Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Waamini wa Parokia ya Mtakatifu Yohane Maria Muzeey – Tegeta ‘A’, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wameadhimisha siku ya Somo wa Parokia hiyo, huku wakitakiwa kupendana katika kila hali walizo nazo, kwani hakuna aliyeumbwa kuwa mtumwa kwa wengine.
Hayo yalisemwa na Padri Prosper Kessy, Gombera wa Kituo cha Hija cha Mtakatifu Padri Pio, San Damiano – Msimbazi, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Somo wa Parokia ya Mtakatifu Yohane Maria Muzeey – Tegeta ‘A’, jimboni humo.
“Kwa hiyo ndugu, tupendane katika hali zozote tulizo nazo, kwa sababu hakuna aliyeumbwa kwa ajili ya kuwa mtumwa kwa watu wengine, yaani hata ukijiona una pesa kiasi kwamba ukaamua kutafuta wafanyakazi wa nyumbani kwako, lakini tambua kwamba wale hawakuumbwa kwa ajili ya kuja kuwa watumwa wako,” alisema Padri Kessy.
Aidha, Padri huyo aliwasihi Waamini kufahamu kwamba Neno la Mungu ni tofauti na maneno mengine, kwani Neno hilo huwabadilisha hata majambazi na kuamua kuishi maisha yanayofaa katika jamii.
Padri huyo aliwasisitiza Wakristu kuliruhusu Neno la Mungu lifanye kazi katika maisha yao ili liwabadilishe, na kuwa watu wema.
Alitoa wito kwa Waamini kuliruhusu Neno hilo lifanye kazi katika biashara zao, akiwataka kuepuka udanganyifu katika biashara hizo, ikiwemo kujipangia viwango vya bei za bidhaa, tofauti na bei halali za bidhaa hizo.
“Liruhusuni Neno la Mungu liingie katika biashara zenu, ili liwasaidie kuwa waaminifu. Wapo wafanyabiashara ambao ukifika wanakudanganya kwamba ‘nguo hii imetokea Uturuki,’ ili akuuzie kwa bei ya juu zaidi, huku ukiamini kwamba kwa sababu imetoka Uturuki, basi itakuwa ni nzuri na imara zaidi…
“Yaani mtu anaamua kuuza bidhaa kwa bei mara tatu zaidi ya aliyonunulia, huo ni udanganyifu wa juu sana katika biashara. Halafu baadaye anatoka mbele za watu anasema, ‘Mungu amenitendea mambo makuu sana katika biashara yangu,’ huyo aliyekutendea siyo Mungu, bali ni shetani kupitia udanganyifu wako,” alisema Padri Kessy.
Padri Kessy alitoa wito kwa wazazi kuwapa watoto wao malezi yaliyo bora, na si ya kuwanyenyekea, kwani wakiwadekeza kupitiliza, watawatengenezea mazingira magumu pale watakapokuwa wakubwa.
Aidha, aliwashukuru Waamini wa Tegeta ‘A’ kwa kumwalika kusali naye katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu ya Somo wa Parokia, akiwaasa kuendelea kushikamana na kuwa wamoja ili waweze kupiga hatua kimaendeleo parokiani hapo.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Urbanus Riziki alimshukuru Padri Kessy kwa kukubali mwaliko wa kwenda kuungana na Waamini wa Tegeta ‘A’, akimshukuru pia kwa kuongoza Misa hiyo Takatifu.
Padri Riziki aliwaasa Waamini parokiani hapo kuongeza nguvu katika kuchangia ujenzi wa kanisa jipya linaloendelea kujengwa, ili waweze kuukamilisha kwa haraka ujenzi huo.
Kwa mujibu wa Katibu wa Parokia hiyo, Prisila Clemence, Parokia ya Mtakatifu Yohane Maria Muzeey - Tegeta ‘A’ ilianzishwa kama Kigango cha Mtakatifu Yohane Maria Muzeey, Julai 6 mwaka 2007.
Kigango hicho kilianzishwa kutoka Parokia ya Bikira Maria Mama wa Huruma - Mbezi Beach (BMMH) iliyokuwa chini ya Paroko wa Mbezi Beach wa wakati huo, Padri Romuald Mukandara.
Baadaye Kigango hicho kilihamishiwa Parokia ya Bikira Maria Consolatha – Makabe, chini ya Mapadri wa Missionaries of Mary Immaculate (MMI), baadaye tena kikahamishwa na kuwa chini ya Parokia ya Benedicta wa Msalaba – Msumi.
Julai 7 mwaka 2018, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam kwa wakati huo,  alikipandisha hadhi kuwa  Parokia Teule.
Julai 7 mwaka 2020, Mtakatifu Yohane Maria Muzeey - Tegeta ‘A’  ilitangazwa rasmi kuwa Parokia Kamili na Askofu Mkuu wa Jimbo hilo, Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, na kuwekwa chini ya Mapadri wa Jimbo hilo, ambapo Padri Urbanus Riziki Ngowi alitangazwa kuwa Paroko wa Parokia hiyo.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Baba Mtakatifu Fransisko ameridhia ombi la kung’atuka kutoka shughuli za kichungaji za Jimbo Katoliki la Iringa, lililowasilishwa na Askofu wa Jimbo  hilo, Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa, akimteua Padri Romanus Elamu Mihali kuwa Askofu mpya wa jimbo hilo.
Askofu Mteule Mihali ameteuliwa baada ya Askofu Ngalalekumtwa aliyekuwa akiongoza jimbo hilo, kufikisha umri wa kustaafu.
Kabla ya uteuzi huo, Askofu mteule Mihali alikuwa Makamu wa Askofu wa Jimbo Katoliki la Mafinga, na Paroko wa Parokia ya Ujewa, jimboni humo.
Askofu Mteule Mihali alizaliwa Juni 10, mwaka 1969 katika Kijiji cha  Itulituli, Wilaya ya Mufindi, Mkoa wa Iringa.
Baada ya majiundo yake ya Falasafa na Taalimungu katika Seminari Kuu ya Songea, alipewa Daraja  Takatifu la  Upadri Julai 13 mwaka 2000 kwa ajili ya Jimbo la Iringa.
Askofu Mteule Mihali katika utume wake, alishika nyadhifa mbalimbali na kuendelea na masomo zaidi, ambapo mwaka 2000 hadi 2003, alikuwa Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu Paulo Mtume huko Ilula, jimboni Iringa.
Mwaka 2003 hadi mwaka 2005 alikuwa Mlezi na Mkufunzi wa Seminari Ndogo ya Mtakatifu Kizito, Jimbo Katoliki la Mafinga.
Aidha, mwaka 2005, hadi 2011, aliendelea na masomo yake ya Uzamili wa Sayansi katika Sayansi ya fani ya wanyama, na kupata  Shahada yake  katika Chuo Kikuu cha Kerala nchini India.
Mwaka 2012 hadi 2015 alifanya utume kama Paroko Msaidizi wa Parokia ya Bikira Maria wa Fatima huko Usomaki, jimboni Iringa.
Mwaka 2015 hadi 2024, alikuwa akifanya utume kama Paroko wa Parokia ya Bikira Maria Mpalizwa, Ujewa,  Iringa.
Baada ya kuundwa kwa Jimbo Katoliki la Mafinga  mwaka  2024, na  kupatikana Askofu mpya wa Jimbo hilo, Padri Romanus aliteuliwa kuwa Makamu Askofu wa Jimbo hilo, na Paroko wa Parokia ya  Bikira Maria Mpalizwa (Mafinga), hadi uteuzi wake.
Askofu Mstaafu Tarcisius Ngalalekumtwa ataendelea kuwa Msimamizi wa Kitume wa Jimbo Katoliki la Iringa hadi Askofu   Mteule Mihali atakapowekwa wakfu wa Kiaskofu kwa ajili ya Jimbo hilo hilo.

