Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha
Makala

Makala (25)

MWANZA

Na Paul Mabuga

Wakati huko wanafunzi wakiandika matusi kwenye mitihani yao, kule watoto wameiba simu  janja yenye thamani ya zaidi ya Shilingi 300,000/-, baada ya kumhadaa  mama muuza barafu.
Kwenye daladala, konda kavaa fulana yenye maandishi  ya Kiingereza,  yenye tafsiri kuwa amefurahia uzinzi, na  kwenye mtaa jirani Askari Polisi kaibiwa kuku wanne. Lakini, wenyewe tukikutana, tunasalimiana, ‘Mambo poa’.
Yaani kwamba, Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani, Dk. Saidi anatuambia wanafunzi 17, watatu wakiwa watahiniwa wa  darasa la nne na 12 wakiwa ni wa kidato cha pili, wamefutiwa matokeo  baada ya kuandika matusi katika mitihani waliyoifanya mwaka jana.
Yaani, watoto hawa wametukana, ila tu ni kwamba walikuwa wanatukana nini na wanamtukana nani hatujui.
Hii si mara ya kwanza kwa tukio kama hili, kwani kwa  kipindi cha miaka  mitano kuanzia mwaka 2018 jumla ya watoto 33 nao walifutiwa matokeo kwa kuandika matusi katika mitihani yao.
Yaani mwaka huu ni hao 17, lakini mwaka 2022 watahiniwa 14 wa kidato cha pili walifutiwa matokeo pia, na wengine wawili wa kidato cha nne, nao walikumbwa na dhahama kama hiyo mwaka 2022.
Angalia, mtoto mwenye umri wa miaka tisa ama 10 akiwa darasa la nne, anaandika matusi, ama tusema anatukana, na kulifanya taifa kusimama kujadili kishindo chake.
Unadhani akifikisha umri wa miaka 22 na akiwa amehitimu Chuo Kikuu kama atafanikiwa, na ikiwa hakurekebishwa, hali itakuwaje katika muktadha wa kujenga kizazi chenye maadili?
Katika mahojiana kwa ajili ya makala haya, Mwalimu John Ndama kutoka Manispaa ya Shinyanga, anasema, “Haya ni mambo yanayotokea katika miaka ya hivi karibuni,” na katika uzoefu wake wa kufundisha kwa karibu miaka 30 kwenye shule za sekondari, hakuwahi kuona mambo kama hayo.
“Hawa ni watoto watukutu, na kwa bahati mbaya wanazidi kuongezeka kadri miaka inavyozidi kwenda. Inawezekana chanzo kikubwa ni wazazi kushindwa kupata muda wa kuwalea kutokana na kubanwa na harakati za kutafuta fedha, baada ya changamoto za kiuchumi kuongezeka, na badala yake, vijana wanalelewa na runinga na mitandao ya kijamii,” anasema Mwalimu Ndama.
Anasema kwamba yaani watoto wanaona vitendo vyenye  maudhui magumu yenye mwelekeo wa matusi kwenye runinga, lakini pia wanaona maandiko na sauti za matusi kwenye mitandao ya kijamii. Lakini baadhi ya familia zinaona haya ni mambo ya kawaida, na hivyo kuyaruhusu yaendelee bia udhibiti! Tunajenge kizazi cha viumbe kisicho na utamaduni, ‘uncultured creatures’.
Katika hali kama hii inakuwaje? Unasafiri kwenda Mtwara kikazi, lakini basi ulilopanda linaharibika njiani katika moja ya vijiji vya mkoa wa Lindi.
Anakuja kijana anauza mahindi ya kuchoma akiwa amevaa fulana yenye maandishi, “Girls for Sex, No offer Rejected,” (yaani Warembo kwa ajili ya ngono, wapo tayari kwa pesa yoyote). Ukimuuliza maana yake anajifanya kufahamu, lakini anakuambia ni zawadi aliyoletewa na baba yake anayeisha jijini Dar es Salaam.
Kijana anadai anafahamu maadishi, na katika umri wake wa miaka 12, bila shaka ubonge wake ulivyo kama sponji, unamnyinya kila kitu, na kuona kuwa haya ni maisha ya kawaida. Kwa nini huyu asione kuwa kuandika matusi kwenye mitihani, siyo ‘jambo mzungu, [la kustaajabisha]?’.
Unapanda moja ya daladala katika Jiji la Mwanza, konda analifunga kiunoni koti lenye nembo kuonesha kuwa hiyo  ni sare ya kazi. Hali hii inaifanya fulani aliyoivaa na maandishi yake yanayosomeka, “We ejoyed sex overnight!” Hakuna anayemsemesha na kumuonya miongoni mwa abiria, na zaidi wanasalimiana miongoni mwao kuwa ‘mambo poa.’ Fikiria kijana aliyemo ndani ya dalada hiyo, hali hiyo anaichukuliaje?
Katika mtaa mmoja jijini Mwanza, wakati Askari Polisi anamsimulia mama jirani yake juu ya kuibwa kwa kuku wake na vibaka, mama huyo naye anaelezea juu ya watoto wawili wenye umri kati ya miaka tisa na 10, walivyofika kwake na kumuibia simu janja kwa namna ambayo hakuweza kuamini.
Mama huyo, Grace Kezla [43], anasema kwamba alipokuwa ameketi kiambazani nje, walifika watoto wawili na kutaka kununua barafu mbili, na wakatoa shilingi 200.
Mama huyo akaingia ndani kwenda kuchukua hiyo bidhaa kwenye jokofu, kwa bahati mbaya akaacha simu janja kwenye mkeka aliokuwa amekalia. Wale watoto bila kuchelewa walichukua ile simu na kuondoka, na alipotoka nje, hakuona kitu.
“Ni kama vile niliuza simu ya Shilingi 300,000/- kwa Shilingi 200.” Anasema Grace ambaye anapoulizwa kuhusu watoto kuandika matusi kwenye mitahani anasema, “Kwenye jamii yetu kuna vitu haviko sawa, wazazi wameelemewa, na waalimu nao wamezidiwa! Hapo panahitajika juhudi nyingine za ziada, vingenevyo tutapata tabu.”
Anasema, “Wazazi  wapo na shida ya kutumia muda mwingi kutafuta fedha kwa ajili ya mahitaji ya familia. Waalimu nao wanataabika na mzigo mkubwa wa wingi wa wanafunzi kuliko uwezo wao, na hivyo kufanya ‘bora liende’. Wakati hali ikiwa hivyo, bado kwa kila hali, inatakiwa kadri iwezekanavyo, kila kijana amalize elimu ya sekondari.
Anashauri kuwa ingawa mtaala mpya wa elimu una msisitizo juu ya maadili, lakini kuna haja ya jambo hili kuwa mtambuka likihusisha wadau na sekta mbalimbali ili kukikomboa kizazi hiki.
“Kama Waunguja wanaona kuwa kwa mwanamke kukaa kwenye boda, ama kipando kama mwanaume ni sawa na kutukana, badala yake anapaswa kukaa upande, inashindikanaje katika maadili yetu?”
Uzoefu mwingine ni kuhitajika umakini juu ya kusimamia maadili ya kijamii, ni maelezo ya Msese Mwanzalima [80], mkazi wa Shinyanga ambaye anasema kwamba kutokana na waalimu kuzingatia kazi zao enzi hizo, alifukuzwa akiwa darasa ka pili mwaka 1958, enzi za Mkoloni kwa kosa ambalo anadhani pengine leo hii lingevumilika.
“Kwenye madawati, enzi hizo kulikuwa na kitundu kwa jiuu, sasa hapo paliwekwa kidau ambapo kilijazwa wino kwa ajili ya kuchovya ‘pen’ iliyokuwa na ‘nib’, na kuandika.
“Mimi badala yake nilikuwa nachovya kidole katika kidau na kujipaka usoni, ila mchezo huo ulitosha kunifukuzisha shule,” anasema Mzee Mwanzalima akikumbukia hali ilivyokuwa wakati huo, huku akidai kwamba hawa waalimu wa siku hizi, ni wapole sana.

Na Dk. Deoscorous B. Ndoloi

Mpendwa msomaji, katika safu hii, wiki iliyopita tuliona vijitabia zoelefu (offending mannerisms) ambavyo vinaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa namna tunavyozungumza katika hadhara. Tulivitaja vijitabia hivi kama sehemu ya mawasiliano silonge.

Kwa kukumbushana tu, na kwa wale ambao hawakupata fursa ya kusoma makala husika, vijitabia hivi vinahusu kuwa na kitu chochote mdomoni (pipi au kimbaka), kujikuna kusikofaa, kutoa kicheko ‘kichafu’, kuwakonyeza ama kuwagusa wasikilizaji, kupiga chafya ama kukuohoa kusiko na staha, nk. Pengine tulishau vilevile kugusia juu ya vijitabia vya kuchezea vitu wakati tunapotoa wasilisho, kwa mfano hutikisatikisa funguo mkononi ama sarafu mfukoni, hutafuna kucha au mfuniko wa kalamu, kutingishatingisha magoti hasa wakati unapotoa wasilisho umemeketi, ‘kuvunja vidole’ (cracking knuckles), kugusagusa simu nk. Haya yote yatakufanya uonekane hujatulia.

Leo, katika safu hii, tushirikishane maarifa kidogo juu ya kujenga uhusiano wenye tija na hadhira (audience). Kwa wale ambao wanafuatilia mada zetu, tulisema kwamba haitoshi tu kwa mwasilishaji kuwa mbobezi katika uwanja wake, na kuwa na weledi katika kuzungumza katika hadhara, ni muhimu vilevile kujua aina ya wasikilizaji na sababu zinazowafanya wakusikilize. Hii itasaidia jinsi ya kujipanga kuwakabili. Tuone kwa kifupi aina za hadhira.

Aina ya kwanza tunaweza kuiita ni ya ‘hadhira-mateka’ (captive audience). Wasikilizaji wa aina hii wanajikuta kwamba, kimsingi, hapo walipo hawakuja kwa ajili ya kukusikiliza wewe. Kwa mfano wanachuo wapo chuoni kwa sababu moja ya msingi – elimu. Lakini, hata kama somo lako hawalipendi, unapoingia darasani, inabidi wakae kimya na kukusikiliza, kinyume na matakwa yao kwa vile sheria inawabana.

Wafungwa wanaweza kuwa mfano mwingine wa hadhira ya aina hii. Wapo kama kundi kwa sababu wanatumikia adhabu kwa makosa mbalimbali, na ‘wamekusanywa’ bila ridhaa yao. Katika sehemu za kazi, wapo wafanyakazi wengine wanaona kama kuhudhuria mikutano inayoitishwa na uongozi ni kama kupotezeana muda. Wafanyakazi wa namna hii, katika mikutano, ni hadhira-mateka. Wapo kwa sababu tu, wasipotii mamlaka, wanaweza kukaripiwa.

Ukujikuta unazungumza na hadhira kama hii, kwanza, unakuwa na kazi ngumu sana kuwabadilisha mtazamo/msimamo na kuwasabibishia kiu ya kukusikiliza. Katika mazingira haya, dakika chache za mwanzo za kutoa wasilisho ni muhimu sana – waaminishe kwamba una uzoefu na ujuzi katika mada husika, lakini pia washawishi kwamba mada yenyewe ni ya muhimu mno katika maisha yao na hasa katika kuimarisha mahusiano. Ikiwezekana tumia mifano ya watu ambao walishawahi kufanikiwa kimaisha kwa sababu walizingatia unayozungumza.

Aina ya pili ya hadhira ni ‘hadhira-chuki (hostile audience). Hadhira ya namna hii inaweza kuwa inaonesha dalili zote za chuki na kukosa shauku ya kutaka kujua/kuambiwa jambo. Chuki hii inaweza kulenga katika mada yenyewe; kwa mfano, wasilisho linalohusu kuwahamisha na kuwapeleka sehemu nyingine ya nchi kupisha suala ya maendeleo kama ujenzi wa miundombinu ama kuendeleza hifadhi ya wanyama pori.

Kama hadhira hii haioni faida ya haraka na ya moja kwa moja, utapata shida sana kuzungumza nao. Katika hali isitotegemewa, hadhira hii inaweza hata kuzua tafrani, uhasama ama ushari (wa maneno au matendo). Tumeona kwa mfano viongozi wakijaribu kuzungumza na hadhira wakati wa migomo. Wakati mwingine katikati ya mgomo kunaweza hata kuzuka mapigano. Hali ikidorora vya kutosha hadhira kama hii kuamua kutojihusisha na jambo lolote (apathy).

