Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

Padri Denis Kunambi, Paroko wa Parokia ya Roho Mtakatifu Segerea, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam akikabidhi vitendea kazi kwa Kamati Tendaji ya Kigango cha Kuzaliwa Bikira Maria, Kisukuru, Parokia ya Roho Mtakatifu, Segerea, wakati wa Misa Takatifu ya Uzinduzi wa Kigango hicho.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba -OSA, akimbatiza mtoto Kiernani James katika Parokia ya Mtakatifu Boniventura, Kinyerezi jimboni humo wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ambapo watoto 93 walibatizwa, na Watoto 43 walipata Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. (Picha na Yohana Kasosi)

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu akiumwagia maji mti baada ya kuupanda katika Parokia ya Mtakatifu Cesilia, Kisarawe II, Kigamboni jimboni humo. Wengine ni Mapadri, Viongozi wa Halmashauri ya Walei, na baadhi ya Waamini. (Picha na Yohana Kasosi)

Baadhi ya Waamini wa Parokia ya Mtakatifu Yakobo Mkuu-Mtume, Kijitonyama, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakitoa sadaka kwa Mtoto Yesu katika Pango alimolazwa, wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Mkesha wa Krismas parokiani hapo. (Picha na Yohana Kasosi)

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Utume wa Wanaume Katoliki (UWAKA) wametakiwa kujadiliana na kupambanua kuhusu mambo msingi, ili waendelee kuwa nguzo imara katika Kanisa.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Padri Vincent Sabiit –SDS, wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Siku ya UWAKA (UWAKA Day) Parokia ya Mtakatifu Polycarp Askofu na Shahidi – Kilamba, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam.
“Ipo haja ya UWAKA kujadiliana na kupambanua juu ya mambo mbalimbali yenye tija, ili muendelee kuwa nguzo imara katika Kanisa...
“Katika kujadiliana huko, ipo haja ya kujadiliana pia kuhusu mambo yanayomhusu Mungu, ikiwemo kuwatia moyo wale wote wanaochechemea kiimani,” alisema Padri Vincent.
Padri huyo aliwasihi UWAKA kutenga muda na kuamua kujadili mambo yenye tija, huku wakiepuka kuwa na mijadala inayosababisha mipasuko na huzuni katika maisha ya watu.
Pia, aliwasisitiza kusaidiana wao kwa wao, huku wakihakikisha pia wanawasaidia vijana, hasa wale wanaosumbuliwa zaidi na malimwengu katika maisha yao.
“Sisi kama UWAKA tunaposherehekea leo, tunapaswa kujiuliza kwamba, je, kweli sisi ni nguzo imara? Je, sisi ni nguzo iliyosimama sawasawa au imeelemea upande mmoja na inataka kuanguka?
“Tukumbuke kwamba tunalo jukumu kubwa la kuendelea kujadiliana juu ya mambo yaliyo mema, ili tuzidi kuwa nguzo imara katika Kanisa letu na katika familia zetu, na pia kuweza kuwa na vijana bora watakaolisaidia Kanisa letu siku zijazo,” alisema Padri huyo.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo ya Kilamba, Padri Timothy Nyasulu Maganga alimshukuru Padri Vincent kwa homilia yake aliyoitoa katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu.
Padri Nyasulu aliwashukuru UWAKA kwa kufika kwa wingi katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu, akiwasihi kuendeleza umoja na mshikamano wao, ili kuendelea kukuza chama hicho cha kitume parokiani hapo.
