nafasi kubwa, hivyo ni wajibu wao kutangaza Habari Njema kama walivyoagizwa.
“Lakini Shemasi, kwenye sehemu ya Liturujia, una nafasi kubwa vile vile. Kuna sehemu kuu tatu zinazoongea na wewe mwenyewe unazitumia. Lakini hizo ni kwa ajili ya Tafakari la Maisha ya Kikristo katika Liturujia…
“Sehemu ya kwanza, ukiwa kwenye Misa, Shemasi wewe ni wa kutangaza Habari Njema, unapokuwa untangaza Habari Njema, furahia sasa, tangaza kwa umakini Habari Njema kwa watu, na unaposoma hivyo, usome maisha yako ya Kikristo na Ukuhani wako,” alisema Askofu Musomba.
Aliongeza kuwa hata wanapotamka juu ya kutakiana amani, wanatakiwa kuhakikisha kwamba hata wao wenyewe wanakuwa na amani hiyo ndani ya mioyo yao, kwani huo ndio Umisionari.
“Unachokitamka, ‘tutakiane amani’, au ‘mpeane amani’, basi kitoke moyoni mwako nayo amani hiyo, lakini ya tatu, nendeni na amani, unapomalizia misa, unaposema nendeni na amani, inamaanisha unatumwa kutangaza Habari Njema, unawatuma watu watangaze Habari Njema, na wewe mwenyewe unatakiwa kutangaza Habari Njema, lakini hilo lote linaonyesha Umisionari, ambalo vile vile ni dhamiri ya Kanisa, Kanisa la Kimisionari,” alisema Askofu Msaidizi Musomba.
Vile vile, Askofu Msaidizi Musomba alibainisha kwamba Waamini wanapomtangaza Yesu Kristo, hawatakiwi kuwa kama wanakwenda sokoni, bali wanatakiwa kuwashirikisha wengine yale wanayoyaishi wao.
Aliwasisitiza Mashemasi hao wapya kutimiza majukumu yao, wakifahamu kwamba sasa wamepokea Daraja Takatifu, kwani ndani ya Daraja hilo, kuna changamoto zake.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mhashamu Henry Mchamungu amewataka Waamini watambue kazi ya Kanisa ni kumfanya mtu aweze kujitafakari na kuwa safi mbele ya Mungu.
Askofu Mchamungu alisema hayo wakati wa Ibada ya Masifu ya Jioni, kiapo cha useja na kukiri imani kwa Mafrateri wanane katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu, Jimboni humo.
“Mnatakiwa kutambua Utume wa Kanisa ni kuwasaidia watu waishi katika nuru, kwani hata Kristo alikuja kutuongoza ili tuweze kutembea katika mwanga,” alisisitiza Askofu Mchamungu
Alisema pia kwamba mtarajiwa wa Ushemasi au Upadri wa kudumu kabla ya kupokea Daraja Takatifu lazima afanye kiapo cha useja katika ibada, na tena hadharani ikiwa ni sheria iliyowekwa.
Askofu Mchamungu aliendelea kusema kuwa hapo awali kulikuwa na aya mbili, lakini kifungu na.1009 kiliongezwa aya ya tatu ambayo ilieleza kuwa wahudumu wanaopewa Daraja la Uaskofu au Padri, wanapewa uwezo au utume wa kutenda katika nafsi ya Kristo (In Persona Christi).
Sambamba na hayo alisema kwamba wale wa Daraja la Ushemasi, nao wanapewa nguvu za kulitumikia Taifa la Mungu katika Liturujia ya Neno na upendo.
Pia, aliwataka watambue kuwa Shemasi ni Mkrelo na siyo Kasisi, huku akiwahimiza wawe katika imani iliyo thabiti, na siyo kuhangaika kwa wahubiri tofauti badala yake wasimame katika imani yao na mafundisho yake.