DAR ES SALAAM

Na Celina Matuja

Madaktari na Wauguzi Wakatoliki nchini wametakiwa kuzingatia mambo muhimu ili waweze kutoa huduma kadri ya mwelekeo wa Bwana Yesu Kristo.
Madaktari na wauguzi hao wameaswa pia kutumia muda wao kusali ili  kuomba mwongozo wa Mungu katika huduma zao kwa wagonjwa.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katopliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu ametoa maagizo hayo katika salamu kwenye Semina ya Madaktari na Wauguzi Wakatoliki, iliyoandaliwa na Jimbo hilo, iliyofanyika katika Parokia ya Kristo Mfalme, Tabata.
Semina hiyo ilikwenda sanjari na Adhimisho la Misa Takatifu, ambapo katika homilia yake aliwataka madaktari hao, kufuata mfano wa Mtakatifu Paulo aliyewaua na kuwatesa Wakristo, lakini aliongoka, hivyo wao nao wahakikishe wanaleta uponyaji kwa wagonjwa  na kuihubiri Injili.
“Kutokana na Ufunuo wa Kristo mwenyewe, Mtakatrifu Paulo alifanya kazi kubwa na nyingi kufundisha habari njema za Yesu Kristo, baada ya kuongoka. Sisi pia tuongoke kama Paulo, hivyo nawapatia ‘take home’ ili mpate kuzingatia katika kazi yenu,” alisema Askofu Mchamungu.
Askofu awapa Madaktari ‘vitendea kazi’:
Moja ya mambo ambayo walitakiwa kuzingatia wanataaluma hao ni kusali na kuomba maongozi ya Mungu, kwa sababu kazi yao inagusa moja kwa moja uumbaji na uhai.
Kuwahi kazini na kuwajibika kwa wagonjwa kwa moyo wa upendo na furaha, kuwasikiliza wagonjwa kwa umakini ili kuelewa shida zao kiafya ili kutoa matibabu sahihi.
Kuepuka uzembe kazini na kuwa makini, kwa kufanya kazi kwa kujiamini ili kumpa mgonjwa tumaini la kupona ama kupata ahueni, kupenda kazi na kuitenda kwa furaha kwa kuwa ni wito wao.
Kutoa huduma bila kudai chochote kwa mgonjwa, na kutumia lugha nzuri, ikiwemo kutunza siri za mgonjwa.
Kutokuwa na mahusiano ya kimapenzi na wagonjwa wao,  kuwahudumia kwa karibu wagonjwa wanaohitaji uangalizi makini, kama wanaoongezewa damu, maji mwilini, na hasa nyakati za usiku.
Aidha, Askofu Mchamungu aliwataka kusoma na kujiendeleza zaidi ili kuwa na ujuzi mkubwa kwa kusoma vitabu mbalimbili vinavyohusu taaluma yao.
Padri Mosha: Fanyeni kazi bila kinyongo:
Kwa upande wake, Padri Dakta Joseph Mosha, Paroko wa Parokia ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alikemea baadhi ya tabia za Wauguzi na Madaktari kutotoa huduma kwa moyo na ari kwa wagonjwa.
Aliwataka kutambua kwamba wao ni washirikishwa wa kazi ya utendaji wa Mwanadamu kutoka kwa Mungu, na kutokuondoa nafasi ya Mungu katika maisha ya Mwanadamu.
Padri Mosha alisema kuwa Maandiko, kitabu cha mwanzo 1:26 akinaeleza kwamba “Sisi Binadamu tumeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu,”, akiwataka Wanataaluma hao kutambua kwamba kila wanapomwona mgonjwa, watambue kuwa ni sura na mfano wa Mungu.
Alisema kwamba maisha huanza kwenye familia, hivyo hawana budi kutenda kwa misingi ya Mwenyezi Mungu pasipo kufuata ile siasa ya uhuru wa kufanya lolote, ambao una upotofu.
Padri Kessy: Tendeni kazi kwa upendo:
Naye Padri Prosper Kessy Gombera wa Kituo cha Hija cha San Damiano Msimbazi, aliwakumbusha  Madaktari na Wauguzi hao, kutenda kazi zao kuzingatia huruma na upendo.
Aidha, aliongeza kuwa itamsaidia sana mgonjwa iwapo atapokea huruma na upendo, bila kusahau kumhudumia kwa hadhi njema, na hisia ya utu.
Kwamba kuna baadhi ya watu wamepoteza hisia, wanaona kila jambo ni sawa, wamezoea kifo, hata wakimwona mgonjwa yu mahututi wanaona kama ni mfu, wasikubali iwatawale, kwani Mungu amempa kila mtu hisia na huruma.
Jambo lingine la kuzingatia ni kuigeuza kazi kuwa sala,kwa maana ya kusali kabla ya kuwahudumia wagonjwa na kuifanya kazi hiyo kwa  umakini, ndipo inapogeuka kuwa injili na sala.
Aliwataka pia kuvumilia kutokana na matukano mbali mbali, ila kusimama na msimamo wa kuutafuta utakatifu na uaminifu kwa kuheshimu uhai mwanzo mpaka mwisho, kwa kukemea maovu mamlaka waliyopewa wasikubali kushiriki katika  dhambi.
Akinukuu Maandiko Matakatifu Matayo 28:16 – 20: Nimepewa mamlaka yote Duniani na Mbinguni enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi mkiwabatiza kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu.