Naye Mwenyekiti wa UWAKA Taifa, Cassian Njowoka, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika siku hiyo ya UWAKA Parokiani hapo, aliwapongeza wana UWAKA wa Parokia hiyo kwa kuandaa Adhimisho hilo la Misa Takatifu ya Siku yao.
Njowoka aliwashauri wanaume kujiunga na chama hicho cha kitume cha UWAKA, kwani kuna faida kubwa watakazozipata ndani ya chama hicho, ikiwemo kusaidiana wakati wa magonjwa na matatizo mengine.
Vile vile, alitumia nafasi hiyo kuwaasa Wanaume Wakatoliki na Waamini wengine, kushiriki katika suala zima la Uchaguzi Mkuu mwaka ujao 2025, ikiwemo kujiandikisha na kupiga kura ili kuwachagua viongozi watakaowaongoza.
Aliwasisitiza pia kuwaunga mkono Waamini wenzao pale wanapohitaji kugombea nafasi wanazozihitaji, kwani kwa kupitia viongozi hao, watampeleka Kristo katika nafasi watakazozipata.
“Kwa hiyo, tunaaswa na Mababa tujitokeze, tujiandikishe kwa wingi, tupige kura, na kama una sifa ya kupigiwa kura, jitokeze ugombee. Na kama tunaona mwenzetu amejitokeza anataka kugombea nafasi fulani, ‘tum-support’ tusianze kupambana naye, ili ampeleke Kristu katika nafasi ambayo yeye atakuwa ameipata,” alisema Mwenyekiti huyo wa UWAKA Taifa.
Aliongeza kwamba Mungu Mwenyezi amewapa Wakristo Wakatoliki uwezo mkubwa wa kutambua mambo mbalimbali, hivyo yeyote atakayejitokeza, awe mwanaume au mwanamke, ana haki ya kuungwa mkono katika nafasi anayowania.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa UWAKA Parokia ya Kilamba, Venance Kavishe, ambaye pia ni Mwenyekiti UWAKA Dekania ya Mbagala, alimshukuru Padri Timothy Nyasulu Maganga kwa kuendelea kuwaunga mkono katika kila wanalolifanya wana UWAKA parokiani hapo.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba- OSA, amewataka Waamini kuachana na tabia na mazoea ya kushiriki na kupokea Sakramenti ya Ekaristi Takatifu bila kujiandaa.
Wito huo aliutoa hivi karibuni wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Uzinduzi wa Kigango kipya cha Kuzaliwa Bikira Maria – Kisukuru, Parokia ya Roho Mtakatifu - Segerea, jimboni humo.
“Mkristo lazima ujitakase ukiwa msafi wa roho ili ushiriki chakula cha Bwana. Huyu ni Mungu, lazima ujinyenyekeze kwake ukiwa mkamilifu. Wakristo muwe watu wa kujitakasa muda wote kwa sababu, isipojiandaa mkiwa wenye usafi wa Roho na wenye Imani Moja Takatifu ya Kristo, lazima mjichunguze kwanza mnaishije hapa Duniani kwa imani hii ya Ukristo wenu. Ndugu zangu Waamini, huu Ukristo tuutumie vizuri, maana ndiyo njia yenye ukweli wa kutuongoza katika maisha yetu,” alisema Askofu Musomba.
Aidha, Askofu huyo aliwasihi Waamini wenye tabia ya kutoa mimba au kuzuia ili wasipate mimba, watambue kwamba wametenda dhambi mbele za Mungu.
“Waamini wenye kutoa mimba au kuzuia wasipate mimba wajue kwamba wametenda dhambi kubwa, wameua. Kwa hiyo msifanye hivyo. Wale wenye tabia hiyo, Mungu amewaleta ninyi hapa duniani ili mumtumikie na umtambue, kwa nini ninyi leo mnamzuia mwenzenu wasizaliwe? Acheni kabisa kufanya hivyo,” alisema Askofu Musomba.
Vile vile, aliwaasa Waamini kujiandaa vyema kwa ajili ya kumpokea Masiha, wakitambua kwamba Masiha anazaliwa kwa ajili yao, hivyo wawe tayari kwa ajili ya mapokezi yake, huku wakiwa wasafi wa mioyo, pamoja na kuachana na tabia ya kuwa watu wa chuki.