Askofu Mchamungu aliwasihi wawe ni watu wenye manufaa, na kufaa katika kazi kusaidiana na Askofu na kusema inapoonekana hana manufaa hatapewa daraja.
Vile vile aliwataka Mafrateri kuwa na nia sahihi kwa kuwa wasaidizi wa Askofu kwa kumsaidia katika kuchunga kondoo wake kwa uadilifu (haimaanishi Maaskofu Wasaidizi).
Mbali na hayo, lazima awe na elimu ya kutosha kabla ya kupewa daraja kwani haiwezekani asimalize kupata elimu na Askofu akampa daraja.
Aliendelea kusema kwamba anayepewa daraja, lazima awe na nidhamu mbele za watu, na watu wamheshimu, na akionekana haheshimiki na watu hataweza kupatiwa daraja la Upadri.
Askofu Mchamungu aliwataka Mafrateri wawe na fadhila za Kimungu, kwani itawasaidia katika kutekeleza majukumu yao vyema, bila matatizo.
Pia aliwataka Waamini wazidi kuwaombea Mafrateri hao{sasa Mashemasi}kwa Mungu, ili waweze kuishi vyema viapo vyao vya kumtumikia Mungu siku zote za maisha yao.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Dekano wa Dekania ya Mtakatifu Thomas More ambaye ni Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Kizito, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Romuald Mukandara amewaasa waamini kumtolea Mungu Sadaka safi.
Padri Mukandala alisema hayo hivi karibuni wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Tokeo la Bwana, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Kizito-Kilongawima.
“Mnatakiwa kumtolea Mungu sadaka ya kupendeza na siyo kufanya maigizo, huku ukitazama zaidi kipato chako na kiasi unacho mtolea Mungu kama shukrani,”alisema Padri Mukandala.
Aidha,alisema mwaka huu ni mpya kila muamini anatakiwa kujitafakari mwenyewe wapi amejikwaa na kumkwaza Mungu, kwa mwaka uliyopita kwa matendo mbalimbali.
Padri Mukandara aliwasihi waamini kusahihisha makosa yao kwa kufuata anacho kihitaji Mungu, na kusema  kama, mwizi, mchoyo, mkorofi, na kama hawajafunga ndoa Takatifu ama kutolipa Zaka wabadilike sasa.
Alisema kwamba Dekania na Parokia anayoiongonza anataka kila Mwanakwaya anayeimba mziki Mtakatifu kanisani kujitahidi kufunga ndoa hasa kwa wale wenye kuishi uchumba sugu.
Kwa mujibu wa Padri Mkandala wanakwaya wanatakiwa kuachana na maisha ya uchumba sugu, kwani wao ni vioo vya jamii.
Aidha, aliwataka waamini kutambua kwamba katika kuimba wanasali mara mbili, akiwasihi wapokee Sakramenti Takatifu.
Naye Padri Josephat Utouh, ambaye ni  Mkuu wa Chuo Cha Ufundi Cha Don Bosco_Jimbo Katoliki la Iringa, aliwataka waamini kuacha tabia za kukumbatia mambo yasiyofaa.
Hata alisema waamini hao wanatakiwa kuhakikisha wanaiishi Imani yao, Katoliki pasipo kutangatanga katika madhehebu mengine.
Padri Utouh aliendelea kusema waamini inawapasa kuwa na upendo kwa wanadamu akiwasihi kuachana na chuki.