VATICAN CITY, Vatican

Baba Mtakatifu Fransisko amekutana na Maaskofu, Marais wa Tume za Mawasiliano za Mabaraza ya Maaskofu na Wakurugenzi wa Ofisi za Mawasiliano za Mabaraza ya Maaskofu.
Katika hotuba yake Baba Mtakatifu aliwashukuru kwa kushiriki nao, akiwakaribisha wote ambao katika Makanisa mahalia wanafanya huduma ya kuwajibika katika nyanja ya mawasiliano.
“Inapendeza kuwaona hapa, Maaskofu, Mapadri, Watawa wa kike na kiume na walei, walioitwa kuwasilisha maisha ya Kanisa na mtazamo wa Kikristo wa ulimwengu. Kuwasiliana na maono haya ya Kikristo ni kuzuri,” alisema Papa Fransisko.
Aidha, Papa aliongeza kwa kusema, “Tunakutana leo, baada ya kuadhimisha Jubilei ya Ulimwengu wa Mawasiliano, kufanya mapitio na pia uchunguzi wa dhamiri pamoja. Hebu tutulie ili kutafakari zaidi juu ya njia halisi tunayowasiliana nayo, inayohuishwa na imani ambayo, kama ilivyoandikwa katika Waraka kwa Waebrania, ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo na bayana ya mambo yasiyoonekana…
Baba Mtakatifu Fransisko alifafanua kuwa hiyo ambayo kwao ni huduma ya kitaasisi, pia ni wito wa kila Mkristo, wa kila mtu aliyebatizwa, na kwamba kila Mkristo anaitwa kuona na kusimulia historia za mema ambayo uandishi wa habari mbaya hujaribu kufuta, na kutoa nafasi ya uovu tu.
Alibainisha pia kwamba uovu upo, hivyo haupaswi kufichwa, lakini lazima ukoroge, uzae maswali na majibu, na kusema kwamba kwa sababu hiyo,  kazi yao ni kubwa na inawahitaji wajitoe wenyewe kufanya kazi ya pamoja ili ya kuwashirikisha kila mtu, kuwathamini wazee, vijana, wanawake na wanaume kwa kila lugha, kwa maneno, sanaa, muziki, uchoraji, na picha.
Aliwataka Waamini kufahamu kwamba wote wameitwa ili kuthibitisha jinsi gani wanawasiliana naye, hivyo wanahitaji kuwasiliana kwa kila linalotokea.
Alisisitiza kuwa changamoto ni kubwa, huku akihimiza kuimarisha harambee kati yao, katika ngazi ya bara na ya ulimwengu mzima ili kujenga mtindo tofauti wa mawasiliano, tofauti katika roho, katika ubunifu, katika nguvu ya kishairi inayotoka katika Injili na isiyokwisha.
Aidha, Baba Mtakatifu alikiri jambo moja kwao kuwa anajali zaidi akili ya asili kuliko akili mnemba, akisema kuwa akili ya asili ndiyo ambayo wanapaswa tuikuze, na kwamba wanapohisi kuwa wameanguka kwenye shimo, watazame zaidi ndani yao wenyewe.