“Mama Bikira Maria alipopewa taarifa kuwa ni mjamzito, utazaa mtoto mwanaume ingawa alishangaa pia alishtuka, lakini alipokea kwa imani moja kubwa, je, wewe mama leo ungeambiwa hivi ungesema nini? Tuwe watu wa imani kupokea kitu kwa unyenyekevu na furaha, huku tukiwa watu wa imani na unyenyekevu mkubwa,” alisema Askofu huyo.
Askofu Musomba aliwaasa Wanakigango hicho kuwa watu wa kupendana na kuheshimiana, kwani wakifanya hivyo, watafika mbali kimaendeleo katika Kigango chao.
“Mkifanya hivyo, mtafika mbali katika Kigango hiki, ili mje mfikie kuwa Parokia kamili. Mtambue kwamba hakuna Kigango kinachozinduliwa na Askofu, Kigango huwa kinazinduliwa na Paroko tu, lakini ninyi leo mmepata bahati kubwa sana kuzinduliwa na mimi Askofu, msiniangushe, mjitahidi kukua haraka, mjenge kanisa kubwa pia mjenge nyumba ya Mapadri haraka sana...
“Nimefurahishwa sana na makubaliano yenu ninyi Maparoko wawili katika Parokia hizi mbili, Parokia ya Makoka na Parokia ya Segerea, mmetoa Jumuiya zenu na kuunda Kigango, mmefanya vizuri sana, huu ndio Ukristo unaotakiwa, siyo kuwa na malumbano,” alisema Askofu.
Askofu Msaidizi, Mhashamu Stephano Musomba alitangaza kuwa Kigango hicho kitahudumiwa na  Mapadri wa Parokia ya Roho Mtakatifu, Segerea.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo ya Segerea, Padri Denis Kunambi aliwaomba Waamini wa Kigango kipya wampe ushirikiano ili waweze kufikia maendeleo zaidi katika Kigango hicho.
Padri Kunambi alisema kuwa Kigango hicho kimezaliwa kwa baraka kubwa, kwa sababu eneo hilo lilinunuliwa na Parokia ya Segerea kwa lengo la kujenga shule kama mradi wa Parokia, lakini sasa wazo hilo limegeuka kuwa Kigango.
Naye Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Gaudence – Makoka, Padri Amaladoss Chinnappan aliwaasa Waamini waliotoka katika Parokia ya Makoka na kujumuika katika Parokia ya Segerea, kupitia Kigango hicho, wasichukie wala kusikitika, bali wafurahi kwa sababu wote ni Waamini Wakatoliki.
Padri Chinnappan alimshukuru Askofu kwa kuwaweka pamoja, kuwapatanisha na kuwapatia Kigango ambacho amekizindua, akiwasihi Waamini kufahamu kwamba huo ndio Ukristo wanaotakiwa kuuishi katika maisha yao ya kila siku.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu amewataka Waamini kutokubali kuyumbishwa kiimani.
Askofu Mchamungu alitoa wito huo hivi karibuni katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara iliyofanyika Parokia ya Mtakatifu Cesilia -Kisarawe ll, Kigamboni.
Askofu Mchamungu alisema waamini wanatakiwa kuitangaza Injili kwa watu wote ili wamjue Mungu wa kweli.
“Ndugu zangu, tushike Maandiko Matakatifu… hayo ndio yatatusaidia kuona utukufu wa Mungu,”alisema Askofu Mchamungu.
Kwa upande wa Waimarishwa wa sakramenti hiyo, aliwataka kutambua majukumu yao sis i kuwasimamia watoto hao, bali hata kuwasaidia na kuwaongoza katika misingi thabiti ya kimaadili.
Askofu Mchamungu aliwataka waamini wa parokia hiyo wajenge Kanisa kwa sababu kanisa la sasa ni dogo.
Naye Paroko wa parokia hiyo,Padri Roger Kamuzinzi, aliwaomba waamini kumpa ushirikiano ili aweze kutekeeleza vyema majukumu yake ya kitume.
Padri Kamuzinzi alimshukuru Askofu Mchamungu kwa kuwapatia vijana 31 Sakramenti ya kipaimara.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Parokia hiyo, Geofrey Lyungu alisema parokia hiyo bado changa kwani ina muda wa miezi sita tu tangu ilipotangazwa na Askofu Mkuu Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, kuwa Parokia Kamili.