Hadhira-chuki inaweza kuelekeza uhasama wake kwa mtoa mada binafsi, endapo atasema jambo linalowafedhehesha wasikilizaji. Ikumbukwe kwamba hadhira inaweza kuanza vizuri kwa usikivu wa kutosha, halafu polepole au ghafla hadhira inageuka kuwa na chuki, na kuamua kutotoa ushirikiano na mtoa mada.

Ni vizuri ukiwa unatoa mada kugundua iwapo kuna mabadiliko ya tabia-fiche kati ya wasikilizaji inayoashiria kwamba sasa ‘joto linapanda’ na hadhira inaanza kubadilika kihisia. Matendo na maneno yao madogomadogo yataashirika kinachoenda kutokea.

Vilevile tuliona juu ya mawasiliano silonge (non-verbal communication) na jinsi watu wanavyoweza kuzungumza hata kwa ‘kupiga kelele’ bila kufungua mdomo. Ukiwa mwasilishaji uwe hodari kugundua hili na kutumia mbinu zote kurudisha hali ya hewa katika hali ya utulivu.

Wakati mwingine hadhira inaweza kuwa na chuki na mamlaka yenye uhusiano na mwasilishaji, kama serikali. Hivyo kwamba chuki hii haielekezwi kwa mzungumzaji moja kwa moja, bali kwa serikali kupitia kwa mzungumzaji. Ni vema kama wewe ni mzungumzaji kujua uhasama au chuki hii inaelekezwa wapi, usije ‘ukanunua’ tatizo lisilokuhusu.

 Ni lazima kuwa mwangalifu na kuwa na weledi wa kisaikolojia kuweza kukabiliana na hadhira ya namna hii. Ni vema kutojitenga na tatizo, lakini ni vema zaidi kujua jinsi ya kukabili mabadiliko ya usununu wa hadhira. Kumbuka mhemko huambukiza; hivyo inasaidia kuukabili inavyofaa, pale unapoanza kwa mtu mmojammoja.

Jambo ambalo ningetaka kumalizia nalo, ni kwamba kama mwasilishaji mada, utakuwa umefeli kabisa ukiruhusu mhemko wa hadhira ukakuingia, na wewe ukapata hasira au ukaanza kuonyesha chuki, kwa sababu eti unahusishwa na masuala yasiyokuhusu.

Katika hali yoyote ile ya mhemko wa chuki toka kwa hadhira, uwe na busara ya kujizuia na usikubali kurubuniwa kisaikolojia, ukafanana na hadhira ya namna hii. Unapotoa mada uwe na utulivu ambao wasikilizaji wataona kwamba unayoyaona yahajakufanya ukatetereka toka kwenye kusudio lililokupeleka.
Tumsifu Yesu Kristu!
Itaendelea wiki ijayo.

DAR ES SALAAM

Na Dkt. Felician Kilahama

Ni vema na haki kumshukuru Mungu Mwenyezi kwa kutuwezesha kuendelea kuishi, tukipumua bila ya athari zozote. Hayo ni mapenzi yake, siyo kwa ridhaa au nguvu zetu wenyewe, bali ni kwa rehema zake kuu, hivyo, jina lake lihimidiwe.
Katika sehemu ya kwanza, Makala iliishia kwenye kipengele kilichozungumzia kuhusu vijana kupenda kupata fedha kirahisi, mfano, kupitia masuala ya ‘kubeti’.
Hatinaye, kueleza ‘ipo michezo mingine mingi inayochezwa kupitia mitandao na vyombo mbalimbali vinavyohimiza Watanzania kucheza ili kujipatia fedha kirahisi.’ Haya yote yanafanyika kwa mwelekeo wa kamari (gambling au gaming), na vijana wengi wamevutwa.
Kimsingi, masuala yanayohusiana na kucheza kamari siyo mazuri, maana yanapelekea mhusika kupotoka na kujikuta akitenda maovu. Kwanza, kuna kutekwa kifikra/kiakili na kupoteza maarifa ya kufanya uamuzi sahihi.
Kila wakati mhusika anabaki akijiweka kwenye nafasi ya kushinda, huku akitumia fedha ambazo harudishiwi iwapo hatashinda. Pili, michezo ya aina hiyo inajenga lango la kutenda uovu, ikiwemo wizi na, au udanganyifu.
Mhusika iwapo hana fedha za kumfanya acheze, atafanya kila linalowezekana apate fedha kihalali au vinginevyo, ili mradi afanikishe lengo.
Kihalali anaweza akauza vitu vyake, mfano, nguo, viatu, simu kiganjani au akahangaika akapata kibarua na kupata fedha akacheze kwa mtazamo kuwa atashinda na kupata fedha atajirike.
Vinginevyo, kuna uwezekano mkubwa wa kujenga tabia ya kudokoa mali za wengine, au kuiba fedha na vitu vingine nyumbani, mitaani na hata kupora, ili mradi afanikishe lengo lake.
Kwa bahati mbaya, mtazamo huu usiofaa kwa vijana ambao ndiyo nguvukazi kubwa ya taifa letu, unachochewa na baadhi ya matangazo yanayofanyika kupitia vyombo mbalimbali vya matangazo.
Mathalani, luninga, redio, magazeti na hata simu janja au za kawaida, kwamba kuna wakati ninapofungua sehemu ya ujumbe kwenye simu; mara kwa mara huwa nakuta ujumbe kutoka namba fulani wakitangaza, ‘wewe umekaribia kushinda kiasi fulani cha fedha, mathalani, milioni mbili, tuma neno fulani ushinde.’
Kadhalika, unaambiwa ‘weka Tshs 500 ujipatie hadi Tshs milioni tatu na bonasi ya Tshs 200,000 papo hapo,’ au ‘wewe ni milionea mpya, chagua namba 1 hadi 6 uweze kushinda hadi milioni mbili na ‘Jackpot’ ya Tshs 300,000 kila siku.’ Vile vile maneno “funua pesa mkwanja tele maisha mapya …”
Wakati mwingine unakuta kwenye gazeti, kumewekwa, mathalani, “Supa Jackpot” (TZS 1,150,172,000 kwa TZS 1,000 tu). Kijana akiangalia tarakimu hizo na kwa lugha ya mitaani: kwa buku tu, anahamasika kucheza. Lakini ili aweze kushinda na kupata hizo fedha, atacheza mara ngapi? Yote haya ni katika kukengeuza akili za wengi na hasa vijana ambao ndiyo kundi kubwa linaloathirika zaidi.
Wakati mwingine yanaletwa maswali kadha wa kadha, na mengi ni ya kimichezo, hasa soka na, au kuigiza. Pia, nyimbo hasa ‘bongo fleva’ na waimbaji wake. Nia ni watu wengi wajibu ili wakwapue hela kutoka kwenye bando kupitia mitandao husika. Katika uhalisia wa michezo kama hiyo, wengi wanaangamia, na wataangamia kwa kukosa maarifa.
Kimsingi, michezo (gaming/gambling) ni aina ya kamari hata kama tukisema imeboreshwa, lakini ni pata potea. Inafanya wengi wapoteze fedha zao kwa matumaini ya kupata/kushinda, wakati wanaoshinda ni wachache sana kulingana na idadi ya wanaocheza.
Kabla mhusika hajacheza mchezo wowote wa kubahatisha, ni lazima kujua asilimia ya kushinda, au uwezekano wa kushinda (probability rating); na hilo ni jambo la msingi, mathalani, kuna wachezaji milioni moja kwa mchezo mmoja, na pengine anatakiwa apatikane mshindi mmoja, washindi kumi, au washindi mia moja. Kinachotakiwa kukifahamu ni kujua kwa kiasi gani unaweza kushinda.
Kwa kundi la kwanza zitatolewa milioni moja; kundi la pili milioni kumi (washindi 10) na kundi la tatu milioni miamoja (washindi 100). Kiwango cha ushindi ni asilimia 0.0001; 001 na 0.01 kwa makundi hayo matatu mtawalia. Hali hiyo inaonyesha kuwa ni asilimia ndogo sana ya mhusika kuweza kuibuka mshindi, ndiyo maana ikaitwa ‘bahati nasibu’.
Kadhalika, baadhi ya vijana hutembeza barabarani baadhi ya bidhaa mbalimbali mikononi wakitafuta wateja.
Wengine wanatumia muda mrefu kutoka eneo moja kwenda jingine wakitafuta wanunuzi.
Jioni inapoingia, mhusika anapoona hana kitu mfukoni na njaa inamuuma, analazimika auze kwa bei mnunuzi anayotaka, ili mradi apate kiasi cha kumsaidia aweze kujikimu. Baadhi wana familia hivyo hujikuta katika changamoto hatarishi kiasi cha kulazimika kutenda uovu kwa kigezo cha hakuna jinsi, bora nusu shari, kuliko shari kamili, anaitelekeza familia yake.
Tujiulize kwa mustabali wa taifa letu, je, vijana kutaka kupata fedha haraka haraka kupitia michezo mbalimbali ya kifedha kama ‘kubeti’ na mingineyo, kitaifa ni jambo jema? Je, vijana na watu wengine tunatumia muda vizuri kwa manufaa yetu, familia na taifa kwa ujumla?
Kimsingi, matumizi halisi ya ‘muda’ kwa nyakati hizi ni suala la kuwekewa mkazo. Kila siku tunapoamka tunafanya nini? Maana unakuta makundi ya watu wa rika mbalimbali wakiongelea masuala ya michezo, mfano, kusajili wachezaji, hususani timu za Tanzania na za Uingereza.
Kadhalika, unaona vijana wanatumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii ‘wakichati’ kupitia simu za kiganjani. Je, ni matumizi halisi ya muda? Siku ina saa 24 na wiki ina siku saba au saa 168.
Kawaida binadamu anatakiwa kulala usingizi (angalau saa 8 kwa siku), kwa wiki atatumia saa 56 kitandani. Kwa wiki, ukiondoa siku moja ya kuabudu/kusali, kuna siku sita za kufanya kazi. Hii inamaanisha kuwa tukiondoa saa za kusinzia, kwa siku tuna saa 16 za kufanya kazi, na ndani ya siku sita, ni takribani saa 96 za kufanya kazi.
Muda huu ukitumiwa kwa kiwango cha kufikia asilimia 75 (takriban saa 12 kwa siku, sawa na saa 72 kwa wiki), ukatumika kuzalisha mali na huduma ili kujipatia kipato, hakika tutajikwamua kimaendeleo (muda uliobaki, takriban saa 4 kwa siku au saa 24 kwa siku sita za kazi; ukatumika kwenda na kutoka mahali pa kazi, pengine kupata mapumziko mafupi wakati mhusika akiwa kazini).
Uzoefu unaonyesha kuwa wengi wetu, wakiwemo vijana, hatuzingatii matumizi mazuri ya muda, iwe ofisini, viwandani au kwingineko, kwani bado kuna kusuasua bila maelezo toshelezi. Hivyo, vijana tujiepushe kufuata mkumbo kwa masuala yasiyotuletea maendeleo ya kweli kimaisha.
Serikali iweke Sera thabiti kuinua maisha ya Watanzania hususan vijana. Tuliporuhusu matumizi ya ‘bodaboda’ na ‘bajaji’ kutoa huduma za usafiri na usafirishaji, jambo hilo limekuwa faraja kwa vijana wengi kujiajiri au kuajiriwa. Wanaoitumia fursa hiyo kwa umakini baada ya miaka miwili au mitatu, wanasonga mbele ipasavyo.
Mkakati wa Serikali wa kuinua zaidi shughuli za kilimo kwa lengo la kuwapatia vijana ajira na kuimarisha au kuendeleza uchumi wa taifa, upewe msukumo zaidi ili kuhusisha sekta mbalimbali za umma na binafsi. Kupanuliwe wigo ili vijana wengi waweze kujipanga vizuri kulingana na uwezo waliopewa na Mwenyezi Mungu.
Wenye ari ya kufuga wafanye hivyo kitaaluma na kibiashara; wenye kumudu masuala ya uvuvi, misitu na nyuki na utalii, pamoja na biashara, wafanye hivyo bila shida. Shughuli za ugani ziimarishwe ili kuhakikisha mafanikio tarajiwa yanapatikana.
Tukiongeza tija kwa bidhaa nyingi kuzalishwa hapa nchini, tutajenga uwezo wetu wa kujitegemea. Wakati huo huo, tutasaidia idadi kubwa ya vijana kuachana na ‘michezo potofu’, hivyo kuimarisha ‘nguvukazi’ ya taifa letu kwa faida ya wengi.
Halmashauri zote nchini na Mamlaka za Mikoa na Wilaya, zihakikishe kuna mazingira mazuri ya kuwezesha vijana kutumia rasilimali ardhi kwa faida na weledi mkubwa, mathalani, Halmashauri zianzishe mifumo thabiti ya kuunganisha ‘nguvukazi-vijana’ kwenye maeneo yao.
Kuweka fursa za ‘mitaji’ kuwakopesha vijana; tukizingatia masharti nafuu na kuweka ‘kanzidata’ kuhusu vijana kuhusiana na taaluma au uwezo wao.
Katika kuyatekeleza hayo, uwazi na uadilifu vizingatiwe ipasavyo. Vijana wajengewe mazingira ya kuwa waaminifu katika kutumia muda vizuri na kutimiza wajibu wao ipasavyo. Viongozi na wenye madaraka kwa ngazi zote, tuwe waadilifu, siyo kwa maneno tu, bali kimatendo.
Tuchukie ‘udanganyifu, wizi, kutoa au kupokea rushwa, au kukwapua’ mali za umma. Hayo yawe mwiko mkubwa katika sifa za kiongozi mzuri anayetumainiwa na wengi.
Tamaa za kujitajirisha ‘chapuchapu’ (yaani haraka haraka) kwa kutumia njia haramu na zisizofaa, vikomeshwe, na watakobainika wachukuliwe hatua kali za kiutawala na kisheria. Tafakari kwa kina, chukua hatua madhubuti.