DAR ES SALAAM

Na Celina Matuja

Waamini wametakiwa kuamua wenyewe kutoka ndani ya mioyo yao  kumtolea Bwana Yesu Kristo, maisha yao kwa imani safi, moyo wa upendo na maadili bora.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Sana Jude Taddaeus Ruwa’ichi wakati akitoa Homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara iliyofanyika Parokia ya Mtakatifu Antony Maria Claret, Kimara Michungwani.
Askofu Ruwaich’i amewashauri na kuwataka kila mwamini mfuasi wa Kristo kujipanga kumtolea Yesu maisha yake akimtambua kuwa ni Bwana na Mungu wake.
“Maisha ya Ufuasi yanatakiwa kuenda sambamba na Matendo mwamini huna budi kumuungama Kristo kwa kumpa maisha yako kwa imani safi, moyo wa upendo, maadili mazuri,”alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.
Aidha alibainisha kwamba MamaJusi watatu Merkioli, Gaspary na Baltazari walimtolea Yesu zawadi, ambazo zinambakisha, katika ukuu wake, na zawadi hizo ni Ubani ambao unawafanya wamuungame Yesu kuwa ni Bwana na Mungu wao,
Alisema waamini wa sasa wanatakiwa pia kumtambua Yesu Kristo kuwa ni Bwana na Mungu wao, kwani Mama Jusi hao pia walimtolea  Yesu Zawadi ya dhahabu ambayo inaelezea ufalme na walimtolea zawadi hiyo kwa kutambua kuwa ni Mfalme wa ulimwengu.
Na zawadi ya tatu Askofu Mkuu aliitaja kuwa ni Mane Mane (Marashi au Mafuta mazuri) ambayo yanatumiwa na watu na kwa kumtolea marashi hayo waliashiria kifo chake  Masalabani tena cha aibu na atakaye fufuka kwa ajili ya ukombozi wa watu wote, kwa maana hiyo Yesu Kristo alijidhihirisha kwa ulimwengu kuwa ni Mungu na mwokozi wa ulimwengu.
Askofu huyo, alisisitiza kwa waamini kuendelea kumkiri Yesu katika maisha yao kuwa ni Bwana na aliyeshinda dhambi, mauti na aliyeukomboa ulimwengu.
Alisema kila mwamini apende kujipambanua na kuishi maisha ya Mwana wa Mungu kama mtu aliyekombolewa na sio kuishi kiholela bali wenye imani thabiti, usafi wa moyo na sahihi.
Kwa upande wa Waimarishwa Askofu Mkuu Ruwa’ichi, aliwataka vijana hao kuzingatia ufupisho wa habari njema ya wokovu kwamba Kristo aliteswa, Kristo alikufa, amefufuka ni mshindi na mtukufu.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba, akiwaombea Mashemasi wapya 11 baada ya kupokea Daraja Takatifu la Ushemasi wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Ushemasi, iliyoadhimishwa katika Parokia ya Roho Mtakatifu, Kitunda, jimboni humo. (Picha na Yohana Kasosi)

ZANZIBAR

Na Salum Ali

Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali inajipanga kwa ujenzi wa Maghala ya kuhifadhia chakula ili kuwa na uhakika wa chakula.
Amesema kuwa kujitokeza kwa Sekta binafsi kuanza kujenga ghala ni jambo linalopaswa kuungwa Mkono.
Rais Dk. Mwinyi alisema hayo alipofungua ghala la kuhifadhia chakula Gando, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba linalomilikiwa na Kampuni ya Yasser Provision.
Aidha Rais Dk. Mwinyi alisema Serikali inalenga kuwapunguzia mzigo wa gharama Wafanyabiashara wanaoleta chakula nchini ili kuwepo kwa Unafuu wa bei kwa Wananchi.
Rais Dk. Mwinyi alielezea njia nyengine ni kuwa na Ushuru Maalum kwa Bidhaa zinazopelekwa Pemba .
Dk. Mwinyi alibainisha kuwa mpango wa kuifungua Pemba kiuchumi una dhamira thabiti ya kuhakikisha bei za bidhaa muhimu zinashuka na kutoa unafuu wa maisha kwa Wananchi.
Alisema ujenzi wa Bandari za mkoani, Shumba Mjini na Wete ambao utaanza karibuni ni miongoni mwa hatua muhimu ya kuwawezesha Wafanyabishara kuleta mizigo yao moja kwa moja Pemba kutoka nchi wanazoagiza ili kupunguza gharama za mzunguko wa Usafirishaji.
Hata hivyo, Dk. Mwinyi alisema Serikali inajipanga Kutafuta njia bora za kupunguza gharama za chakula kwa Wananchi wa Pemba.