VATICAN CITY, Vatican

Baba Mtakatifu Fransisko amewataka Waamini kuwahubiria maskini Habari Njema, kuwatangazia wafungwa uhuru wao.
Aliyasema hayo katika Adhimisho la Misa Takatifu katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, katika Dominika ya Januari 26 mwaka huu wa 2025, ambapo ni katika muktadha wa Maadhimisho ya Dominika ya VI ya Neno la Mungu iliyoanzishwa na Papa mwenyewe mwaka 2019.
Aidha, katika fursa hiyo, ilitolewa pia Huduma ya Usomaji wa Neno la Mungu kwa waamini 40 kutoka mataifa mbalimbali duniani, ambayo pia ilikuwa ni Adhimisho la Misa Takatifu ya Kufunga Jubilei ya Ulimwengu wa Mawasiliano, iliyoanza tangu Januari 24 kwa ufunguzi wa Misa.
Katika homilia yake Baba Mtatifu Fransisko alisema kuwa Injili waliyoisikia katika Adhimisho hilo inatangaza utimilifu wa unabii unaofurika katika Roho Mtakatifu, na yule anayeitimiza ni Yeye ajaye kwa nguvu za Roho.
“Neno la Mungu liko hai, linatembea nasi kwa karne nyingi, na kupitia nguvu za Roho Mtakatifu linafanya kazi katika historia. Bwana kiukweli siku zote ni mwaminifu kwa ahadi yake, ambayo huiweka kwa sababu ya upendo kwa wanadamu. Hivi ndivyo alisema Yesu katika sinagogi la Nazareti. Leo Maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” alisema Baba Mtakatifu.
Baba Mtakatifu alisema kuwa ni bahati iliyoje yenye furaha katika Dominika ya Neno la Mungu, ambapo bado wakiwa mwanzoni mwa Jubilei, ukurasa huo wa Injili ya Luka unatangazwa, ambamo Yesu anajidhihirisha kuwa Masiha aliyewekwa wakfu kwa kupakwa mafuta na kutumwa kutangaza mwaka kwa neema ya Bwana.
Papa alisema kuwa katika Dominika hiyo iliyowekwa maalum kwa ajili ya Neno la Mungu, ni wajibu wa kila mmoja kumshukuru Mungu kwa kuwa amewaelekezea Neno lake lililomfanya mtu kwa wokovu wa ulimwengu.
Aliongeza pia kuwa hilo ndilo tukio ambalo Maandiko yote yanazungumza juu yake, ambayo yana watunzi wao wa kweli, yaani watu na Roho Mtakatifu, na kwamba Biblia nzima inamkumbuka Kristo na kazi yake, na Roho hufanya uwepo katika maisha yao na katika historia.
“Tunaposoma Maandiko, tunapoomba na kuyasoma, hatupokei  habari kuhusu Mungu tu, bali tunamkaribisha Roho ambaye hutukumbusha yote ambayo Yesu alisema na kutenda (Taz Yh 14:26). Hivyo mioyo yetu, ikiwa imewashwa na imani, inangojea kwa matumaini ujio wa Mungu,” Papa alisema.
Aliongeza kuwa kila mwamini lazima awe na mazoea zaidi ya kusoma Maandiko, na kwamba katika hilo, alipendekeza tena kuwa kila mtu awe na Injili ndogo mfukoni ya Agano Jipya, na kubeba katika mfuko, na wakati wa mchana kuisoma.

MOROGORO

Na Angela Kibwana

Mpendwa msomaji, katika mfululizo wa makala haya ya “Wajibu wa Kanisa kwa Watu Wenye Ulemavu katika Huduma za Kiroho,” Makala yaliyopita yalianza na kuonesha kwamba Kanisa kama Jumuiya ya Waamini wanaomwamini Kristo, msingi wake ni Kristo mwenyewe ((Waefeso 5: 29; Wakolosai, 1: 24 na Wakolosai 2:10).
Katika kulithibitisha hilo, makala hayo yalionesha namna Yesu Kristo mwenyewe alivyokasimisha majukumu yake  ya  kulihudumia Kanisa  la hapa duniani  kupitia Mtume Petro, na msingi huo huo ndiyo asili ya uwepo wa  Kanisa Katoliki ((Mathayo, 16:18).
Makala hayo yalisisitiza kwa kuwa Yesu Kristo ndiye msingi wa Kanisa, Kanisa la duniani halina budi kuyaishi maneno, matendo pamoja na kuubeba wajibu ambao Yesu Kristo aliukasimisha kwa Kanisa la hapa duniani, kama ilivyothibitishwa kupitia Biblia Takatifu na mafundisho ya mama Kanisa.
Makala hayo pia yalisisitiza kuwa Kanisa kama Jumuiya ya Waamini wanaomwamini Kristo, Waamini wake wanayo mahitaji tofauti, ambayo ndio msingi wa ustawi wao, kiroho na kimwili.
Makala hayo yakaangazia ni kwa namna gani Kanisa la hapa duniani linaweza au linayatafsiri mahitaji hayo katika utekelezaji wa majukumu yake kiroho na kimwili, pasipo kumwacha Waamini yeyote ambaye ni mwili na Kielelezo cha Kristo nje ya huduma hizo. “Waamini wenye ulemavu na mahitaji yao ya kiroho, ndio ukawa msingi wa makala hayo.”
Katika makala ya toleo hili, tunaendelea kuangazia hali ya upatikanaji wa huduma za kiroho ndani ya Kanisa Katoliki kwa watu wenye ulemavu, pasipo kuyatenga makundi mengine ya watu wenye ulemavu. Makala haya yatajikita kwa undani zaidi kwenye vikwazo vya mawasiliano kwa kundi la watu wenye ulemavu wa kuongea na kusikia, ili kuweka usawa wa kihuduma kiroho, kiafya,kijamii na kimtazamo pia.
Kutokana na takwimu za matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 nchini Tanzania, kati ya watu wote wenye ulemavu, ulemavu wa kuona,kusikia, kuongea na kutembea ni 6.5% ya Watanzania wote, ambayo ni sawa na jumla ya watu 3,154,514kuanzia umri wa miaka saba (7)na kuendelea pasipo kujali dhehebu au dini ya mhusika, kwa hiyo kutokana na hali zao watu hawa wanahitaji mipango na mikakati maalum ya kuwafikia kwa huduma za kimwili, kijamii, kiafya, kielimu na kiroho pia.
Mpendwa msomaji wa makala haya katika kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma za kiroho leo hii nitaangazia wajibu huo kuanzia katika msingi wa familia na  jumuiya ndogondogo za Kikristu.
Kanisa Katoliki linajengwa kuanzia ngazi ya familia halafu jumuiya  ndogondogo za Kikristu ukiwa ni mwito wa kuwakaribisha watu wote  katika jamii ya waamini wanao mwamini Kristo kuwa Kristo ndiyo  kichwa na mwili wa kanisa
Katika waraka wa Mtakatifu Paulo kwa Wakorintho, tunakumbushwa kuwa mwili wa Kristo una viungo vingi, na kila kimoja kina thamani na nafasi yake (1 Kor. 12:12-27).
Hili ni somo muhimu linalotufundisha kuwa hakuna anayepaswa kuachwa nyuma katika mpango wa wokovu, ikiwa ni pamoja na watu wenye ulemavu kwa ujumla.
Huduma za kiroho kwa watu wenye ulemavu wa kusikia ni mwaliko wa dhati wa kuhakikisha kwamba kundi hili linaloshiriki kikamilifu katika maisha ya kiroho ya jumuiya, ikiwa ni haki yao ya kimsingi kama waamini na wana wa Mungu, ambao walibatizwa na kuwa sehemu ya familia ya Kanisa.
Kwa msingi huu, huduma hizi zinapaswa kuwekwa kama kipaumbele katika jitihada za Kanisa za kujenga jumuiya ndogondogo zinazojumuisha watu wote kuanzia ngazi ya familia bila ubaguzi unaotokana na hali zao.
Jumuiya za Kikristo, hasa ndani ya mazingira ya Parokia, zina jukumu la kutambua kuwa ulemavu wa kusikia,kutembea, kuongea au kuona, siyo kikwazo kwa imani, badala yake, ni fursa ya kuthibitisha wito wa Kanisa wa kuwa sauti ya matumaini na mshikamano kwa kundi hilo.
Maandiko Mtakatifu, mfano Warumi, 15:1, inaonesha jinsi ambavyo wana Kanisa wanavyoitwa kuwa na moyo wa huduma na kusaidia wale walio na udhaifu wa aina yoyote, ikiwemo ulemavu.”Basi imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wa wanyonge, wala si kujipendeza wenyewe.”
Kanisa Katoliki linapofanya sensa kujua idadi ya waamini wake, kadhalika sensa hiyo inapaswa kuwajumuisha watu wenye ulemavu ili kujua idadi yao, taarifa na mahitaji yao ili yatafsiriwe katika huduma za kiroho na huduma nyingine.
Kadhalika, Kanisa lina wajibu wa kuandaa mwongozo kwa watu wenye ulemavu, ambao utaonesha namna ya kuwafikia kuanzia ngazi ya familia, jumuiya Ndogo Ndogo,Parokia na taasisi zake  kwa ujumla, ili waweze kupata huduma za kiroho, ikiwa ni pamoja na kuwalinda kwa sababu Kanisa nalo lina wajibu wa kulinda haki kwa maisha ya kila binadamu.