Wiki iliyopita tuliwaletea kazi alizozifanya Papa Yohana XXIII katika kipindi kifupi cha uongozi wake. Leo tunawaletea historia ya uongozi wa Mrithi wake Papa Paulo VI na kuendeleza yale ya mtangulizi wake. Sasa endelea

Papa Yohana XXIII (1958 - 1963: wa 261) alipofariki Juni 3 1963, mambo yote ya Mtaguso yalisitishwa kumsubiri Papa mpya ambaye angeliamua kama Mtaguso uendelee au uishie hapo. Tarehe 21 Juni 1963 alichaguliwa Kardinali Yohana Baptista Montini, Askofu Mkuu wa Milano.

Montini alikuwa mmoja wa Makardinali wenye msimamo wa kati. Siku moja baada ya kuchaguliwa, alitangaza kwamba Mtaguso utaendelea na kwamba atajaribu kutimiza malengo yaliyowekwa na Papa Yohana XXIII. Alisisitiza kuwa  Mtaguso ndio utakuwa kipaumbele chake cha kwanza.

Kardinali Montini alizaliwa tarehe 26 Septemba 1897 huko Concesio Italia. Alipadrishwa mwaka 1920 na kutumwa Roma kwa masomo, ambako baadaye aliingizwa katika Idara ya Mambo ya Nje na kutumwa Ubalozini Warsaw, Poland, mwaka 1923 na baadaye kurudi ofisini katika idara hiyo Roma.

Mwaka 1954 Papa Pius XII (1939 - 1958: wa 260) alimteua Montini kuwa Askofu Mkuu wa Milano, na Papa Yohana XXIII akamfanya Kardinali mwaka 1958. Tarehe 21 Juni 1963, akachaguliwa kuwa Papa na kuchukua jina la Paulo VI.

Papa Paulo VI (1963 - 1978: wa 262) aliamini katika muendelezo wa mapokeo ya Kanisa bila kuyachakachua, lakini pia aliamini mapokeo yasiyokuwa ya msingi na yanayokinzana na alama za nyakati yanapaswa kuhuishwa na kufanywa upya.

Mara moja aliimarisha Tume alizoziweka Papa Yohana XXIII na kuongezea sura mpya. Kati ya Wenyeviti wa Mikutano, jumla aliweka mchanganyiko wa wanamapinduzi kama Kardinali Suenens wa Ubelgiji, Kardinali Doepfner wa Ujerumani, na Kardinali Lercaro wa Bologna, Italia, na wale wenye msimamo wa wastani kama Kardinali Agagianian. Makardinali hawa wanne ndio walikuwa mpini wa mwenendo wa Mtaguso.
 
Papa Paulo VI aliwaalika Walei kuhudhuria vikao vya jumla bila kusema au kipiga kura. Aliruhusu vile vile habari za mwenendo wa Mtaguso kutolewa mara kwa mara kwa Waandishi wa Habari.

Kikao cha Pili, Septemba 29 hadi Desemba 4, 1963:
Papa Paulo VI aliitisha kikao cha pili kuanzia tarehe 29 Septemba hadi Desemba 4 mwaka 1963. Katika ufunguzi wa kikao hicho, alirudia nia yake ya kufuata nyayo za mtangulizi wake. Wakati wa ufunguzi, alitoa madhumuni manne ya msingi kwa Mtaguso huo:

1.    Kanisa lijitambulishe kwa Ulimwengu kwa tamko rasmi, likijielezea kwa kujielewa.

2.    Aggiornamento, yaani kufanya upya, lazima iendelee, si kwa kuvunja mila na mapokeo msingi, bali kwa kuondoa kile ambacho kina kasoro.

3.    Kanisa lazima lifanye kazi kuelekea kwa umoja kati ya Wakristo wote. Wakati wa ufunguzi akisema hivyo, aliwageukia waangalizi wasio Wakatoliki na kuomba msamaha kwa jeraha lolote ambalo Kanisa Katoliki lingekuwa limewasababishia Wakristo wengine.

4.    Kanisa lazima lijihusishe na mazungumzo na Ulimwengu: “siyo kushinda na kuuteka, bali kutumikia, si kudharau bali kuthamini, si kuhukumu bali kufariji na kuokoa”.

Kikao cha Tatu, Septemba 14 hadi 21 Novemba 1964:
Katika kikao cha tatu, kutokana na manung’uniko ya Kardinali Suenens kwamba kulikosekana Wanawake Walei Waangalizi kwa sababu kulikuwepo Masista tu, Papa aliwateua Wanawake 15 Walei Waangalizi kuungana na Masista 10.
 
Kipya kingine katika ufunguzi wa kikao hicho, Papa aliadhimisha Misa na Maaskofu 24 kutoka nchi 19. Hii ilikuwa mara ya kwanza katika Kanisa la Kirumi, kwa sababu kabla ya hapo kila Padre aliadhimisha peke yake. Mapinduzi ambayo sasa ni jambo la kawaida yalikuwa yameanza.

Kikao cha Nne, Septemba 14 hadi Desema 8, 1965:
Kikao cha nne na cha mwisho kilikuwa tarehe 14 Septemba hadi 8 Desemba mwaka 1965. Kikao hiki kilikuwa kirefu zaidi ya kingine chochote kilichotangulia  kwa wiki mbili, kwani hiki kilikuwa cha wiki 12.

Katika ufunguzi wa kikao hiki, alitangaza kwamba kutakuwepo na Sinodi za Maaskofu pamoja na Baba Mtakatifu katika ngazi ya Kimataifa ili kumshauri Papa. Hii iliwafurahisha wengi. Hadi sasa, Sinodi hizi zinafanyika.

Mwishoni mwa kikao cha nne ambacho ndicho kilikuwa kikao cha mwisho, kuna matukio muhimu yalifanyika. Kitu kipya kabisa Papa alisali pamoja na Wakristu wa madhehebu mengine waliokuwa katika Mtaguso.

Tarehe 6 Desemba 1965, alitangaza Mwaka wa Jubilee kuanzia tarehe 8 Desemba 1956 hadi tarehe 8 Desemba 1966, kwa ajili ya kutangaza na kueneza Mafundisho ya Mtaguso wa Vatikani II (1962 - 1965).

Tarehe 7 Desemba akiwa pamoja na Patriarka Athenegoras wa Konstantinople, ambaye alikuwa Mkuu wa Kanisa la Kiortodosi, walilaani utengano, chuki na kuhukumiana (Excommunications) zilizofanyika mwaka 1054, zilizotenganisha Kanisa la Kiortodosi na Kanisa Katoliki.

Wote walisameheana rasmi, na kuahidi kufanya wawezavyo ili kurudisha umoja. Tarehe 8 Desemba 1965, Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatikano ulifungwa kwa Misa Takatifu iliyoadhimishwa na Papa katika Uwanja wa Basilica ya Mtakatifu Petro, huko Vatikano.

Matokeo ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano ni kwamba kwanza uligeuza muono wa Kanisa Katoliki na kulileta katika mtazamo wa nyakati zake, bila kugeuza Mafundisho na Mapokeo Msingi ya Kanisa.