MOROGORO

Na Mwandishi wetu

Katibu wa Askofu wa Jimbo Katoliki la Morogoro, Padri Boniface Mliga amewataka Watawa wa Kike wa Shirika la Maria Imakulata (SMI), walioweka Nadhiri za Daima kuona fahari kwa kutoa maisha yao kama Sadaka ili kumtumikia Mungu.
Padri Mliga alisema hayo hivi karibuni wakati wa Adhimishi la Misa Takatifu ya Nadhiri za Daima kwa Masista wa Shirika la Maria Imakulata –SMI, iliyofanyika katika Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli –Kihonda, jimboni Morogoro.
“Ndugu zangu, inawapasa kutambua Agano ni makubaliano, kwani hata Wana Waisraeli waliweka Agano na Mungu, nanyi mnaweka Agano kati ya Mungu na Kanisa, la kumtumikia kama kiumbe chake mwenyewe, huku mkitoa maisha yenu kama zawadi na sadaka kwake,”alisema Padri Mliga.
Aidha, aliwataka Masista hao kutenda mema na kumtumikia Kristo siku zote za misha yao, akiwakumbusha kuwa kila mtu anayehitaji kumfuata Yesu, lazima aikane nafsi yake kwa kuachana na mambo ya kidunia, na kumfuata.
Padri Mliga aliendelea kusema, “Ukiikana nafsi yako, pia unatakiwa ubebe msalaba wako.”
Aliendelea kusema  kwamba kama mtu amechagua kumfuata Kristo na kukubali, yampasa kujiuliza, je, ana uwezo huo wa kuacha  mambo yote?
“Kwani wasije kukubali kuacha ya ulimwengu, na baadaye wakashindwa na wakakata tamaa, kwani maisha ya kumfata Kristo, si maisha ya kimasihara,”alisema Padri Mliga.
Kwa mujibu wa Padri Mliga, Kristo alichekwa na kudhihakiwa na baadhi ya watu, lakini hakukata tamaa na badala yake, aliendeleza kazi yake ya kuhubiri Injili kwa mataifa, na mwishowe aliteswa na kukubali kufa msalabani, ili atimize agano lililoandikwa hapo kale.
Alitoa wito kwa Masista wamkimbilie Mungu siku zote za maisha yao, kwa kupokea msalaba na kuubeba kwa furaha na si kwa huzuni, ili waweze kukidhi vigezo vya kuwa wafuasi wa Kristo.
Mbali na hayo, Padri Mliga aliwataka watawa hao wasitazame walipotoka wala kukata tamaa, bali watazame Msalaba wa Kristo kwa imani na matumaini makubwa, kwa kujitoa zaidi, wakiomba Mungu waendelee kuubeba Msalaba wa Kristo, kwa amani na upendo.

KARONGA, Malawi
Chama cha Wanawake Wakatoliki (Catholic Women Association: CWA) nchini Malawi, kimefanya Mkutano Mkuu wa 45 wa Mwaka kuanzia Desemba 18–22 mwaka huu.
Mkutano huo ulifanyika katika Misheni ya Chaminade, Jimbo Katoliki la Karonga chini ya kauli mbiu isemayo: “Kukuza Uzazi, Njia ya Furaha ya Furaha na Utakatifu.”
Akizungumza, Mwenyekiti wa CWA Taifa, Doreen Banda Zimba alisema kuwa maandalizi yalikuwa yakiendelea vizuri, akitolea mfano shughuli za kamati ndogo.
“Kila kamati, ikiwa ni pamoja na zile za itifaki, liturujia, malazi, afya, na usafi wa mazingira, miongoni mwa zingine, ziko chini kuhakikisha kwamba kila kitu kinawekwa kabla ya muda uliopangwa,” alisema.
Aliongeza kuwa wanawake kutoka kila Jimbo walijitolea kufanya maandalizi ya usafiri wa kuwapeleka kwenye eneo la mkutano.
Mazungumzo mengine yalihusu mada, kama vile asili na madhumuni ya ndoa na familia, Kanuni Nne za Mafundisho Jamii ya Kanisa, Kiroho cha CWA, na Uongozi Kanisani, na Maoni ya Kitamaduni na Kisheria kuhusu Utoaji Mimba na Muungano wa Jinsia Moja, miongoni mwa mambo mengine.
Mawasilisho hayo yaliwezeshwa na Maaskofu, Mapadre na Walei, ambapo Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Malawi, Mhashamu Askofu Mkuu George Desmond Tambala, aliongoza liturujia ya ufunguzi katika Mkutano huo.