Mzungu hajakubali kuwa bin-Adam wote ni sawa, wala kwamba wote ni wa baba mmoja,  Adam.
Pamoja na kwamba alituletea Msahafu wa dini – Biblia wenye kusisitiza “upendo,” hiyo ni ghiliba tupu kwa sababu inawabagua wana-Adam kati ya walio wana wa Taifa teule la Mungu (Israeli), na wana wa Mataifa yasiyo teule. Huko ni kukweza ngozi nyeupe.
Kwa kutumia Mungu wa kujiundia (Yahweh) na Msahafu wa kibeberu, wanaidhinishwa kutugeuza watumwa wao, eti kwamba:
“Na wageni watakuwa watumwa wa kulisha mifugo yenu; na wana wa Mataifa watawalimia na kutunza mashamba ya mizabibu yenu”. Huo ndio ubaguzi wa ubeberu wa kimataifa ambao umedumu hadi leo.
Ubaguzi huo kwa misingi ya rangi ulioasisiwa, kusimikwa na kukomazwa Kimataifa na Mjerumani Johann Friedrich Blumenbach (1752 – 1840) unawagawa bin-Adam kwa viwango vya ubora katika makundi sita ya Watu weupe (Coucassians) kama daraja la kwanza; Wamongolia (Mongoloid) daraja la pili; Watu weusi (Ethiopoid); Wamarekani wenye asili ya Kihindi (Red Indians) na Wahimalaya (Malayans) kama daraja la mwisho kwa ubora.
Wamefika mbali kwa kudai kuwa Mwafrika si Mwana-Adam, yaani hakuzaliwa na Adam. Dhana hiyo mpya inayoitwa “Pre-Adamisma inadai kuwa Mwafrika alikuwepo kabla ya kuumbwa Adam na alikuwa kiumbe asiye na roho.
Mwasisi na Mwenezi wa dhana hiyo inayoshika kasi kipindi hiki cha utandawazi ni Mfaransa Isaac La Peyrere (1596 – 1676). Dhana hiyo inapinga usahihi wa Biblia juu ya uumbaji, ikidai kuwa kulikuwa na watu kabla ya kuumbwa kwa Adam na Hawa.
Anasema kwamba kulikuwa na uumbaji mbili za watu: uumbaji wa kwanza ulikuwa wa dunia nzima na Mwafrika kama mtu wa kwanza; na uumbaji wa pili ulihusu Wayahudi kama Taifa ambalo Adam alikuwa mkuu wake.
Anadai kuwa, Mataifa yote hayatokani na Nuhu, kwamba watu wa Mataifa (wasio wa Taifa teule) hawakutenda wala hawahusiki na dhambi ya asili kwa sababu walikuwepo kabla ya Adam, na hivyo hawakupokea “Sheria” au Maagizo ya Mungu, bali ni Adam na uzao wake pekee. Chini ya dhana hiyo Wazungu ni Wana-Adam, na Mwafrika siye.
Dhana hii ina watetezi wengi miongoni mwa Mataifa ya Ulaya: Mathew Fleming Stephenson, katika kitabu chake “Adamic Race” anasema, “Mungu alitumia mamilioni ya miaka kuumba mtu duni (Mwafrika) kabla ya kuumba mtu bora aina ya Mzungu (Caucasian) juu yake”. Wengine, kwa kutaja wanataaluma wachache tu, ni pamoja na John Harris (The Pre-Adamite Race), Isabelle Duncan (Adamites and Pre-Adamites), na wengine.
Iwe ni kwa mtizamo wa dhana ya “Pre-Adamite”, “Uumbaji” au “Mageuko” (evolution), hakuna ubishi mpaka sasa, kwamba binadamu (mtu) wa kwanza aliishi Loliondo/Ngorongoro zaidi kabla ya mwaka 10,000, Kabla ya Vizazi (KV) ambao ndio mwaka unaosemekana Adam aliumbwa.
Ustaarabu wa mtu huyu ulianza na shughuli za Kilimo, ufugaji, ibada na makazi eneo ambalo sasa linajulikana kama Nubia, au Sudan Kaskazini. Utawala wa kwanza ulianzia Ta-Seti eneo hilo; watu hawa walijulikana kama “Anu”.
Nchi waliyokalia ilijulikana kwa majina mengi, kama vile, Nubia, Kermet, Kush, Ethiopia au Egypt (Misri) na Mji Mkuu ulikuwa Kerma. Nubia imetajwa kwenye Biblia, Kitabu cha Mwanzo 2:11 kama nchi ya Havillah.
Ni Ufalme ulioundwa na watu weusi kutoka eneo la Maziwa Makuu (ANU) miaka ya 5900 Kabla ya Vizazi (KV) na maelfu ya miaka kabla ya Kristo (KK). Hapa ndipo Gharika (la Nuhu) lilipowakuta watu hawa, wakaangamia isipokuwa mtu mmoja – Nuhu na wanae watatu – Yafeti, Shem na Hamu. Hiyo ilikuwa Mwaka 5000 KK. SOMA ZAIDI KWA KUNUNUA TUMAINI LETU.