DAR ES SALAAM

Na Joseph Mihangwa

Mzungu hajakubali kuwa bin-Adam wote ni sawa, wala kwamba wote ni wa baba mmoja, Adam. Pamoja na kwamba alituletea Msahafu wa Dini, yaani Biblia wenye kusisitiza “upendo”, hiyo ni ghiliba tupu kwa sababu inawabagua wana-Adam kati ya walio wana wa Taifa teule la Mungu [Israeli] na wana wa Mataifa yasiyo teule. Huko ni kukweza ngozi nyeupe.
Kwa kutumia Mungu wa kujiundia [Yahweh] na Msahafu wa kibeberu, wanaidhinishwa kutugeuza watumwa wao, eti kwamba: “Na wageni watakuwa watumwa wa kulisha mifugo yenu; na wana wa Mataifa watawalimia na kutunza mashamba ya mizabibu yenu”. Huo ndio ubaguzi wa ubeberu wa kimataifa ambao umedumu hadi leo.
Ubaguzi huo kwa misingi ya rangi ulioasisiwa, kusimikwa na kukomazwa Kimataifa na Mjerumani Johann Friedrich Blumenbach [1752 – 1840], unawagawa bin-Adam kwa viwango vya ubora katika makundi sita ya Watu weupe [Coucassians] kama daraja la kwanza; Wamongolia [Mongoloid] daraja la pili; Watu weusi [Ethiopoid]; Wamarekani wenye asili ya Kihindi [Red Indians] na Wahimalaya [Malayans] kama daraja la mwisho kwa ubora.
Wamefika mbali kwa kudai kuwa Mwafrika si Mwana-Adam, yaani hakuzaliwa na Adam. Dhana hiyo mpya inayoitwa ‘Pre-Adamisma’, inadai kuwa Mwafrika alikuwepo kabla ya kuumbwa Adam, na alikuwa kiumbe asiye na roho.
Mwasisi na Mwenezi wa dhana hiyo inayoshika kasi kipindi hiki cha utandawazi, ni Mfaransa Isaac La Peyrere [1596 – 1676]. Dhana hiyo inapinga usahihi wa Biblia juu ya uumbaji, ikidai kuwa kulikuwa na watu kabla ya kuumbwa kwa Adam na Hawa.
Anadai kwamba kulikuwa na uumbaji mbili za watu: uumbaji wa kwanza ulikuwa wa dunia nzima na Mwafrika kama mtu wa kwanza; na uumbaji wa pili ulihusu Wayahudi kama Taifa ambalo Adam alikuwa mkuu wake.
Anadai kuwa, Mataifa yote hayatokani na Nuhu, kwamba watu wa Mataifa [wasio wa Taifa teule] hawakutenda wala hawahusiki na dhambi ya asili kwa sababu walikuwepo kabla ya Adam, na hivyo hawakupokea “Sheria” au Maagizo ya Mungu, bali ni Adam na uzao wake pekee. Chini ya dhana hiyo, Wazungu ni Wana-Adam, na Mwafrika, siye.
Dhana hii ina watetezi wengi miongoni mwa Mataifa ya Ulaya: Mathew Fleming Stephenson, katika kitabu chake “Adamic Race” anasema, “Mungu alitumia mamilioni ya miaka kuumba mtu duni [Mwafrika] kabla ya kuumba mtu bora aina ya Mzungu [Caucasian] juu yake”. Wengine, kwa kutaja wanataaluma wachache tu, ni pamoja na John Harris [The Pre-Adamite Race], Isabelle Duncan [Adamites and Pre-Adamites], na wengine.
Iwe ni kwa mtizamo wa dhana ya “Pre-Adamite”, “Uumbaji” au “Mageuko” [evolution], hakuna ubishi mpaka sasa, kwamba binadamu [mtu] wa kwanza aliishi Loliondo/Ngorongoro zaidi kabla ya mwaka 10,000, Kabla ya Vizazi [KV], ambao ndio mwaka unaosemekana Adam aliumbwa.
Ustaarabu wa mtu huyu ulianza na shughuli za kilimo, ufugaji, ibada na makazi, eneo ambalo sasa linajulikana kama Nubia, au Sudan Kaskazini. Utawala wa kwanza ulianzia Ta-Seti, eneo hilo watu hawa walijulikana kama “Anu”.
Nchi waliyokalia ilijulikana kwa majina mengi, kama vile, Nubia, Kermet, Kush, Ethiopia au Egypt [Misri], na Mji Mkuu ulikuwa Kerma. Nubia imetajwa kwenye Biblia, Kitabu cha Mwanzo 2:11 kama nchi ya Havillah.
Ni Ufalme ulioundwa na watu weusi kutoka eneo la Maziwa Makuu [ANU] miaka ya 5900 Kabla ya Vizazi [KV], na maelfu ya miaka kabla ya Kisto [KK]. Hapa ndipo Gharika [la Nuhu] lilipowakuta watu hawa, wakaangamia, isipokuwa mtu mmoja – Nuhu na wanae watatu – Yafeti, Shem na Hamu. Hiyo ilikuwa Mwaka 5000 KK.
Wakati ardhi ilipoonekana kutotosheleza familia za ukoo huu ulioendelea kupanuka, Nuhu akawagawia wanawe maeneo ya kutawala: Yafeti alipewa eneo lote la nchi ya Kaskazini ya Dunia, yaani Ulaya yote; Shem maeneo yote ya Mashariki ya Kati na Asia, wakati Ham aligawiwa eneo lote la Bara la Afrika na Marekani Kusini. Ifahamike kuwa wote hawa walikuwa watu weusi kipindi hicho kabla ya koo zao kubadilika rangi maelfu ya miaka baada ya kuhamia nchi mpya.
Ham na ukoo wake alijijengea himaya ya Kikemeti yenye nguvu kiuchumi, Kijeshi na Kitheolojia kwa imani ya Kikemeti iliyotambua uwepo wa Mungu mmoja [Baba].
Mkanganyiko wa kidini na kitheolojia kati ya Mwafrika na Mzungu, unaanza na mtu mmoja aliyeitwa Abraham kutoka Mesopotamia [Ur], aliyeoteshwa ndoto na Mungu wake akielekezwa kwenda [kutafuta makazi] Kanaani, nchi ya Mwafrika aliyeitwa Kanaani, mwana wa Ham na mjukuu wa Nuhu.
Kutoka Kanaani, akaenda Misri Mwaka 1871 KK wakati mtu mweusi alikuwa mtawala na kurejea tena Kanaani, akanunua shamba kutoka [Ephron] ukoo wa Hiti [Wahiti], mwana wa pili wa Kanaani, na kufanya makazi [Mwanzo 23:1-20; 25: 7-10].
Wakati Abraham akiondoka Ur [kwa kukosana na mtawala wa eneo lake] Mesopotamia, ilikuwa chini ya himaya ya utawala wa Mwafrika aliyeitwa Nimrodi, mwana wa Kush na mjukuu wa Ham. Dini na theolojia iliyoongoza huko ilikuwa ya Kikemeti/Kiafrika kutoka Nubia/Afrika. Abraham alikuwa wa uzao wa Nmrod, kwa hiyo alikuwa Mwafrika na alikimbilia Kanaani na Misri kwa watu weusi wenzake.
Musa alikuwa mtu mweusi, la sivyo asingelelewa kwa Farao mweusi, na hatimaye kupewa madaraka ya kitawala kabla ya kukimbilia Nubia/Ethiopia kwa tuhuma za kuua raia. Huko alioa mke wa Kikushi aliyeitwa Tharbis, mweusi tii, wakapata watoto.
Kutoka ukimbizini Nubia/Ethiopia akaenda Midiani, akafikia kwa Kingozi wa eneo hilo, Mzee Yethro aliyepata kuwa Mshauri wa Farao miaka ya nyuma. Akamuoa Ziporah, binti wa Yethro, mweusi tii kama alivyokuwa Tharbis wa Nubia. Akawa na wake wawili wakiishi mbali mbali. Hawa aliwakusanya na kwenda nao Kanaani.
Yethro alikuwa mtu mweusi wa ukoo wa Abraham kwa mke wa mjomba wake, Keturah. Na Musa angekuwa Mwisraeli [wa Taifa teule] asingeoa wake wa Kiafrika – Tharbis na Ziporah.
Wanaofikiriwa kuwa “Waisraeli” aliwaongoza kutoka Misri kwenda kuvamia Kanaani ya Wakanaani, hawakuwa Waisraeli kwa maana halisia, wengi walikuwa weusi hasa wale wa uzao wa wake za Yakobo, Leah, Raheli, Zilpha na Bilha ambao walikuwa Wakush/Wanubia kwa asili.
Na hii inajieleza wazi kuwa walioongoza maasi jangwani dhidi ya Musa walikuwa wenye asili ya Nubia/Afrika, akiwamo On [Anu] mwana wa Paleth na mmoja wa Wakuu wa kabila la Reuben, mtoto wa kwanza wa Yakobo kwa Leah.
Wengine walikuwa ni Korah [mtoto wa tatu wa Esau kwa mke wa Kikanaani, Aholibamah]; Dathan na Abiram, wote wana wa Eliab, waliendesha mgomo kupinga uvamizi wa Kanaani uliokusudiwa na Musa na washirika wao wachache wenye nia ovu.
Mazungumzo ya Musa na Mungu wa jamii ya Kiyuda yenye lengo la kujikweza ambapo inadaiwa alipewa amri kumi, ndicho chanzo cha ubaguzi wa kikabila na kitheolojia uliojenga ubeberu wa Taifa moja dhidi ya mengine. Ni nani mwenye uhakika juu ya usahihi wa dhana ya “Mungu wa Israeli” dhidi ya Mataifa mengine sawa tu na dhana ya “Pre-Adamism?”
Wanaakeolojia wanatuambia kuwa, dunia iliumbwa miaka bilioni 13 iliyopita; Adamu aliumbwa Mwaka 10,000 KV, na Wanahistoria wanasema mwaka huo [10,000], tayari Mwafrika alikuwa ameenea sehemu zote za Ulaya, Asia, Australia na Marekani Kusini.
Waafrika hao walisambaa kutoka Loliondo/Ngorongoro hadi Nubia na kuenea duniani kama ifuatavyo: Miaka 100,000 iliyopita, walijaza Palestina, Israeli na Yemen; Miaka 65,000 iliyopita wengine walitumia mkondo wa Bahari ya Atlantiki, wakaingia Amerika ya Kusini.
Miaka 50,000 iliyopita, wengine walitokea Kusini Mashariki ya Bara la Asia wakawasili Australia, wakajaza Visiwa vya Pasifiki mpaka Hawaii. Na Miaka 40,000 iliyopita wakaingia nchi za Skandinavia na Uingereza.
Wanahistoria na Wanafalsafa nguli wa kale, Flavius Josephus [37 – 86 BK], Lucius Plutarchus [46 – 119 BK], Publius Tacitus [56 – 120 BK], Eusebius Pamphilus [260 – 339 BK] na Diodurus Siculus [90 – 20 KK] walioishi kabla ya Torati [Diodurus] na Kabla ya Biblia ya Agano Jipya kuandikwa [78 BK], wanakiri kuwa Waebrania asilia walikuwa ni kikundi cha Wanubi/Wakush waliolazimika kuhama Nubia/Kush/Ethiopia kwa miguu kwenda nchi ya Kanaani, aliyotawala Kanaan, mwana wa Ham na mjukuu wa Nuhu. Ilikuwa nchi ya Waafrika eneo la Afrika Kaskazini Mashariki.
Hii ndiyo nchi ambayo Abraham aliishi kwa miaka 100 na kumuoa Hajir, Mkushi [Mwanzo 15:3]. Mipaka ya nchi hiyo Kanaani na ukoo wake waliishi na kutawala, kwa mujibu wa Mwanzo 10:19] ilikuwa “kutoka Sidoni hadi Gerari hata Gaza; Sodoma na Gomora, na Adma, na Seboimu hadi Lasha na Afrika Mashariki yote.”
Ham ni Mwafrika kwa mujibu wa Biblia. Mwanae [Kanaani] hawezi kuwa mtu mweupe. Kush, mwana mwingine wa Ham, alitawala Sudani ambayo imo Afrika – ikijulikana wakati huo kama nchi ya Kush.
Misraim, mwana mwingine wa Ham, alitawala Misri ambayo imo Afrika [Zaburi 105:23 – 27]. Uzao wake ni wa Waafrika, si wa watu weupe.
Phut, mwana mwingine wa Ham, alitawala nchi yote inayoitwa leo Libya. Kwa hiyo, ni wazi kuwa nchi na Mataifa yote yanayotajwa katika Biblia ni mali ya Afrika na Waafrika, na si ya Ulaya na Wazungu.
Mungu aliwekeza Loliondo/Ngorongoro siri na madhumuni ya uumbaji kwa utukufu wake. Uwekezaji mwingine hapo kwa uchu wa mali na wenye kufifisha kazi yake ni kufuru kubwa kwa wakfu.

Wiki iliyopita tuliwaletea historia ya mchango wa Kanisa wakati wa kupambana na athari ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia (1939-1945). Leo tunawaletea mrithi wa Papa Pio X11 (1939-1958: wa 260) ambaye ni Papa Yohana XX111, aliyepigiwa kura mara 12 kumpata. Sasa endelea.