DODOMA

Na Mwandishi Maalum

Serikali imegawa mashine mpya 185 zenye thamani ya Shilingi bilioni saba  kwa ajili ya uchunguzi na ugunduzi wa vimelea vya ugonjwa wa Kifua Kikuu ili kutokomeza ugonjwa huo nchini, ifikapo mwaka 2030.
Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Afya, Jenista Mhagama, kwenye hafla ya ugawaji wa mashine hizo iliyofanyika katika Kituo cha Afya Chamwino, Dodoma, iliyoenda sambamba na uzinduzi wa Mpango Harakishi wa Kuibua Wagonjwa wa Kifua Kikuu katika Halmashauri 76 za Mikoa tisa.
Waziri Mhagama alisema kuwa Tanzania inafanya vizuri kwenye mapambano dhidi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu, ambapo kwa sasa ni nchi ya sita kati ya nchi zote zinazofanya vizuri, lakini bado juhudi zinaendelea ili kufanya vizuri zaidi kwa kuwa bado tupo ndani ya nchi 30 zenye maambukizi makubwa.
“Ugonjwa wa Kifua Kikuu bado ni ugonjwa tishio nchini na ulimwenguni kwa ujumla, kwa kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi 30 zenye maambukizi makubwa ya ugonjwa huo, ambazo kwa pamoja zinachangia asilimia 87 ya wagonjwa wote wa Kifua Kikuu Duniani,” alisema Waziri Mhagama.
Alisema, “Tanzania ilikadiriwa kuwa na wagonjwa wapya wa Kifua Kikuu 122,000, ikiwa ni sawa na wagonjwa 183 kwa kila watu 100,000, ambapo kwa mwaka 2023, Tanzania iliweza kugundua na kuwaweka katika matibabu wagonjwa 93,250, ikiwa ni sawa na asilimia 76 ya wagonjwa 122,000 waliokadiriwa na Shirika la Afya Duniani (World Health Organization: WHO) kuwepo nchini.
Alisema kuwa hali hiyo imeleta msukumo mkubwa ndani ya Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Sekta katika kuongeza juhudi za kupambana na Kifua Kikuu.
Kwa kuzindua mashine hizo, Tanzania inaendelea kuimarisha mtandao wa huduma za uchunguzi na ugunduzi wa vimelea vya Kifua Kikuu kwa njia ya vinasaba ambapo sasa kutakuwa na jumla ya mashine 569 zenye uwezo wa kupima vimelea vya Kifua Kikuu pamoja na usugu wa dawa kutoka mashine 384 zilizokuwepo mwaka 2023, sawa na ongezeko la asilimia 48.
Katika hatua nyingine Waziri Jenista alizindua Mpango Harakishi wa Kuibua Wagonjwa wa Kifua Kikuu kwenye Halmashauri 76 katika Mikoa 9, amabyo kwa 2024 imeonyesha kuwa na kiwango kidogo cha uibuaji wa wagonjwa, ikilinganishwa na ilivyokuwa katika miaka ya nyuma.
Waziri Jenista aliitaja mikoa hiyo kuwa ni Dar es Salaam, Dodoma, Geita, Kagera, Mara, Ruvuma, Shinyanga, Simiyu na Tanga
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Janeth Mayanja, aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuboresha huduma za afya nchini.
Alisema kuwa mashine hizo zilizotolewa, zitakwenda kusaidia katika utambuzi wa mapema wa wagonjwa wa Kifua Kikuu, hivyo kuibua watu wengi zaidi wanaougua ugonjwa huo, na kupata tiba mapema.
Naye Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dk. Ahmad Makuwani alisema kwamba licha ya ugonjwa huo kuendelea kuwa tishio, Tanzania imepiga hatua kubwa katika kukabiliana na Kifua Kikuu, ikiwa ni miongoni mwa nchi sita (6) zinazofanya vyema katika mapambano.
Dk. Makuwani alisema kuwa juhudi kubwa sasa zinaelekezwa katika uibuaji wa wagonjwa wapya wa Kifua Kikuu, na Serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika teknolojia ya matibabu, hasa kwenye vifaatiba, hivyo sasa tuna jukumu la kutoacha mtu nyuma kwenye mapambano hayo ya kutokomeza Kifua Kikuu ifikapo mwaka 2030.