VATICAN

Na Angela Rwezaura

Kitabu hiki kinapatikana katika lugha ya Kijerumani, ambacho kinasimulia historia ya Ukristo katika dunia.
Kitabu hicho kimeeleza kwa kina kuhusu safari za Papa Fransisko alizotimiza nchini Iraq mwaka 2021, na kuhusu diplomasia ya Vatican katika nchini Iraq.
Matthias Kopp ni mwandishi na Mtaalimumgu ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Baraza la Maaskofu nchini Ujerumani.
Desemba mwaka 2024, Baba Mtakatifu Fransisko alimteua kuwa mshauri wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano.
Dibaji ya Papa Fransisko:
Kwa shukrani ya kumbukumbu ya ziara yangu ya kitume nchini Iraq, ambaye licha ya janga la Uviko 19, na mashaka ya usalama, nilitimiza ziara hiyo kunako Machi 2021 ili kueleza kwa Wakristo na watu wote wenye mapenzi mema katika Nchi hiyo, upendo wangu na mshikamano wangu.
Nchi hiyo inachukua nafasi daima na kila wakati katika moyo wangu katika sala.
Licha ya matatizo mengi ambayo Iraq inakabiliana nayo, ninatazama  Nchi hiyo kwa matumaini, kwa sababu inayo nguvu maalum.
Nguvu hiyo awali ya yote, ni watu hao hao  nchini Iraq, wale wote wanaoshiriki ujenzi wa jamii ya raia, ambao wanahamasisha demokrasia katika Nchi na ambao wanajibidiisha kwa ajili ya mazungumzo ya wazi na ya kweli kati ya dini.
Kwa njia hiyo, ziara yangu kwa Mkuu Ayatollah wa Najaf, Sayyid Ali Al-Sistani, ilikuwa muhimu na ya maana. Mkutano ule ulikuwa unataka kuwa alama kwa ulimwengu wote kwamba : kufanya vurugu katika jina la dini, ni matumizi mabaya ya dini.
Kama watu wa dini, tunawajibika kuelekeza amani, na lazima kuiishi, kufundisha na kuieneza amani hii.
Katika muktadha huo ninafikiri hata ziara yangu huko Ur, Kusini mwa Iraq, kwa maana kama wawakilishi wa dini mbali mbali, tulizungumza na kusali pamoja, chini ya maelfu na maelefu ya nyota zilizotazamwa na  baba yetu Ibrahimu alipoinua macho yake angani.
Urithi wa utajiri katika historia ya Bimillenaria del Cristianesimo kisayansi, karibu haijavumbuliwa.
Ninafikiri shule za kiteknolojia za Wakristo wa kwanza wa Mesopotamia, uwepo wa amani kwa mamia ya miaka kati ya Wakristo, na Waislamu kati ya Eufrate na Tigri, na tamaduni mbali mbali za ibada ya Kikatoliki katika kanda.
Aidha, mapambano kati ya Madhehebu ya Kikristo, katika nyakati za mateso mwanzoni mwa karne ya 20,  na visasi vingine vya kisiasa  na kwa mwendelezo wa uwepo wa Kikristo, hadi sasa.
Haya yote yanapendeza kwamba katika kazi ya Matthias Kopp, urithi huu na historia hiyo inakuja kuonesha katika muktadha wao mafunzo ya kidini, katika wingi na kwa kuzingatia fasihi nzito.
Mwandishi kwa namna ya pekee anaweka umakini katika jitihada za Kikanisa nchini Iraq na katika shughuli za Vatican,  kwa wawakilishi wake wa kidiplomasia, ambao wanamulika uhasishaji mwingi wa Mapapa kwa ajili ya Iraq na Wakristo wanaoishi ndani mwake.
Kwa njia hiyo, imezaliwa zawadi kama anavyoandika mwandishi mwenyewe, kwa Wakristo nchini Iraq, ambao ninawatia moyo kujihusisha kwa kina zaidi utajiri wao mkubwa wa kihistoria na kudumisha uhai wa urithi wao:
Kwa wakati ujao ambao hata leo hii unahatarishwa kwa sababu ya uhamiaji na ukosefu wa uhakika kisiasa.
Ninataka kueleza kwa kina na kuamini kwamba  haiwezekani kufikiria Iraq bila Wakristo, kwa sababu pamoja na Waamini wengine wote wanawakilisha kwa nguvu utambuzi maalum wa Nchi, ambao tangu karne za kwanza pamekuwa ni mahali pa kuishi, kuvumiliana na kukubaliana wao kwa wao.
Kwa hiyo, Iraq inaweza na kwa watu wake, kuonekana, katika Mashariki ya Kati na katika Ulimwengu kwamba inawezakana kuishi pamoja kwa amani, licha ya tofauti zao.