Papa Yohana XXIII (1958 - 1963: wa 261), zilipigwa kura mara 12 kabla ya kumpata. Uchaguzi wa Papa wa kumrithi Papa Pio XII, haukuwa rahisi kama uchaguzi wake. Inasemekana kwamba kura zilipigwa mara 12 ili kumpata. Kulikuwepo na wengi ambao walidhaniwa wangemrithi, lakini sasa dunia ilihitaji zaidi Mchungaji kuliko Mtawala.
Papa Pio XII alikuwa labda Papa wa mwisho wa mapokeo ya kifalme. Katika hali ngumu ya kumpata mtu wa kukidhi mategemeo ya wote, walimchagua mtu wa mpito wakiwa wanajipanga vizuri.
Walimchagua mtu ambaye hisia zake zilikuwa za mkulima, mtu rahisi kuongea naye na kufikiwa. Umri wake, miaka 76, ulikuwa umekwenda, hivyo hakutegemewa kukaa muda mrefu.
Alichaguliwa Kardinali Angelo Ronccali ambaye alichukua jina la Papa Yohana XXIII. Kardinali Ronccali alikuwa na uzoefu wa kukutana na watu wa aina mbalimbali wa kutoka nchi mbalimbali.
Ni vema na haki kujua vizuri maisha ya Papa huyu aliyebadili mwelekeo wa Kanisa katika Ulimwengu wa sasa. Kinyume na mategemeo ya wote, alifanya kazi ambayo ilikuwa haijafanyika tangu Mtaguso Mkuu wa Trento katika karne ya 16.
Angelo Giuseppe Roncalli, mtoto wa tatu kati ya watoto kumi na watatu, alizaliwa tarehe 25 Novemba 1881 huko Sotto il Monte (Bergamo), kwenye familia ya wakulima. Alipadrishwa mwaka 1904, na akaendelea na masomo na kupata Shahada ya Uzamivu katika Sheria za Kanisa.
Akiwa Katibu wa Askofu mpya wa Bergamo, Giacomo Radini –Tedeschi, Angelo alipigania haki za jamii, na baadaye alifundisha Seminarini Historia ya Kanisa, na masomo mengine. Wakati wa Vita Kuu vya Kwanza (1914-1918), mwaka 1915 alijitolea kama mhudumu wa kiroho (Chaplain) wa wanajeshi. Baada ya vita, alikuwa mlezi wa kiroho wa Seminari.
Mwaka 1921 aliitwa Roma na Papa Benedikto XV (1914-1922: wa 258) kusaidia kupanga upya Idara ya Uinjilishaji (Propaganda Fide). Mwaka 1925 alitumwa Bulgaria kama Mwakilishi wa Papa, na huko alijishughulisha na Makanisa ya Mashariki (Waortodosi). Mwaka 1934 alitumwa Uturuki na Ugriki, makao yake yakiwa Istanbul (Konstantinople ya zamani).
Huko, licha ya Wakristu Waortodosi, alikutana kwa karibu na Waislamu. Mwaka 1944 alitumwa kumwakilisha Papa huko Paris, Ufaransa, ili kusaidia Kanisa hilo kubwa kujiunda upya baada ya vita.
Hii haikuwa kazi rahisi kwa sababu Balozi aliyetangulia alishirikiana na Wajerumani. Hivyo serikali ya Rais De Gaule na Wafaransa, walimchukia pamoja na Maaskofu waliofuta, nyayo zake. Sasa Askofu Mkuu Roncalli, ilibidi afanye kazi ya ziada kutuliza hali.
Wakati huo alikuwa vile vile Mwakilishi wa Papa katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Kushughulikia Watoto (United Nations International Children’s Emergency Fund: UNICEF). Baada ya kazi nzuri akiwa na umri wa miaka 71, mwaka 1953 aliteuliwa kuwa Kardinali na Patriarka wa Venezia.
Papa Pio XII alipofariki (Oktoba 1958), Makardinali walikuwa na wakati mgumu kukubaliana juu ya nani amrithi. Ilikuwa vigumu kupata theluthi mbili za kura kwa mtu mmoja. Hivyo, baada ya kupiga kura mara 11, waliona wampate Papa wa mpito atakayekubalika kwa wote wakati hali inaendela kuwa shwari.
Tarehe 9 Oktoba 1958 katika kura ya 12, walimchagua Kardinali Angelo Roncalli, mwenye umri wa miaka 76, mtu asiyekuwa na misimamo mikali, lakini mtu wa watu na Mwanadiplomasia mzuri katika kuleta mahusiano na watu.
Alichagua jina la Yohana XXIII. Mfano wa maisha yake na mtu ambaye alitaka kufuata nyayo zake alikuwa Mtakatifu Papa Pio X (1903-1914: wa 257) ambaye alizaliwa akiwa maskini, na kufa akiwa maskini. Naye kabla ya kuchaguliwa kuwa Papa, alikuwa Patriarka wa Venezia.
Katika hotuba zake za mwanzo, mara moja Papa Yohana XXIII aligusia mambo makuu mawili ambayo alitamani kuyatekeleza. Kwanza kuhuisha Kanisa ili lioane na nyakati, yaani kusoma alama za nyakati kama alivyoiita (Aggionamento).
Alitaka kulihuisha Kanisa kiroho. Pili aligusia kuita Mtaguso Mkuu wa Kanisa kufanya kazi hiyo muhimu. Papa Yohana XXIII alihisi kwamba amevuviwa na Roho Mtakatifu kutengeneza Kanisa na kulihuisha.
Wakati akiamini juu ya Neno la Mungu na Mapokeo rasmi ya Kanisa ambayo ni msingi wa Imani na hayawezi kugeuka, aliona mazoea mengine yaliyoingia kufuatana na utamaduni na mwenendo wa watu wa mahali, au wakati fulani yanaweza na mara nyingine yanapashwa kugeuka kukidhi mahitaji ya wakati na mahali.
Kwanza alianza na desturi za maisha ya Papa. Tofauti na watangulizi wake waliokaa ndani Vatikano, yeye alitoka nje mjini Rona na kwenda kuwatembelea watoto wagonjwa hospitalini, na hata wafungwa.
Alisisitiza kuwaona hata wafungwa sugu na hatari. Aliwaambia wafungwa: “Kwa sababu ninyi hamuwezi kuja kunitembelea, imebidi mimi nije kwenu.” Vile vile alikutana na watu ambao kabla haikufikirika kukutana na Papa kama mpwa wa Rais wa Urusi Nikta Khrushchev, Askofu Mkuu wa Kantebury, yaani Mkuu wa Kanisa la Anglikana, kasisi mkuu wa dini ya Shinto kutoka Japan, na wengine.
Kwa mara ya kwanza katika karne moja, alisafiri nje ya Roma na kwenda Asizi. Alipokutana na watu, hakujiona au kujionyesha kama Kiongozi Mkuu wa Vatikano, bali kama mchungaji au kama alivyosema “Mtumishi wa watumishi” (Servus Servorum), akiwa na sura ya Mchungaji kuliko ya Mtawala.
Papa Yohana XXIII aliliona Kanisa kama chombo cha kiroho kilicho juu ya madaraka yote ya siasa, na chenye jukumu la kuwapatanisha, mathalani wakati wa mzozo wa silaha za nuklia wa Cuba mwaka 1962, ambapo ilikuwepo hatari ya vita vikuu vya mabomu ya nuklia kati ya Urusi na Marekani kutokea.
Papa Yohana XXIII aliingilia kati baina ya John Kennedy wa Marekani na Khrushchev wa Urusi kwa kuzungumza nao, na hivyo akapunguza munkari. Mambo yalipotulia, wote wawili walimshukuru.
Papa Yohana XXIII aliongeza Jopo la Makardinali kiasi kwamba kufikia mwaka 1962, lilikuwa na Makardiali 89, ikiwa 19 zaidi ya wale 70 wa Kanuni iliyowekwa na Papa Sisto IV (1471-1484: wa 212) katika karne ya 15.
Kati ya Makardinali hao, aliwateua wengine kutoka Afrika, Filipino na Japan, licha ya Marekani na nchi nyingine. Kati ya Makardinali alimteua Mwafrika wa kwanza na mtu mweusi wa kwanza kuwa katika jopo hili, Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa, Mtanzania kutoka Jimbo la Rutabo, Bukoba, Kagera, Tanganyika wakati huo, mwaka 1959.
Kuna watu ambao hawakuamini kwamba mtu mweusi angelikuwa Kardinali. Ikumbukwe kwamba wakati huo karibu nchi zote za Afrika zilikuwa bado koloni na Marekani mtu mweusi hakuweza kupiga kura na hata kukaa sehemu moja na wazungu, kwani alitengwa kama mkoma. Katika uongozi wake, aliwateua Makardinali 54.
Kama Baba Watakatifu waliomtangulia, naye alitoa barua mbalimbali za kichungaji. Tofauti na wengine, barua zake hazikuwa za kulaumu, au za kutoa fasili ngumu za teolojia, bali mambo ya kawaida yenye ladha ya kichungaji yaliyowahusu na kuwagusa watu, bila ubaguzi.
Papa Yohana XXIII aliandika barua nane za kichungaji, na kati ya barua hizo  alizoziandika, mbili zilikuwa na msukumo mkubwa. Mater et Magistra (Kanisa kama Mama na Mwalimu), hii ilikuwa barua ya tano iliyotolewa tarehe 15 Mei 1961 ikiwa ni miaka 70 tangu barua ya Papa Leo XIII (1878-1903: wa 256) Rerum Novarum, na miaka 30 tangu barua ya Papa Pio XI (1922-1939: wa 259) “Quadragesimo Anno.”
Katika barua hiyo iliyosifiwa na kukubalika Ulimwengu mzima, ilijadili masuala ya jamii kama walivyofanya watangulizi wake kwa mtazamo chanya, huria na wa kujenga. Barua maarufu kuliko zote ni ile ya “Pacem in Terris“ (Amani Ulimwenguni) aliyoiandika tarehe 11 Aprili 1963, miezi miwili kabla ya kifo chake Papa Yohana XXIII.
Tofauti na barua nyingine za Baba Watakatifu wengine, Papa Yohanne XX111, aliwaadikia watu wote wenye mapenzi mema. Kweli ilikuwa inawafundisha na kuwaasa watu wa Ulimwengu mzima. Ulikuwa kama wosia wake wa mwisho kwa Ulimwengu.
Barua hii imechambua hali halisi ya kijamii Duniani. Papa Yohana XXIII anatutaka kuheshimu utu wa watu, na anadai kwamba kuheshimu haki za binadamu wote, ndio msingi wa haki na amani ya kweli.
Anaandika “Mwanadamu ana haki ya kuishi. Ana haki ya uadilifu wa mwili na njia zinazohitajika kwa maendeleo sahihi ya maisha, haswa chakula, mavazi, malazi, matibabu, mapumziko na, mwishowe, huduma muhimu za kijamii. Ana haki ya kutunzwa katika hali mbaya ya afya; ulemavu unaotokana na kazi yake; mjane, uzee; kulazimishwa kukosa kazi; au wakati wowote bila kosa lake mwenyewe, ananyimwa njia ya kujikimu.”
Licha ya kusisitiza juu ya utu na usawa wa binadamu, anaasa juu ya haki za wanawake, anawasihi kutoenezwa kwa silaha za nyuklia. Anafundisha juu ya umuhimu wa Umoja wa Mataifa kwa ajili ya kuwaleta watu wote pamoja, kujadili na kuleta muafaka juu ya kutatua mafarakano na kuleta maendeleo ya kweli kwa watu wote.
Bahati nzuri, tafsiri ya barua hii iko katika Kiswhili, na inapatikana kwenye mtandao wa Vatikano.

Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita tuliwaletea Kuibuka kwa Kanisa la Misioni Katika Karne ya 20 Sehemu ya Pili. Leo tunawaletea historia jinsi Papa Pio XI kama mwalimu na Mwanadiplomasia, alivyopambana na madikteta na Ukomunisti dhidi ya Kanisa. Sasa endelea…