KASESE, Uganda

Padri Raphael Balinandi Kambale ameadhimisha Jubilei ya Dhahabu katika Parokia ya Nsenyi, Jimbo Katoliki la Kasese nchini Uganda, akiwasihi Mapadri vijana na Wakristo kwa ujumla, kujenga upendo kwa Kanisa, na kujitolea kwa ajili ya Miito.
Padri Balinandi, ambaye kwa sasa ni Padri mzee zaidi katika Jimbo Katoliki la Kasese, alipewa Daraja Takatifu la Upadri, Desemba 14 mwaka 1974 katika Parokia ya Nsenyi na Askofu Vincent J. McCauley, mbele ya Askofu Sarapio Magambo na Askofu Kathaliko Emmanuel, kutoka Jimbo Katoliki la Butembo-Beni.
Yeye alikuwa Padri wa tatu kutoka Jimbo Katoliki la Kasese, akifuatiwa na Monsinyori Augustine Muhindo Hayati, aliyepewa Daraja la Upadri wa kwanza mwaka 1958 na Padri Louis Isingoma Byakuyamba mwaka 1972.
Katika hotuba yake muda mfupi baada ya Misa iliyoongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki la Kasese, Mhashamu Francis Aquirinus Kibira Kambale, Padri Balinandi alitajwa kuwa mtu wa thamani katika Jimbo na Wilaya kwa ujumla, ambaye amechangia maendeleo ya kiroho, kitamaduni na mazingira.
Askofu Francis Kibira alisema kuwa Ndoa Takatifu inachukuliwa kuwa ni Sakramenti yenye nguvu katika Kanisa Katoliki ambayo wanandoa wanapaswa kuilinda kwa wivu kwa sababu ni mfugaji wa Sakramenti nyingine.
Vile vile, Askofu Kibira ambaye alitoa wito wa mafunzo ya Katekesi miongoni mwa watoto, alisema kwamba ili Kanisa liwe na Mapadri wazuri na wanandoa miongoni mwa Miito mingine kanisani, wazazi wanatakiwa kuwa na sababu na kuweka thamani katika ndoa ili kuwalea watumishi makini wa Kanisa na Jumuiya.
Katika ujumbe wake, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Gulu, Mhashamu John Baptist Odama, mwanafunzi mwenza wa Padri Balinandi, alirejea maelezo ya watu wengine kuhusu Padri, kwamba yeye ni mtu mwenye imani kubwa kuhusu maisha kama Kasisi.
Mbali na hilo, aliendelea kwa kusema, “Nina kumbukumbu zake za kuwa na shauku kubwa ya liturujia, na kutamani sana kufuata kanuni za kiliturujia na Neno la Mungu.”
Askofu Mstaafu wa Jimbo Katoliki la Kasese, Mhashamu Egidio Nkaijanabwo alisema kuwa Padri Balinandi alikuwa mtu wa mila nzuri, na alipenda utamaduni wake.
Kupitia utamaduni wake, kujifundisha, na kupitia elimu yake zaidi, Padri Balinandi ameonekana kuwa na ujuzi katika lugha ya Lhukonzo.
Miongoni mwa umahiri mwingine, alitafsiri vitabu vingi vya kiliturujia katika lugha ya kienyeji, zaidi ya yote aliyoheshimu Ufalme wake.
Katika mahubiri yake, Padri Expedito Masereka, Msimamizi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Bukangara, aliwataka Wakristo kujifunza kutoka kwa Padri Balinandi kujiendeleza kiujumla kwa kuanza na wao wenyewe.
Mratibu huyo wa zamani wa Kichungaji, alimpongeza mshereheshaji huyo kwa michango yake ya umoja, na kukuza lugha ya Lhukonzo, kazi inayowalazimu Wakristo katika Miito mingine kutimiza wajibu wao kwa umakini na matumaini, kama inavyotarajiwa hadi mwisho.
Mjubilei huyo, Padri Balinandi Kambale akiwa na furaha tele, alimpongeza Askofu Kibira kwa upendo na matunzo katika uzee wake, akisema kuwa aligubikwa na upendo, ukarimu na uangalizi alioonyeshwa na Wakristo, na watu wema.
Naye Mkuu wa Walei wa Jimbo Katoliki la Kasese, George Mayinja, aliwataka wazazi kuwalea watoto wao kulingana na huduma ya Kanisa, lakini pia kuwekeza katika Elimu yao.