MOROGORO

Na Angela Kibwana

Katika nyumba moja huko Wilayani Kilosa Mkoani Morogoro, Lucy Patrick (siyo jina lake halisi), mfanyakazi wa majumbani, anajikuta akifanya kazi kwa saa 18 kila siku, bila kupumzika.
Hajawahi kulipwa mshahara wake wa miezi mitatu, sasa, ambapo malengo yake ya awali ilikuwa ni kujiongezea kipato kusaidia familia yake na mara nyingi anakula mabaki ya chakula cha familia.
Kwa muda mrefu, sauti yake haikusikika, lakini sasa, juhudi za Chama cha Wafanyakazi Wakatoliki (CWW) zimeanza kuleta matumaini kwake baada ya kutoa mafunzo ya kuboresha mahusiano kati ya waajiri na wafanyakazi.”
Wafanyakazi wa majumbani wanakabiliwa na changamoto nyingi, zikiwemo kutolipwa mishahara inayoendana na kazi zao, kunyimwa chakula, kupigwa, na kudhulumiwa haki zao za msingi.
Aidha, wengi wao hawana mikataba ya ajira, jambo linalowafanya kukosa ulinzi wa kisheria, hivyo wanajikuta wakifanya kazi kwa mazingira magumu bila msaada wowote wa kisheria au kijamii.
Victor Mackyao, mwanasheria na mwezeshaji wa mafunzo yaliyoandaliwa na (Chama cha Wafanyakazi Majumbani: CWM), anasema kuwa wafanyakazi wa majumbani, mara nyingi hawajui sheria za ajira, wala haki zao za msingi.
Wafanyakazi wa majumbani wengi wao ukiwauliza wanasema wanakumbana na vipigo, wananyanyapaliwa, wanatengwa,wanateswa maeneo wanayoishi siyo rafiki, wanakosa fursa ya matibabu wanapougua, wengine kukosa chombo maalum cha kuwasemea” alisema Mackyao.
Alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwaelimisha wafanyakazi hao wa majumbani ili kujua nini maana ya haki, lakini pia waajiri watambue wajibu wao ni upi kwa wafanyakazi hao ili kujenga usawa katika makundi yote mawili.
Alifafanua kuwa moja ya changamoto zinazochangia wafanyakazi hao wa majumbani kukosa hali zao msingi ni kutokana na vyombo au mamlaka mbalimbali ambazo zina dhamana ya kuwasimamia haki zao, kutowafikia kwa wakati kwa sababu wafanyakazi hao wanatoka kwa waajiri tofauti na maeneo tofauti.
Alisema kuwa tangu Cwm ilipoanza kutoa mafunzo hayo wamebaini kwamba baadhi ya wafanyakazi wa majumbani wanapohojiwa, ambao wanakaa kwao nje ya mwajiri wake, baada ya kuulizwa, wamedai kwamba wanalipwa kiasi cha shilingi elfu 30 au 50, wakati sheria inamtaka alipwe kuanzia 120,000/=.
“Wafanyakazi ambao wanakaa kwa waajiri wao sheria inawataka walipwe shilingi elfu 60, lakini hawalipwi kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo changamoto hizo ndizo zilizotufanya tuweze kupita na kutoa elimu kwa jamii lakini tutoe rai na tuviombe vyombo vyenye mamlaka ya kushughulikia masuala ya wafanyakazi wa majumbani, waweze kutumia mbinu kama tunazotumia sisi, ili waweze kuwafikia kujua changamoto zao na kazitatua wasikae tu mijini.”
Alisema kwamba kazi za majumbani si rahisi, na sheria inakataza ajira ya watoto katika kazi hizi kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009, Sura ya 13, Hata hivyo, bado kuna ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu,
Kwa kutambua changamoto hizi, CWM jimbo la Morogoro limeanza kutoa mafunzo kwa waajiri na wafanyakazi wa majumbani katika Dekania ya Kilosa.
Kwa mujibu wa CWM, kati ya wafanyakazi 161 waliopata mafunzo, asilimia 70 hawakuwa wanajua haki zao za msingi, na wala hawajui lolote kuhusu haki yao ya kuwa na mikataba ya kazi, ili kulinda haki zao.
Lengo ni kujenga mahusiano bora kati ya waajiri na wafanyakazi wa majumbani, kwa kuhakikisha haki na wajibu vinazingatiwa pande zote mbili.
Mratibu wa CWM, Edson Yeyeye, alisema kuwa mafunzo haya yalianza mwishoni mwa mwaka 2024 katika Dekania za Kihonda, Morogoro mjini, na sasa yamefikia Kilosa. Tayari wafanyakazi 161 na waajiri 62 wamepatiwa mafunzo hayo, huku Viongozi wa Dini na serikali 27 wakiungwa mkono katika juhudi hizi.
“Lengo letu ni kuhakikisha kila mfanyakazi wa majumbani anapata elimu ya haki zake na waajiri wanajua wajibu wao,” alisema Yeyeye.
Bahati Ramadhani, mmoja wa waajiri walioshiriki mafunzo hayo, alisema, “Ni muhimu elimu hii kufika vijijini kwa sababu huko ndiko wafanyakazi wengi wa majumbani wanatoka, Wengi wanapokuja mjini, wanakosa haki zao kwa sababu hawana mikataba wala hawajui sheria”.
Maria Chalalika, mshiriki mwingine, aliongeza kuwa kunahitajika kuundwa vyombo maalum vya kushughulikia haki za wafanyakazi wa majumbani, hasa kwa wale wanaopelekwa nje ya nchi, bila kujua wanachokwenda kukifanya
Kwa upande wake, Hosea Nikodemas Mgunda, Mwenyekiti wa Mtaa wa Mlimani Boma, aliwapongeza CWM kwa juhudi zao za kutoa elimu hiyo kwa jamii, ili haki za wafanyakazi wa nyumbani ziweze kulindwa na kuthaminiwa.
“Wafanyakazi wa majumbani wanapitia madhila mengi, hivyo tunahitaji kuwa na chama chao maalum ili kuwatetea na kuhakikisha wanapata haki zao.ili kupunguza vitendo vya ukatili miongoni mwao
Hata hivyo, Mgunda aliahidi kutumia mikutano yake ya kijamii kutoa elimu kuhusu haki za wafanyakazi wa majumbani ambavyo anatarajia kufanya kuanzia tarehe mosi Februari mwaka huu 2025.
Mafunzo haya yameongeza uelewa miongoni mwa wafanyakazi na waajiri, ambapo wengi wao sasa wanatambua umuhimu wa mikataba ya ajira, haki ya likizo, na mishahara inayotambulika kisheria.
Hata hivyo, changamoto bado zipo, hasa katika kuwafikia wafanyakazi walioko maeneo ya vijijini, na wale wanaofanyiwa ukatili wa kimya kimya.
Washiriki wa mafunzo hayo walipendekeza kuundwa kwa vyombo maalum vya kushughulikia haki za wafanyakazi wa majumbani, Kuongeza uhamasishaji kuhusu sheria za kazi vijijini na mijini, Kuwapatia wafanyakazi wa majumbani elimu ya malezi na maadili, kwani mara nyingi wao ndio walezi wa karibu wa watoto katika familia nyingi
Mratibu wa CWM, Edson Yeyeye, alisisitiza kuwa jitihada hizi zitaendelea hadi sauti za wafanyakazi wa majumbani zisikike na kuheshimiwa kikamilifu.
 “Ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha haki na heshima kwa kila mfanyakazi wa majumbani, kwani mchango wao katika familia na jamii hauwezi kupuuzwa,” alisema Yeyeye.
Sasa ni wakati wa jamii kushirikiana ili kuhakikisha kwamba kila mfanyakazi wa majumbani anapata heshima anayostahili, na mahusiano ya kazi yanajengwa kwa misingi ya haki na usawa.
Nashauri wafanyakazi wa majumbani wapewe elimu ya malezi na maadili mara kwa mara, kwa sababu katika nyumba nyingi za mijini na hata vijijini, sauti ya mfanyakazi wa majumbani ndiyo inayopokelewa kwanza asubuhi, ikiongoza familia katika maandalizi ya siku.
Wakati mwingine, wao ndio waangalizi wa karibu wa watoto; wanahakikisha wanakula, wanavaa, na mara nyingi hata wanasaidia katika kujenga maadili ya msingi kwa watoto hao, ikiwa ni pamoja na kuwafundisha kusoma au kuandika. Hata hivyo, mchango huu wa kipekee mara nyingi unapuuzwa, ukifichwa na mwanga wa jukumu lao la kazi za nyumbani.