Kipindi kati ya vita Kuu ya Kwanza na Vita Kuu ya Pili (1918-1939), kilijaa hali ya kutoelewana na serikali, kwa sababu hazikuwa na msimamo thabiti. Kwa upande mmoja, kulikuwa na wale waliopenda demokrasia isiyo na kipimo, ambayo ilipinga hata maadili ya dini kama kandamizi.
Kwa upande mwingine, kulikuwa na udikteta ambao mtu au kundi la watu walitaka kuunda serikali yenye madaraka yote, bila kuingiza mawazo au ushiriki wa wananchi.
Kazi ya kwanza aliyoifanya Papa Pio XI ni kuleta amani na uelewano kati ya serikali ya Italia, na kanisa. Mwaka 1929 aliweza, baada ya majadiliano marefu, kufikia muafaka na serikali ya Italia juu ya nafasi ya Papa kama mtawala huru wa nchi huru ya Vatikano.
Hii ilikuwa hatua kubwa sana.  Alijitahidi kufikia makubaliano na nchi nyingine ambayo yalilinda haki na uhuru wa Kanisa.
Upinzani dhidi ya Udikteta:
Ingawa Papa Pio XI alifikia mapatano na nchi mbalimbali, hili halikumzuia kupinga majaribio ya kuwafanya watawala kuwa miungu, au kufanya serikali kuwa juu ya maadili ya Mungu.
Papa Pio XI anajulikana sana kwa kuweka nguvu zake nyingi katika kuunda “Actio Catolica,” yaani kwetu iliitwa “Aksio Katolika“. Kwa kuunda Aksio Katolika, alikuwa anasisitiza kwamba ni jukumu la walei kushiriki katika kazi ya hierakia ya uinjilishaji.
Hivyo, vyama vya Aksio Katolika, tofauti na vyama vingine vya sala na kujitakatifuza, vilipaswa kutoka nje na kuinjilisha, kuimarisha maadili ya jamii na kuleta uongozi bora wenye sura ya Kikristu katika kila nyanja.
Wana Aksio Katolika kama chama, hawakuingilia siasa ya vyama, ilibidi wawe juu ya vyama, lakini binafsi walihamasishwa kushiriki katika siasa na kuifanya iwe nzuri na takatifu.
Aksio Katolika ilitengeneza waamini walei wenye imani kubwa na nguvu za kutetea imani na Kanisa lao ulimwenguni kote. Kwa sababu hiyo, viongozi wa serikali waliovunja maadili, hawakuwapenda.
Vugu vugu hili lilienea hata mpaka Nchi za Misioni. Tanzania waliitwa “Aksio Katolika” au Waaksio nao walikuwa watu wenye uwezo, na hata mara nyingine walivaa kama Wamisionari na kuongoza Makanisa yaliyokuwa mbali na Wamisionari.
Wengine walitumwa katika sehemu ambazo Wamisionari walikuwa bado kufika, watayarishe watu kupokea imani. Katika siku zetu, vyama kama Wanataaluma Wakatoliki (Catholic Professionals of Tanzania: CPT) wanaoaswa kufanya kazi, ambayo ilikuwa inafanywa na wana Aksio Katolika.
Wakati huo, nchi nyingi zilianza kuingia udikiteta. Watawala madikteta kundi la kwanza ambalo walilipiga vita likikuwa lile la Aksio Katolika kwa sababu walikuwa na nguvu, na hawakuyumba katika imani yao. Walishtakiwa kupokea maagizo kutoka kwa Papa dhidi ya serikali.
Papa Pio XI aliandika barua 31 za kichungaji juu ya mambo mbalimbali. Kati ya hizo, barua tatu zilikuwa na uzito mkubwa kwa sababu aliongelea juu ya hali ya kisiasa, na hasa juu ya unyanyasaji wa wana Aksio Katolika na vyama vingine, hasa vile vya watoto na vijjana au‚ Vijana Wakatoliki.
Italia chini ya uongozi wa Musolini:
Wakati wa Vita Kuu ya Kwanza, Musolini akiwa na chama kidogo cha mafashisti, alisaidia Italia kuingia katika vita dhidi ya Ujerumani. Baada ya ushindi alilalamika kwamba katika makubalinao ya Versailles, Italia haikupewa ardhi ilizotaka.
Kwa namna hiyo, alitumia utaifa wa Waitaliani na ari waliyoipata wakati wakiwa katika harakati ya kuunganisha Italia, kusema kwamba kuna Waitaliani ambao bado ni mateka katika nchi nyingine, hivyo sehemu zote wanakoishi Waitaliani zinapashwa kuunganishwa na Italia.
Pole pole alitumia malalamiko ya watu juu ya hali mbaya ya uchumi, na hivyo kuunda kikosi cha wanamgambo wafashisti. Mwaka 1922 kikundi hiki kiliingia na kuvamia Roma na kuipindua serikali, na Musolini akawa Waziri Mkuu.
Akiwa madarakani, alitumia kigezo cha utaifa kuvamia nchi kama Ethiopia, ili nao wawe na koloni. Vile vile, alivamia Albania akisema ni sehemu ya Italia. Alipenda kuvamia na kuchukua sehemu nyingine zilizokuwa kando ya Italia.
Ufashisti ni nini?
Ufashisti ni aina ya serikali iliyojumuisha mfumo wa kimabavu na serikali ya uzalendo  kitaifa pamoja na kushirikisha jamii kwa kuwarubuni kiakili kwa mikutano mikubwa na kampeni.
Ni serikali ambayo dikteta au mfalme anaidhibiti serikali, watu wanaotawaliwa inabidi kufuata maagizo ya dikteta wao, la sivyo, wataadhibiwa. Pole pole alichukua madaraka yote.
Mwanzoni alitaka kuwa na amani na Kanisa Katoliki, akijua kwamba lina nguvu. Hii ndiyo sababu aliweza kufikia Makubaliano ya Laterano yaliyounda Nchi ya Vatikano. Lakin siku zilivyoendelea, alianza kupiga vita mafundisho ya Dini yaliyoendana tofauti na mawazo yake.
Alipiga marufuku vyama vya Walei Wakristo. Mfalme Emmanuel III wa Italia alibaki kuwepo bila madaraka. Musolini alijiita “Il Duce” maanake “Kiongozi Mkuu.”
Kwa kupinga hayo yote, Papa Pio XI tarehe 21 Juni 1931, aliandika barua kwa lugha ya Kiitaliano, tofauti na barua nyingine ambazo zilikuwa katika Kilatini, ikiitwa, “Non Abbiami Bisogno“ ikimaanisha “Hatuwahitaji.”
Barua hii ilikuwa inampinga Musolini ambaye alikuwa amefanya serikali itukuzwe sana. Musolini alikuwa ameunda serikali ya kifashisti ambayo ilikuwa serikali ya kidikteta, ambayo ilitaka kutawala kila sehemu.
Musolini alikuwa amepiga marufuku chama cha “Aksio Katolika“ na vikundi na vyama vyote vya watoto na vijana. Musolini alitaka awe na ukiritimba wa elimu ya watoto na vijana na pasiwepo na chama chenye kuhamasisha watu.
Papa Pio XI alikiona chama cha Musolini kama “ibada ya kipagani ya Serikali” (kuabudu Serikali) na “mapinduzi ambayo huwanyakua vijana kutoka kwa Kanisa na kutoka kwa Yesu Kristo, na ambayo hukazia kuingiza ndani ya vijana hao moyo wa chuki, jeuri na ukosefu wa heshima.”
Papa Pio XI alimwita Musolini mpinga Dini, na kwamba sera yake  haiendani na mafundisho ya Kanisa.  Mwanzoni itikadi ya Musolini haikuwa mbaya sana, lakini tangu Mei 1938 Hitler alipotembelea Roma na pamoja wakaunda umoja wa ushrikiano (Axis), mambo yalibadilika. Musolini akaanza kuiga sera za Hitler za Ujerumani, mfano mmojawapo ni ule wa kuwakandamiza, hata kuwaua Wayahudi.

Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliwaletea Historia ya Dini ilivyokuwa wakati wa Mapinduzi ya Viwanda (Industrial Revolution) barani Ulaya. Leo tunawaletea Misingi na Haki ya Mafundisho ya Kijamii ya Kanisa. Sasa endelea…

Mwaka 1967 Papa Paulo VI (1963-1978: wa 262) alitoa barua yake ya Kichungaji “Populorum Progressio,” yaani ‘Maendeleo ya Binadamu’. Licha ya mengine, alisisitiza kwamba hakuna maendeleo ya kweli, kama siyo ya binadamu wote.
Anasisitiza juu ya wajibu wa mataifa tajiri kusaidia yale maskini. Wakati wa kuadhimisha miaka 80 tangu itolewe barua ya Rerum Novarum Mei mwaka 1891, Papa Paulo VI alitoa barua ya Kitume mwezi Mei 1971 “Octogesima Adveniens”, yaani ”Ujio wa Miaka Themanini”.
Katika barua hiyo, aliongelea hasa hali duni katika miji. Tarehe 26 Oktoba 1975 alitoa barua nyingine ya “Evangelii Nuntiandi”, yaani “Utangazaji wa Injili”, ikiadhimisha miaka 10 ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano (1962-1965), alisisitiza kwamba kazi ya Kanisa ni kupigana dhidi ya uonevu na udhalilishaji.
Papa Yohana Paulo II (1978-2005: wa 264) alitoa barua mbili kukazia mafundisho hayo ya Kanisa juu ya jamii. Mwaka 1981 ikiwa miaka 90 tangu barua ya Rerum Novarum, aliandika barua ya kitume ya “Laborem Exercens” akisisitiza kwamba haki binafsi ya kuwa na mali haipashwi kuathiri umma, yaani haki ya wote kuwa na mali au kukiuka haki za jamii.
Papa Yohana Paulo II alirudia mawazo hayo kwa mkazo zaidi, hasa akikosoa ubepari uliopindukia, na ujamaa hasi katika barua yake nyingine ya kitume “Centesimus Annus” ya mwaka 1991, akiadhimisha miaka 100 ya Rerum Novarum.
Kwa namna hii, unaonekana umuhimu wa barua ya Papa Leo XIII (1878-1903: 256) iliyolitoa Kanisa katika makucha ya mabepari bila kuiingiza katika utumwa wa wajamaa hasi, au ukomunisti. Kabla Papa Yohana Paulo II hajafariki mwaka 2005. ulitolewa muhtasari (Compendium) ya Mafundisho ya Kanisa juu ya jamii.
Papa Benedikto XVI (2005 -2013: wa 265) akifuata katika nyayo za watangulizi wake, mwaka 2009 alitoa barua ya Kitume “Caritas in Veritate”, yaani “Upendo katika Ukweli”.
Licha ya kusisitiza yale yaliyosemwa na watangulizi wake, pia aliisifu hasa barua ya kitume ya Papa Paulo VI ya mwaka 1967” Populorum Progressio” kwa kuongelea, siyo tu juu ya maslahi ya wafanyakazi, bali pia juu ya maendeleo ya binadamu mzima (Integral Developoment).
Papa Benedikto XVI alikosoa sana ubepari, akiuona kukosa utu na kuwa na ubinafsi wa kujitafutia faida kutoka kwa wengine bila kuona wajibu wa kurudisha vilevile kwa jamii. Alisisitiza juu ya haki za jamii kuzidi haki za mtu binafsi kupata faida. Alilaumu ubepari kwa madhara ya siki hizi, yakiwemo vilevile balaa la madawa ya kulevya.
Papa Fransisko (wa sasa: 2013: wa 266), mafundisho yake yote ni juu ya upendo na kujali. Mwaka 2016 alitangaza mwaka wa Huruma ya Mungu na Upatanisho. Mafundisho yote ya wakati huo yalikuwa Mungu atakuhurumia, nawe ukiwahurumia wengine.
“Kuweni na Huruma kama Baba yenu wa Mbunguni alivyo na Huruma.” Katika barua yake ya Kitume “Evangelium Gauduim” au “Furaha ya Injili” ya mwaka 2013, anasihi serikali mbalimbali na vyombo vya kimataifa vya fedha kuhakikisha kuwa watu wanapata haki za msingi, yaani kazi, afya na elimu.
Anakubali haki ya serikali kuingilia uchumi kwa wema wa umma. Anapinga utamaduni wa kuabudu fedha na kuacha soko huria kwa faida ya wachache, wakati wengi wanakuwa fukara. Analaami utofauti unaoongezeka kati ya walionacho na wasionacho.
Katika barua nyingine ya Kitume ya mwaka 2015 “Laudato Si”, ambayo ilipokelewa vizuri sana na watu wa rika na Imani mbalimbali, anaongelea siyo tu juu ya haki ya wanyonge, bali na ulazima wa kutunza mazingira, na kulaani matumizi mabaya ya nyenzo za dunia kwa sababu ya ulafi.
Aliongeza barua nyingine mbili akisisitiza juu ya upendo na kujali; “Gaudete et Exultate” yaani “Furahini na Kushangilia” ya mwaka 2018 na “Fratelli Tutti”, yaani “Sote ni Ndugu”, ya mwaka 2020.
Kanisa katika mafundisho yake ya kijamii katika miaka hii yote, imesisitiza juu ya mambo yafuatayo:

1.    Haki ya Uhai:
    Maisha ya binadamu ni matakatifu tangu kutungwa mimba hadi kifo. Kila binadamu siyo tu ana haki ya kuishi, bali pia ana haki ya kupata heshima. Katika mafundisho yake yote, Kanisa linasisitiza kwamba kila binadamu ameumbwa katika sura ya Mungu, na watu wote wana haki sawa mbele ya Mungu, na hivyo wanastahili heshima.

2.    Auni (Subsidiarity):
    Hii ilisisitizwa hasa kuanzia na barua ya Papa Pio XI ya Quadragesimo Anno mwaka 1931. Madaraka ya juu yasichukue kile ambacho madaraka ya chini yanaweza, na yana haki nacho. Mkubwa asaidie kile ambacho mdogo hawezi peke yake kufanya, la sivyo unamnyang’anya heshima na juhudi zake.

3.    Mshikamamno na kufanya juhudi kwa wema wa wote (Common Good):
    Watu hatuko kisiwa, hivyo lazima kusaidiana kama binafsi, kama junuiya, na kama mataifa.

4.    Upendo ndio upeo wa yote:
    Hapa siyo upendo wa kihisia, bali ni upendo wa kweli wa kujitoa kwa ajili ya wengine.
    Hayo maagizo manne yanakuwa msingi wa haki na wajibu katika Mafundisho ya Kanisa juu ya jamii kama haki ya kupata kazi; haki ya familia; haki ya uhuru wa kuabudu na kuwasiliana; utunzaji wa mazingira; haki ya kuwa na mali binafsi; kujali maskini; na wasiojiweza.