MELBOURNE, Australia
Alexander Zverev amekerwa na shabiki kwa madai ya unyanyasaji wa kijinsia wakati wa hafla ya kupokea tuzo ya Australian Open.
Mchezaji huyo namba mbili wa Ujerumani, alishindwa kwa seti moja kwa moja kutoka kwa nambari moja duniani, Jannik Sinner huko Melbourne.
Alipopiga hatua kupokea kombe lake la washindi wa pili, shabiki mmoja alipaza sauti: “Australia inaamini katika Olya na Brenda.”
Mchezaji huyo alishitakiwa kwa kumnyanyasa mpenzi wake wa zamani Olya Sharypova mnamo mwaka 2020, na unyanyasaji wa nyumbani mnamo 2023 aliyofanya kwa Brenda Patea, ambaye alizaa nae mtoto mmoja.
Zverev mara kwa mara amekuwa akikanusha kesi zote mbili za madai, na kesi ya mahakama ya Berlin iliyoletwa na Patea ilikomeshwa mwaka jana.
Mnamo Oktoba 2020, mpenzi wa zamani Sharypova, alimshtaki Zverev kwa vurugu na unyanyasaji wa kihemko wakati wa uhusiano wao. Zverev alikanusha madai hayo na kusema, “hayana msingi”.
Sharypova hakufungua mashtaka, na uchunguzi wa miezi 15 wa ATP Tour ya wanaume uligundua kuwa hakuna “ushahidi wa kutosha” kuthibitisha madai yaliyotolewa na Sharypova, na hivyo Zverev hakukabiliwa na hatua za kinidhamu.