Dar es Salaam

Na Edvesta Tarimo

Juni 14 kila mwaka, nchi mbalimbali Duniani huadhimisha Siku ya Wachangia Damu Duniani (World Blood Donor Day: WBDD).
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (World Health Organisation: WHO), kila mwaka watu takribani milioni 92 ni wachangiaji wa damu, asilimia 50 ya watu hao wanatoka katika nchi zinazoendelea, ambao wanafanya asilimi 15 tu ya watu wote Duniani.
Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu akiwasilisha hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 mwanzoni mwa mwezi Mei mwaka 2023, katika hotuba hiyo kuimarisha upatikanaji na udhibiti wa dawa, vifaa tiba, vitendanishi, na damu salama, ni baadhi ya maeneo yaliyopewa vipaumbele katika wizara hiyo.
Shirika la Afya Duniani (World Health Organisation: WHO), linasema kuwa upatikanaji wa damu salama ni sehemu ya utekelezaji wa lengo la huduma za afya kwa wote, lakini pia ni kipengele muhimu katika utendaji kazi wa mifumo ya afya kote Duniani.
Siku ya Wachangiaji Damu Duniani huadhimishwa kwa kutambua na kuenzi siku ambayo alizaliwa mvumbuzi wa makundi ya damu A, B, na O (ABO blood group system), huko New York, Marekani mwaka 1943, ni raia wa Austria, Dk. Karl Landsteiner aliyezaliwa Vienna mwaka 1868.
Daktari huyo alikuwa ni mtafiti Vienna, Austria, na tangu mwaka 1922 alihamia katika taasisi ya Rockefeller ya Utafiti wa Matibabu huko New York, Marekani. Mwaka 1900 uhamisho wa damu ulikuwa umefanyika kwa zaidi ya karne mbili kabla, bila kufikia matokeo mazuri.
Mwaka 1901, daktari wa Austria, Karl Landsteiner alipindua Ulimwengu wa Uhamisho wa Damu kutokana na ugunduzi wa mfumo wa makundi ya damu ABO, na mwaka 1930 alipewa tuzo ya Nobel ya Dawa. Aliunganisha jina lake la ugunduzi wa makundi ya damu ABO na kipengele cha Rh na A.
Daktari Landsteiner ni mwandishi wa ripoti za tafiti mbalimbali, umuhimu msingi wa majaribio ya magonjwa, juu ya hemoglobinuria baridi, juu ya maambukizi makubwa na majaribio ya tafiti nyingine nyingi kuhusiana na damu.
Nchini Tanzania, Mpango wa Taifa wa Damu Salama Tanzania (National Blood Transfusion Service: NBTS), ulianza kuadhimishwa rasmi hapa nchini mwaka 2004, ingawa ulianza takribani katika miaka ya 1950.
Uchangiaji Damu kwa Hiari
Tanzania ni miongoni mwa nchi wanachama, hivyo kila ifikapo tarehe 14 Juni ya kila mwaka, huungana na Shirika la Afya Duniani (World Health Organization: WHO), na nchi wanachama kuwatambua, kuwashukuru, kuongeza uelewa na kuleta hamasa kwa wachangiaji, ili waendelee kuchangia damu, na wale ambao hawajawahi kuchangia damu, wajitokeze kuchangia.
Zaidi ya aslimia 70 ya idadi ya Watanzania ni vijana wa chini ya umri wa miaka 35, hii ni kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022. Kundi hili pia linatajwa kuwa nguzo muhimu katika uchangiaji damu kwa hiari.
Kijana Fredy Mavika ni mdau na balozi wa kuchangia damu, anasema kuwa ameshachangia damu zaidi ya mara 9, na ameanza tangu akiwa shule ya sekondari, mpaka sasa.
Akizungumza na mwandishi wa makala hii katika Hospitali ya Lugalo kitengo cha kuchangia damu jijini Dar es Salaam, anasema kuwa hawana elimu ya uchangiaji damu, kitu ambacho kwake anaona ipo sababu ya mtu binafsi kutambua mchakato wa uchangiaji damu.
Mavika anabainisha kuwa tangu alipoanza kuchangia damu, hajawahi kusikia utofauti wa kiafya kama ambavyo baadhi ya watu katika jamii wamejenga dhana potofu kwamba damu inaisha mwilini, na mtu hupata kizunguzungu.
Mavika anawasihi vijana na Watanzania kwa ujumla, kujitokeza kuchangia damu kwa hiari, kwani endapo utachangia damu zaidi ya mara tatu, ikitokea unauguliwa na mgonjwa anayehitaji kupata damu, kadi yako itatumika ili kupata huduma hiyo.
Faida za Kuchangia Damu kwa Hiari
Sadaka siyo lazima iwe fedha, hata hili la kuchangia damu ni kujisadaka kwa ajili ya wengine, ni sadaka ambayo ni hazina isiyotiwa kutu, wala kuliwa na mchwa.
Wataalamu wa afya wanasema kwamba mwanadamu pekee ndiye anayeweza kuchangia damu kwa ajili ya wahitaji wa damu, kwani haiwezekani kuunda damu katika maabara yoyote kuokoa maisha ya mwanadamu, hivyo utoaji damu kwa hiari, ndiko kutakakowezesha kuwakidhi wenye uhitaji huo.
Katika uchangiaji damu huo, baada ya kuwa mwanachama wa kuchangia damu, mwanaume anaweza kuchangia mara nne, na mwanamke mara tatu katika mwaka.
Afisa Mhamasishaji Msaidizi Kitengo cha Damu Salama,  Elizabeth Msemwa anafafanua kuwa licha ya kwamba kuchangia damu ni ishara ya upendo, pia zipo faida lukuki na chanya za kiafya ambazo mchangiaji wa damu anazipata bure pindi anapofanya tendo hilo la hiari, na la upendo kwa wengine.
Anabainisha kuwa mchangia damu anapata vipimo maalum ambapo pia katika utoaji damu inawezekana kugundua pia ugonjwa mapema unaoanza kuunyemelea mwili wake, na hivyo kuanza matibabu mapema.
Dhana potofu dhidi ya Kuchangia Damu
Waswahili walinena, “Jambo usilolijua, ni kama usiku wa giza,” “Asiyejua maana, usimwambie maana, maana atapoteza maana, kama si kuharibu kabisa,” na, “Tatizo lisikie kwa mwingine, usiombe likakufika.”
Pengine baadhi ya watu katika jamii huogopa kwenda kuchangia damu kwa kuogopa maneno ya wenzao, ama hawana elimu sahihi kuhusu kuchangia damu kwa hiari.
Siku moja alisikika mtu akisema, “Ukishachangia damu, baada ya muda fulani usipokwenda kuchangia tena, itakuletea shida.” Wengine hujisemea, “Nichangie damu ya nini wakati sipati chochote, na damu yenyewe kwanza inauzwa?”
Elizabeth anakata mzizi huo kwa kusema kuwa hizo ni dhana potofu, na kwamba mchangiaji anapofika kituoni, kwanza anapewa elimu kuhusu kuchangia damu, anafanyiwa vipimo likiwemo suala la kuangalia uzito, kiwango cha damu aliyonayo kabla ya kuanza kutolewa damu.
Anaongeza kuwa endapo mchangiaji damu anakuwa hajakidhi vigezo vinavyotakiwa, hatachangia damu. Na endapo pia atakuwa chini ya umri wa miaka 18 au ni mjamzito, hawataruhusiwa kuchangia, hata kama vigezo vingine vimekidhi.
Aidha, Afisa huyo anaongeza kuwa baadhi ya watu katika jamii wanashindwa kutambua kuwa,wanapochangia damu kwa ajili ya kuwaongezea wengine, au mgonjwa haitumii damu hiyo ambayo imetolewa muda huo, bali inachukuliwa nyingine kwenye benki ya damu, kisha ikishachakatwa, inarejeshwa kwa ajili ya wahitaji wengine.
“Labda niseme kwamba watu wanadhani damu inapotolewa, mgonjwa anawekewa muda huo huo, la hasha. Damu lazima ipitie uchakatwaji. Huwezi kutoa na ikatiliwa mwingine hivi hivi tu,” anasema Afisa Elizabeth.
Elimu ya Kuchangia Damu kwa Hiari
Judith Charle, Msimamizi wa huduma za wachangiaji damu kutoka Mpango wa Taifa wa Damu Salama Makao Makuu, anasema kuwa timu za ukusanyaji damu huelimisha jamii kuhusu suala la kuchangia damu kupitia vyombo mbalimbali vya habari.
Anaongeza kwa kusema kuwa wanaendesha kampeni ya uchangiaji damu katika sehemu mbalimbali, mathalan kwenye Vituo vya Kanda, Vituo vya Damu Salama vya Hospitali za Rufaa za Kanda, Hospitali za Rufaa za Mikoa, na Hospitali za Wilaya zote nchini, ili kuleta mwamko kwa jamii kuhusu uhitaji wa zao hilo.
Anaongeza pia kuwa wanatumia Siku ya Wachangiaji Damu Duniani, Juni 14, kuwashukuru, kuongeza uelewa, na kuleta hamasa kwa wachangiaji ili waendelee kuchangia damu, na wale ambao hawajawahi kuchangia damu, wajitokeza kuchangia.
Uchangiaji damu umeendelea kuongezeka, kwani mwamko ni mkubwa, na uelewa pia unaongezeka, kwa sababu mwitikio wa uchangiaji damu kwa hiari kadri miaka inavyokwenda, ndivyo unavyozidi kuongezeka, na dhana nzima ya uchangiaji damu pia inaongezeka.
Uhitaji wa Damu Nchini Tanzania
Dokta Judith Charle aliliambia Tumaini Letu kuwa kulingana na Shirika la Afya Duniani, (World Health Organization: WHO), mahitaji ya damu ya nchi husika ni aslimia 1 ya wingi wa watu.
Anasema kuwa mahitaji ya damu salama ni takribani chupa laki 5 na elfu 90 (590,000) kwa mwaka kulingana na Shirika la Afya Duniani.
Aidha, anaongeza kuwa kwa sasa hawajaweza kufikia mahitaji kwa sababu ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022, na kwamba kabla ya hapo Watanzania walikuwa takribani milioni 50 hadi 55, kwa hiyo mahitaji ya damu walilenga kukusanya chupa laki 5 hadi 5 na nusu (500,000 hadi 550,000) za damu salama.
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika mwaka 2022, Tanzania ina watu 61,741,120, huku Bara ikiwa na watu 59,851,357, na Zanzibar watu 1,886,773.
Dokta Charle anasema kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/2024 na Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022, wameweka malengo ya kukusanya chupa laki 5 hadi 5 na nusu za damu salama.
Wito kwa Jamii wa Kuchangia Damu kwa Hiari
Dk. Judith Charle anaiasa jamii kuona umuhimu wa kuchangia damu kwa hiari, ili kuweza kuwasaidia Watanzania ambao wanahitaji huduma ya damu katika hospitali mbalimbali.
Aliwasihi kutembelea Vituo vya Mpango wa Taifa wa Damu Salama ambavyo vipo katika ngazi ya Kanda, Mkoa, Hospitali za Rufaa za Kanda, Hospitali za Taifa, na Hospitali zote za Halmashauri nchini, ambapo Vituo vya Uchangiaji Damu vinapatikana.
Hakuna mbadala wa damu, mgonjwa anapohitaji huduma ya damu anahitaji damu ya kutoka kwa binadamu mwenzake ili kuweza kumwongezea, na damu lazima iandaliwe ili pale dharura ya kumwongezea mgonjwa damu inapotokea, damu hiyo iwe tayari ili kuweza kuokoa vifo vinavyotokana na upungufu wa damu katika hospitali mbalimbali nchini.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Kila Wiki ya Ugavi wa Damu wa Kundi O ya AABB (Association for the Advancement of Blood and Biotherapies), ambayo ni Chama cha Kuendeleza Damu na Tiba Viumbe iliyotolewa mwishoni mwa mwezi Mei mwaka 2023, inasema kuwa uchangiaji wa damu unahitajika ili kuhakikisha upatikanaji wa damu.
Chama cha kuendeleza Damu na Tiba viumbe (Association for the Advancement of Blood and Biotherapies: AABB) inawahimiza wale wanaostahili kuchangia damu mara kwa mara, ili kuhakikisha kwamba nyenzo hiyo muhimu ya kuokoa uhai, inapatikana kwa wagonjwa wanaohitaji.
Kaulimbiu ya Kimataifa ya Siku ya Wachangia Damu Duniani, hubadilika kila mwaka kwa kutambua watu waliojitoa kuchangia damu yao kwa watu wengine wasiowafahamu.
Kwa maana hiyo, tuunganishe nguvu zetu pamoja kwa ajili ya kujitokeza kuunga mkono suala la uchangiaji damu kwa hiari, ili kuokoa maisha ya watu.
Karibu katika ‘group’ la WhatsApp la kuchangia damu kwa hiari la Marafiki wa Vijana Club, kipindi kinachoruka kupitia Tumaini Televisheni. Changia damu, okoa maisha, wasiliana na ‘group’ la WhatsApp +255 713 062 953.

KAYANGA

Na Angela Kibwana

Jimbo Katoliki la Kayanga ni mojawapo kati ya Majimbo 34 ya Kanisa Katoliki nchini Tanzania, ambalo limo katika Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza.
Jimbo hili linaundwa na wilaya mbili ambazo ni wilaya za Karagwe na Cherwa. Upande wa kaskazini linapakana na Uganda-Jimbo Kuu Katoliki la Mbarara. Upande wa Magharibi linapakana na Rwanda, na upande wa Mashariki linapakana na Wilaya ya Misenyi na kusini linapakana na wilaya ya Ngara nchini Tanzania.
Jimbo Katoliki la Kayanga lilitangazwa rasmi na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedict XVI Agosti 14 mwaka 2008, ambalo lilimegwa kutoka Jimbo Katoliki la Rulenge – Ngara, na hatimaye kuzaliwa majimbo mapya mawili, yaani Jimbo Katoliki la Rulenge – Ngara, na Jimbo Katoliki la Kayanga.
Kunako mwaka 1929 ilianzishwa  Apostolic Vicariate ya Rulenge-Ngara kutokana na Apostolic Vicariate ya Tabora, ambapo Machi 25  mwaka 1953 Rulenge ilitangazwa kuwa Dayosisi. Hivyo, tarehe 14 Agosti 2008, ikamegwa Dayosisi ya Rulenge na hivyo kuanzishwa Jimbo Katoliki jipya la Kayanga.
Jimbo Katoliki la Kayanga lilizinduliwa Novemba 06 mwaka 2008, ambapo Askofu Almachius Vincent Rweyongeza aliwekwa wakfu akiwa Askofu wa kwanza wa jimbo hilo lenye kilomita za mraba 70,716 likiwa na wakazi zaidi ya laki 6, Wakatoliki wakiwa ni asilimia 60 Jimboni humo, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012.
Jimbo Katoliki la Kayanga lilianzishwa likiwa na Mapadri 24, hivyo kwa wastani, kila Padri mmojawao anahudumia waamini 11,200 katika Parokia 11 ilivyokuwa katika mwaka wa 2008, idadi ya watawa wa kike walikuwa 61 wa Shirika la Kijimbo.
Katika muktadha huo, Mhashamu Askofu Almachius Rweyongeza wa Jimbo Katoliki la Kayanga anamshukuru Mungu kwa mafanikio ya kiroho yaliyopatikana Jimboni humo, hasa ongezeko la Mapadre, Watawa wa kike, na Makatekesta ambao wamekuwa chachu ya kuimarisha katekesi kwa waamini.
Anabainisha kuwa hadi sasa Jimbo hilo lina jumla ya Mapadre 51, Watawa 94 wa kike, na ongezeko la Makatekesta kutoka 398 katika kipindi cha mwaka 2008, na kufikisha idadi ya Makatekesta 438 kwa mwaka 2022.
Aidha, alisema kuwa kwa kipindi cha miaka 14 tangu kuanza kwa Jimbo hilo kunako mwaka 2008 hadi mwaka huu 2022, kumekuwa na ongezeko kubwa la wahudumu, hasa Mapadre na miito ya Upadre, ambapo kwa mwaka huu amewapatia Daraja Takatifu Mapadre wapya watatu, na kufikisha idadi ya Mapadre 51 jimboni humo.
Hata hivyo ametaja pia mafanikio mengine, hasa ongezeko la familia za Kikatoliki kupitia Sakramenti ya Ndoa Takatifu, hali iliyosaidia kupunguza ndoa za mseto, uchumba sugu, ndoa mgando, ndoa za mitala, pamoja na kupungua kwa ndoa za kiserikali.
Miongoni mwa mafanikio mengine jimboni humo ni ongezeko la Jumuiya Ndogo Ndogo za Kikristo kutoka Jumuiya 1,039 hadi kufikia Jumuiya 1657, pamoja na uwepo wa Vituo vya Hija ambavyo amevitaja kuwa ni ‘Zahanati za Kiroho’ kwa ajili ya kutibu mahangaiko ya waamini.
Alisema kuwa wakati jimbo linazinduliwa lilikuwa na Parokia 11 tu, Vigango 234, Jumuiya za Kikristu 1,039 na Mapadre 24, Masista wa Jimbo 61 wa Shirika la Mitume wa Upendo, Upendo ambalo ndilo Shirika la Jimbo Katoliki la Kayanga, wakiwamo Makatekesta 398.
“Wahenga wetu wamesema ‘daima mwanzo ni mgumu’, ugumu huu ulitokana na shida za kiuchumi, hasa kuweka miundombinu ya msingi ya kichungaji na kijamii.
Namshukuru Mungu wakati jimbo linazinduliwa, Kanisa Kuu la Mtakatifu George, Kayanga, lilishajengwa na kutabarukiwa na Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki la Rulenge - Ngara, Septemba 1, 2008, siku tano kabla ya kuzinduliwa kwa Jimbo Katoliki la Kayanga” alisema Askofu huyo.
Askofu Rweyongeza anasema kwamba alipokabidhiwa Jimbo la Kayanga hakuwa na uzoefu wowote wa kuzindua jimbo, hakuwa na ujanja wala mbinu za kuongoza jimbo hilo. Hivyo, aliandika katika Ngao yake ya Kiaskofu akijisalimisha kwa Bwana kwa kutumia maneno yasemayo: “Mimi ni Mtumishi wa Bwana.”
“Nilijisalimisha kwa Mungu kwa kutumia maneno ya Bikira Maria. Nilimkabidhi yote Mungu kwa sababu Mwenyezi Mungu asipojenga Jimbo Katoliki la Kayanga, wajengao wanajisumbua bure, nami nikiwa mmojawapo. Kusema kweli, Mwenyezi Mungu amenitendea makuu kwa kipindi cha miaka 14, kwani nimeshuhudia mafanikio makubwa,” alisema Askofu Rweyongeza.
Anasema vile vile kuwa licha ya idadi ndogo ya Mapadri wanaotoa huduma za kiroho Jimboni humo, anashukuru pia mchango wa Makatekesta ambao ni wasaidizi wa karibu wa Mapadre, hasa Vigangoni na Vijijini, kwa sababu Parokia moja inakuwa na vigango zaidi ya 30 ambavyo vinahudumiwa na Mapadre wawili, hivyo  Makatekesta wanasaidia sana kutoa huduma za kiroho kwa waamini wao.
Anasema kuwa hadi sasa kuna ongezeko la Parokia, kutoka 11 katika kipindi cha mwaka 2008, na sasa imefikia idadi ya Parokia 20 mwaka huu 2022, zenye Mapadre wenye makazi maalumu  katika Parokia hizo.
“Mapadri bado ni wachache kulingana na idadi ya Waamini Jimboni humu, kwani baadhi ya Parokia moja moja anaishi Padre mmoja tu, ambapo inakuwa ni kazi ngumu. Hata hivyo naamini kwamba Mungu ndiye anayeweza kutufanikishia kwa kuwategemeza katika Utume wa Kanisa licha ya uchache wao.”
Mbali na hayo, Askofu Rweyongeza amesifu ongezeko la Vyama vya Kitume Jimboni humo, ambavyo ni uhai wa Kanisa na Jimbo, na alivitaja kuwa ni Utoto Mtakatifu, WAWATA, UWAKA, VIWAWA, Lejio ya Maria, Wafransiskani na vyama vingine vya kitume, ambavyo ni chachu ya mafanikio ya kiroho Jimboni humo.
Amewasifu pia Viongozi wa Halmashauri Walei Katoliki (HAWAKA), ambao ni washiriki wenza katika shughuli za uchungaji ambao umejengwa na viongozi wanaojituma, ili kuhakikisha Jimbo linasonga mbele kiimani.
Sambamba na hayo kwa upande wa taasisi za Dini, ametaja uwepo wa Vituo vya Hija ambavyo ni ‘Zahanati za Kiroho’ zinazosaidia Waamini wengi Wakatoliki na wasio Wakatoliki kwenda kuchota neema na baraka kutoka katika vituo hivyo vya hija na maisha ya kiroho.
“Nilivizindua Vituo hivi vya hija  wakati Jimbo lilipoanza. Nikaona kwamba hili ni hitaji kubwa la kuwasaidia Waamini na jamii kuhusu masuala mbalimbali ya kiroho, kiimani na uponyaji, nikiamini kwamba Vituo hivi vya Hija ni zahanati za kiroho.”
Kalvario Kayungu ni miongoni mwa Vituo vya Hija jimboni humo, kilichozinduliwa septemba 14 mwaka 2011 kwa heshima ya Msalaba Mtakatifu. Pia, kituo kingine cha hija cha Lurd Bughene kilijengwa kwa heshima ya Bikira Maria wa Lurd  na Afya ya Wagonjwa, kikizinduliwa Februari 11, mwaka 2012.
Askofu Rweyongeza anasema kuwa familia ya Mungu Jimboni humo huwa wanafanya hija za kijimbo kila Februari 11, Kitaifa na Kimataifa huko Lurd Bughene katika kuadhimisha sikukuu ya Bikira Maria wa Lurd na Afya ya Wagonjwa. Pia, wanafanya hija za kijimbo, kitaifa na kimataifa huko Kalvario Kayungu kila ifikapo Septemba 14, kwa heshima ya kutukuka  kwa Msalaba.
Licha ya Jimbo hilo kuwa miongoni mwa majimbo machanga nchini Tanzania, limewekeza katika taasisi mbalimbali za jamii, hususan zinazogusia masuala ya Elimu kama vile shule, vituo vya afya hosptatali na zahanati, pamoja na tasisi za mazingira (CHEMA).
“Tuna taasisi muhimu sana Jimboni ijulikananyo kama CHEMA, kifupi cha Community Habitat Environment Management, kama mwitikio kwa Baba Mtakatifu kuhusu barua yake ya kitume ‘Laudato Si’ , inayohusika hasa na utunzanji wa mazingira,” alisema.
Anaeleza kwamba Taasisi ya CHEMA inashughulika na mazingira, kama vile upandaji miti na utengenezaji wa vitalu mbalimbali vya miti mbalimbali ya matunda na miti ya mbao, kivuli na biashara. Pia, ikiwemo utengenezaji wa majiko sanifu yanayotumia kuni kidogo, au majiko yanayotumia unga wa mbao kunusuru uangamizaji wa miti kwa ajili ya kujipatia kuni na mkaa, sanjari na ufugaji wa nyuki.
Wakati huo huo Askofu Rweyongeza anabainisha kwamba uharibifu wa mazingira ni moja kati ya changamoto zinazolikumba Jimbo hilo, hususani uharibifu wa vyanzo vya maji; ukataji wa miti kiholela; uchomaji moto misitu; na utumiaji wa sumu kuua magugu kwa kulima mazao ya muda.
“Jimbo langu limekumbwa na uharibifu wa mazingira, kwani mtu anakata mti wa miaka 30 ili apande mazao ya haraka kujipatia pesa ya haraka, bila kuangalia ni aina gani ya uharibifu wa mazingira anaousababisha.”
Kupitia taasisi ya CHEMA, Askofu Rweyongeza anasema kwamba anahimiza watu waoteshe miti ili kuhakikisha wanatunza uoto uliopo kwa sababu ya uharibifu wa mazingira, kwani ni hatari katika maisha ya binadamu na viumbe vyote.
“Jimbo Katoliki la Kayanga linao msitu wa mfano kuhakikisha kwamba mazingira yanatunzwa, nami namshukuru Mungu nina msitu wangu wa mfano ambao unaitwa bustani ya Edeni, ambako lengo ni kutunza miti ya asili ya matunda ambayo imeshatoweka. Nimepanda miti ya Kibiblia ambayo ni mizeituni, mitende, mitini na mizabibu, ambayo ninayo kwenye shamba langu la ekari 05”.
Itaendelea wiki ijayo.

Page 2 of 2